Zaburi 28 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kuomba musaada 1 Zaburi ya Daudi. Ninakulilia, ee Yawe! Ewe kikingio changu, usikuwe kama kiziwi kwangu. Usikuwe kama haunisikilizi, nisikuwe kama wale wanaoshuka katika shimo la wafu. 2 Sikiliza sauti ya ombi langu, ninapokulilia unisaidie, ninapoinua mikono yangu kuelekea hekalu lako takatifu. 3 Usiniazibu pamoja na watu wabaya, wale watenda maovu wanaosema vizuri na wenzao, kumbe wanajaa ubaya ndani ya moyo. 4 Uwalipe kwa kadiri ya matendo yao, kufuatana na maovu waliyotenda. Uwalipe kwa kadiri ya matendo yao wenyewe; uwatendee yale wanayostahili. 5 Hawashuguliki na matendo ya Yawe; hawatambui mambo aliyofanya. Kwa sababu hiyo atawabomoa, wala hatawajenga tena upya. 6 Atukuzwe Yawe, maana amesikiliza ombi langu. 7 Yawe ndiye nguvu na ngao yangu; tegemeo la moyo wangu ni kwake. Amenisaidia, nami nikashangilia kwa moyo wote; kwa wimbo wangu ninamushukuru. 8 Yawe ni nguvu ya watu wake; yeye ni kimbilio la mufalme aliyemuchagua. 9 Ee Mungu, uwaokoe watu wako; uwabariki watu hao wanaokuwa mali yako. Ukuwe muchungaji wao na kuwalinda milele. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo