Zaburi 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Shukrani kwa ajili ya ushindi 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. 2 Ee Yawe, mufalme anashangilia kwa nguvu yako, anafurahi sana kwa musaada uliomupa. 3 Umemutimizia mapenzi ya moyo wake; wala haukumukatalia ombi lake. 4 Umemufikia, ukamupatia baraka nzurinzuri; umemuvalisha taji ya zahabu safi juu ya kichwa chake. 5 Alikuomba maisha, nawe ukamupatia; ulimupatia siku nyingi milele na milele. 6 Kwa musaada wako, amepata utukufu sana; wewe umemujalia sifa na heshima. 7 Unamujalia baraka zako siku zote; unamufurahisha kwa sababu uko pamoja naye. 8 Mufalme anamutumainia Yawe; kwa wema wa Mungu Mukubwa atakuwa salama. 9 Mukono wako, ewe mufalme, utawakamata waadui zako wote; mukono wako wa nguvu utawakamata wanaokuchukia. 10 Utakapotokea utawaangamiza kama kwa moto wa furu. Yawe atawamaliza kwa hasira yake, moto utawateketeza kabisa. 11 Utawaangamiza wazao wao watoweke katika dunia; watoto wao hawatabaki kati ya wanadamu. 12 Hata kama wakifanya shauri baya juu yako, kama wakikamata mipango ya udanganyifu, hawataweza kitu hata kidogo. 13 Kwa maana wewe utapiga mishale mbele yao, utawakimbiza mbio. 14 Utukuzwe, ee Yawe, kwa sababu ya nguvu yako! Tutaimba na kusifu kwa ajili ya uwezo wako. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo