Zaburi 37 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kufanikiwa kwa waovu kusikufazaishe 1 Zaburi ya Daudi. Usihangaike kwa sababu ya waovu; usiwaonee wivu wanaotenda mabaya. 2 Maana hao watatoweka mara moja kama nyasi; watanyauka kama majani. 3 Umutumainie Yawe na kutenda mazuri, upate kuishi katika inchi na kuwa salama. 4 Uitafute furaha yako kwa Yawe, naye atakujalia unayotamani katika moyo. 5 Umutolee Yawe maisha yako, umutumainie yeye, naye atakufanyia kitu. 6 Ataifanya haki yako iangae kama mwangaza wa jua muchana kati. 7 Tulia mbele ya Yawe, umungojee kwa uvumilivu; usihangaike juu ya wale wanaofanikiwa, ndio watu wanaojaliwa katika mipango yao mibaya. 8 Usiwake hasira wala kuwa na kasirani; usihangaike, maana hiyo inazidisha ubaya. 9 Watu wanaotenda mabaya wataangamizwa, lakini wanaomutumainia Yawe watarizi inchi. 10 Bado kidogo, mwovu atatoweka; utamutafuta pale alipokuwa, wala hautamwona. 11 Lakini wapole watarizi inchi, hao wataifurahia amani kamili. 12 Mwovu anamufanyia mutu wa haki shauri baya, na kumusagia meno kwa chuki. 13 Lakini Yawe anamuchekelea mwovu, kwa maana anajua mwisho wake ni karibu. 14 Waovu wanachomoa panga na kuvuta pinde zao, wapate kuwaua wamasikini na wakosefu; wawachinje watu wenye mwenendo sawa. 15 Lakini panga zao wenyewe zitawapenya mioyo, na pinde zao zitavunjwavunjwa. 16 Afazali mali kidogo ya mutu wa haki kuliko utajiri mwingi wa watu waovu. 17 Maana nguvu za waovu zitavunjwa, lakini Yawe atawaimarisha watu wa haki. 18 Yawe anatunza maisha ya watu wakamilifu, na urizi wao utadumu milele. 19 Hawatafezeheka nyakati mbaya zikiwafikia; siku za njaa watakuwa na chakula tele. 20 Lakini waovu wataangamia, waadui za Yawe watanyauka kama maua katika jangwa; kweli watatoweka kama moshi. 21 Mutu mwovu anakopesha bila kurudisha; lakini mutu wa haki anatoa kwa moyo safi. 22 Waliobarikiwa na Yawe watarizi inchi, lakini waliolaaniwa naye wataongolewa. 23 Yawe anaongoza mutu katika njia yake, anamulinda yule anayemupendeza. 24 Hata akianguka, hatabaki chini, kwa sababu Yawe anamuimarisha. 25 Nilikuwa kijana na sasa mimi ni muzee; hata kidogo sijaona mutu wa haki ameachwa na Mungu, au watoto wake wakiombaomba chakula. 26 Siku zote yeye anakopesha kwa moyo safi, na watoto wake ni wenye baraka. 27 Achana na uovu, utende mazuri, nawe utaishi katika inchi siku zote; 28 maana Yawe anapenda haki, wala hawaachi waaminifu wake. Anawalinda hata milele; lakini wazao wa waovu wataangamizwa. 29 Watu wa haki watarizi inchi, nao wataishi humo milele. 30 Mutu wa haki anasema maneno ya hekima, kwa ulimi wake anasema kufuatana na sheria ya Mungu. 31 Sheria ya Mungu wake ni ndani ya moyo wake, naye hapiti pembeni katika mwenendo wake. 32 Mutu mwovu anamuvizia mutu wa haki, na kujaribu kumwua; 33 lakini Yawe hatamutoa mutu wa haki katika makucha yake, wala kumwachilia aazibiwe anaposhitakiwa. 34 Umutumainie Yawe na kushika njia yake, naye atakuinua uirizi inchi, na kuwaona waovu wakiongolewa. 35 Nilimwona mwovu aliyejivuna sana, akinyanyua shingo juu kama mierezi ya Lebanoni! 36 Kisha nikapita pale, naye hakukuwa tena; nikamutafuta, lakini hakuonekana tena. 37 Muangalie mutu mukamilifu, mutu wa usawa; mutu anayependa amani anajaliwa wazao. 38 Lakini wakosaji wote wataangamizwa; na wazao wao wataongolewa. 39 Yawe anawaokoa watu wa haki, na kuwalinda wakati wa taabu. 40 Yawe anawasaidia na kuwaokoa; anawaopoa kutoka makucha ya waovu na kuwaokoa, maana wanakimbilia kwake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo