Zaburi 148 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ulimwengu wote umusifu Mungu 1 Haleluia! Mumusifu Yawe kutoka mbinguni, mumusifu kutoka huko juu mbinguni. 2 Mumusifu enyi wamalaika wake wote, mumusifu enyi jeshi lake lote. 3 Mumusifu enyi jua na mwezi, mumusifu enyi nyota zote zinazoangaza. 4 Mumusifu enyi mbingu za juu, na maji yanayokuwa juu ya mbingu. 5 Vyote visifu jina la Yawe, maana yeye aliamuru, na vyote vikakuwa. 6 Yeye aliviweka nafasi yao kwa milele, kwa amri ambayo haiwezi kuvunjika. 7 Mumusifu Yawe tokea katika dunia; enyi nyoka wakubwa wa bahari na mashimo ya bahari, mumusifu. 8 Mumusifu, enyi moto, mvua ya mawe na teluji, upepo wenye zoruba unaotimiza amri yake! 9 Mumusifu, enyi milima na vilima, miti ya matunda na ya mierezi! 10 Mumusifu, enyi nyama wa pori na wa kufugwa, viumbe vinavyotambaa na ndege wote! 11 Mumusifu, enyi wafalme na mataifa yote; waongozi na watawala wote katika dunia! 12 Mumusifu, enyi vijana wanaume na wabinti; wazee wote na watoto! 13 Wote musifu jina la Yawe, maana jina lake peke yake linatukuzwa; utukufu wake unapita dunia na mbingu. 14 Amewapa watu wake nguvu; nayo heshima kwa watu wote waaminifu, ndio watu wa Israeli wapendwa wake. Haleluia! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo