Zaburi 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kumwomba Mungu uongozi na ulinzi 1 Zaburi ya Daudi. Ee Yawe, ninakutolea moyo wangu. 2 Ninakutumainia wewe, ee Mungu wangu, usiniache nifezeheke; waadui zangu wasifurahie kushindwa kwangu. 3 Usimwache anayekutumainia kupata haya; lakini wafezeheke wote wanaokuasi kwa makusudi. 4 Unijulishe njia zako, ee Yawe; unifundishe nifuate unayotaka. 5 Uniongoze katika ukweli wako na kunifundisha, kwa maana wewe ni Mungu, mwokozi wangu; ninakutegemea wewe kila siku. 6 Ee Yawe, ukumbuke rehema yako na wema wako ambazo ni za milele. 7 Usikumbuke zambi na makosa ya ujana wangu; unikumbuke kwa kadiri ya wema wako, kwa ajili ya uzuri wako, ee Yawe. 8 Yawe ni muzuri na wa usawa, kwa hiyo anawafundisha wakosaji njia. 9 Anawaongoza wanyenyekevu katika haki; anawafundisha njia yake. 10 Njia zote za Yawe ni njema na za uaminifu kwa wale wanaoshika agano lake na maagizo yake. 11 Kwa ajili ya jina lako, ee Yawe, unisamehe kosa langu, kwa maana ni kubwa. 12 Kila mutu anayemwabudu Yawe, Yawe atamufundisha njia ya kufuata. 13 Mutu wa namna hiyo atafanikiwa siku zote, na wazao wake watarizi inchi. 14 Yawe ni rafiki ya wale wanaomwabudu; yeye anawajulisha agano lake. 15 Ninainua macho kwa Yawe siku zote; yeye ataopoa miguu yangu kutoka mutego. 16 Unielekee, ee Mungu, unionee huruma, maana mimi ni pekee na zaifu. 17 Uniondolee mahangaiko ya moyo wangu; uniondoe katika mashaka yangu. 18 Uangalie mateso yangu na taabu yangu; unisamehe zambi zangu zote. 19 Angalia jinsi waadui zangu wanavyokuwa wengi; ona jinsi wanavyonichukia vikali. 20 Uyalinde maisha yangu, uniokoe; ninakukimbilia wewe, usikubali nifezeheke. 21 Ukamilifu na usawa vinanikinga, maana ninakutumainia wewe. 22 Ee Mungu, uwaokoe watu wako, Israeli; uwaokoe kutoka taabu zao zote. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo