Zaburi 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kusifu Mungu juu ya ushindi ( 2 Sam 22.1-51 ) 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi, mutumishi wa Mungu, aliyomwimbia wakati alipomwokoa katika mikono ya Saulo na waadui wengine. 2 Ninakupenda, ee Yawe, nguvu yangu! 3 Yawe ni kikingio changu, kimbilio langu, mukombozi wangu, Mungu wangu, yule ambaye ninamukimbilia, ngao yangu, nguvu ya wokovu wangu, munara wangu. 4 Ninamwita Yawe anayestahili sifa anisaidie, nami ninaokolewa kutoka waadui zangu. 5 Kamba za kifo zilinizunguka, mafuriko ya maangamizi yalinishambulia; 6 kamba za kuzimu zilinizunguka, mitego ya kifo ilikuwa mbele yangu. 7 Katika taabu yangu, nilimwita Yawe; nilimulilia Mungu wangu anisaidie. Toka katika hekalu lake, alisikia sauti yangu; kilio changu kilimufikia katika masikio yake. 8 Halafu dunia ikatetemeka na kutikisika, misingi ya milima ikayumbayumba na kutetemeka, kwa maana Mungu alikuwa amekasirika. 9 Moshi ulifuka kutoka katika pua lake, moto wenye kuteketeza ukatoka katika kinywa chake, makaa ya moto yakatokea. 10 Aliinamisha anga, akashuka chini, na wingu jeusi lilikuwa chini ya miguu yake. 11 Alipanda juu ya kerubi na kuruka, akaruka juu ya mabawa ya upepo. 12 Alijifunika giza pande zote, alijizungushia mawingu mazito ya mvua. 13 Umeme ulimetameta mbele yake; na katika mawingu kukatokea mvua ya mawe na makaa ya moto. 14 Yawe alinguruma kutoka mbingu; Mungu Mukubwa akatoa sauti yake. 15 Aliwapiga waadui mishale yake, akawatawanya; alirusha umeme mukali, akawakimbiza. 16 Ee Yawe, ulipovikaripia, pumzi ya pua yako ilifunua vilindi vya bahari na misingi ya dunia ikaonekana. 17 Mungu alinyoosha mukono wake kutoka juu, akanitwaa, alininyanyua kutoka ndani ya maji mengi. 18 Aliniokoa kutoka adui yangu mwenye nguvu, kutoka hao walionichukia na kuwa na nguvu kunishinda. 19 Walinishambulia nilipokuwa katika taabu, lakini Yawe alinikinga. 20 Alinileta, akaniweka kwenye nafasi ya usalama; aliniponyesha kwa sababu alipendezwa nami. 21 Yawe alinitendea kwa kadiri ya haki yangu; alinilipa kwa vile mikono yangu haina kosa. 22 Maana nimefuata njia za Yawe, wala sikujitenga na Mungu wangu kwa ajili ya uovu. 23 Nimeshika maagizo yake yote, sikuacha kufuata masharti yake. 24 Mbele yake nilikuwa mukamilifu; nimejikinga nisikuwe na kosa. 25 Yawe amenilipa kwa kadiri ya haki yangu; kwa kadiri ya usafi wa mikono yangu mbele yake. 26 Wewe ni mwema kwa wema, mukamilifu kwa wakamilifu, 27 bila kosa kwa wale ambao hawafanyi makosa, lakini mukali kwa waovu. 28 Wewe unawaokoa wanyenyekevu, lakini unawashusha wenye macho ya kujivuna. 29 Wewe, ee Yawe, unawakisha taa yangu. Mungu wangu anafanya giza langu likuwe mwangaza. 30 Kwa musaada wako, ninashinda kundi la waaskari; kwa musaada wa Mungu wangu, ninaruka kuta. 31 Njia ya Mungu ni kamilifu. Ahadi ya Yawe ni ya kuaminika. Yeye ni ngao kwa wote wanaomukimbilia. 32 Nani anayekuwa Mungu isipokuwa Yawe? Nani anayekuwa kikingio isipokuwa Mungu wetu? 33 Ni Mungu ambaye ananipatia nguvu, na kuifanya salama njia yangu. 34 Ameiimarisha miguu yangu kama ya swala, na kunilinda salama juu ya milima. 35 Ananifundisha kupigana vita, mikono yangu iweze kuvuta upinde wa chuma. 36 Umenipa ngao yako ya wokovu na kuniimarisha kwa mukono wako wa kuume. Nimefanikiwa kwa sababu ulikubali kunisaidia. 37 Umepanua njia yangu wala miguu yangu haikuteleza. 38 Niliwafuata waadui zangu na kuwakamata; sikurudi nyuma mpaka wamemalizika. 39 Niliwaangamiza, wasiweze kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. 40 Wewe ulinijalia nguvu ya kupigana vita; uliwaporomosha waadui chini yangu. 41 Uliwakimbiza waadui zangu, na wale walionichukia niliwaangamiza. 42 Walitafuta musaada, lakini hakukukuwa wa kuwasaidia; walimulilia Yawe, lakini hakuwajibu. 43 Niliwatwanga, wakakuwa kama vumbi inayopeperushwa na upepo; niliwakanyaga kama matope katika barabara. 44 Wewe uliniokoa kutoka mashambulizi ya watu, ukanifanya kuwa mutawala wa mataifa. Watu nisiowajua walinitumikia. 45 Waliposikia tu habari zangu, walinitii; wageni walinijia wakinyenyekea. 46 Wageni walivunjika moyo; wakakuja kutoka makimbilio yao wakitetemeka. 47 Yawe anaishi! Yeye ni kikingio changu – asifiwe! Mungu ni mwokozi wangu – atukuzwe! 48 Yeye ameniwezesha kulipiza kisasi; na kuwaweka mataifa chini ya mamlaka yangu. 49 Ameniokoa kutoka waadui zangu, Ee Yawe, ulinitukuza juu ya wapinzani wangu na kuniponyesha kutoka watesaji wakali. 50 Kwa hiyo, nitakutukuza kati ya mataifa, nitaliimbia sifa jina lako. 51 Mungu anamujalia mufalme wake ushindi mukubwa; anamutendea mema muchaguliwa wake, ndiye Daudi na wazao wake milele. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo