Zaburi 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kilio 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Mutindo wa wimbo “Swala wa mapambazuko”. 2 Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Mbona uko mbali sana kwa kunisaidia, mbali na maneno ya kilio changu? 3 Ee Mungu wangu, ninakulilia muchana lakini haujibu; ninakulalamikia usiku, lakini sipumziki. 4 Hata hivyo, wewe ni mutakatifu; wewe unatawala na kusifiwa na Waisraeli. 5 Babu zetu walikutegemea; walikutegemea, nawe ukawaokoa. 6 Walikulilia wewe, wakaokolewa; walikutegemea, nao hawakufezeheka. 7 Lakini mimi ni mududu tu, wala si mutu; nimetukaniwa na kuzarauliwa na watu. 8 Wote wanaoniona wananichekelea; wananizomea na kutikisa vichwa vyao. 9 Wanasema: “Alimutegemea Yawe, basi, Mungu amuponyeshe! Kama Mungu anapendezwa naye, basi, amwokoe!” 10 Lakini wewe ndiwe uliyenitoa katika tumbo la mama yangu, uliniweka salama kwa kifua cha mama yangu. 11 Nimekutegemea tangu kuzaliwa kwangu. Tangu nilipozaliwa, wewe umekuwa Mungu wangu. 12 Usikae mbali nami, kwa maana taabu imekaribia; wala hakuna wa kunisaidia. 13 Waadui wengi wananizunguka kama ngombe dume; wamenisonga kama ngombe dume wanono wa Basani! 14 Wanafungua vinywa vyao kama simba, tayari kushambulia na kurarua. 15 Nimekwisha kama maji yaliyomwangika; mifupa yangu yote imeteguka; moyo wangu ni kama inta, unayeyuka ndani yangu. 16 Koo langu limekauka kama kigae; ulimi wangu unanata ndani ya kinywa changu. Wewe umenilaza pembeni ya kaburi. 17 Kundi la waovu limenizunguka; wananizunguka kama kundi la imbwa; wamenitoboa mikono na miguu. 18 Nimebaki mifupa mitupu; waadui zangu wananiangalia na kunisimanga. 19 Wanagawanya nguo zangu, na kuipigia kanzu yangu kura. 20 Lakini wewe, ee Yawe, usikae mbali nami. Ukuwe musaada wangu, ukuje haraka kunisaidia. 21 Uokoe nafsi yangu toka upanga, uokoe maisha yangu toka mikono ya imbwa hao! 22 Uniokoe toka kinywa cha simba; uokoe nafsi yangu zaifu toka pembe za mbogo hao. Wimbo wa shukrani 23 Nitawaelezea wandugu zangu matendo yako; nitakusifu kati ya kusanyiko lao, nikisema: 24 “Enyi munaomwabudu Yawe, mumusifu! Mumutukuze, enyi wazao wote wa Yakobo! Mumwogope Mungu, enyi wazao wote wa Israeli! 25 Maana yeye hatupilii au kuzarau taabu ya muzaifu; wala hajifichi mbali naye, lakini anamusikiliza anapomwomba musaada.” 26 Kwa sababu yako ninakusifu katika kusanyiko kubwa la watu; nitatimiza ahadi zangu mbele ya wanaomwabudu. 27 Wamasikini watakula na kushiba; wanaomutafuta Yawe watamusifu. Mungu awajalie waishi milele! 28 Ulimwengu wote utakumbuka na kumurudilia Yawe; jamaa zote za mataifa zitamwabudu. 29 Maana Yawe ni mufalme; yeye anatawala mataifa. 30 Wenye kiburi wote katika dunia watamwabudu; wote ambao ni wa kufa watainama mbele yake, wote ambao hawawezi kudumisha uzima wao. 31 Vizazi vyao vitamutumikia; watu wataelezea kizazi kinachokuja habari za Yawe, 32 watatangazia wale watakaozaliwa matendo yake ya wokovu. Watu wasiozaliwa bado wataambiwa: “Yawe ndiye aliyefanya hayo!” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo