Zaburi 29 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Sauti ya Mungu katika zoruba 1 Zaburi ya Daudi. Mumupe Yawe heshima, enyi viumbe vya mbingu, museme kwamba Yawe ni mutukufu na mwenye nguvu. 2 Museme kwamba jina la Yawe ni tukufu. Mumwabudu katika pahali pake patakatifu. 3 Sauti ya Yawe inasikilika juu ya maji; Mungu mutukufu anapiga radi, sauti ya Yawe inasikilika juu ya bahari! 4 Sauti ya Yawe ni yenye nguvu, sauti ya Yawe ni yenye mamlaka. 5 Sauti ya Yawe inavunja miti mikubwa ya mierezi; Yawe anavunja mierezi ya Lebanoni. 6 Anarusha milima ya Lebanoni kama mwana-ngombe, milima ya Hermoni kama mwana-mbogo. 7 Sauti ya Yawe inatokeza ndimi za moto. 8 Sauti ya Yawe inatetemesha jangwa, Yawe anatetemesha jangwa la Kadesi. 9 Sauti ya Yawe inatikisa mivule, inaongoa majani ya miti ya pori, na wote wanaokuwa katika hekalu lake wanasema: “Utukufu kwa Mungu!” 10 Yawe ameikaa juu ya mafuriko ya maji; Yawe ni mufalme anayetawala milele. 11 Yawe awape watu wake nguvu! Yawe awabariki watu wake kwa amani! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo