Zaburi 114 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu na watu wake 1 Watu wa Israeli walipotoka Misri, wazao wa Yakobo walipotoka katika inchi ya kigeni, 2 Yuda ikakuwa makao ya Mungu, Israeli ikakuwa urizi wake. 3 Bahari iliona hayo ikakimbia; muto Yordani ukaacha kutiririka! 4 Milima ilirukaruka kama kondoo dume; vilima vikaruka kama wana-kondoo! 5 Ee bahari, nini iliyokufikia hata ukakimbia? Nawe Yordani, kwa nini uliacha kutiririka? 6 Enyi milima, mbona muliruka kama kondoo dume? Nanyi vilima, namna gani mumeruka kama mwana-kondoo? 7 Utetemeke, ee dunia, mbele ya Yawe; utetemeke mbele ya Mungu wa Yakobo, 8 anayegeuza jiwe kubwa kuwa ziwa, nalo jiwe gumu kuwa chemichemi za maji! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo