Zaburi 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kumutumainia Mungu 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi. Yawe ni kimbilio langu; namna gani basi munaweza kuniambia: “Ruka kama ndege, mpaka kwenye milima, 2 maana waovu wanavuta pinde; wameweka mishale tayari juu ya kamba, kusudi wawapige mishale watu wenye moyo wa usawa katika giza! 3 Kama misingi ikiharibiwa, mutu wa haki atafanya nini?” 4 Yawe yuko katika hekalu lake takatifu; kiti cha kifalme cha Yawe kiko mbinguni. Kwa macho yake anawachungulia wanadamu, na kujua kila kitu wanachofanya. 5 Yawe anawapima watu wa haki na waovu; anawachukia wanaopenda kutesa kwa ukali. 6 Atawanyeshea waovu makaa ya moto na kiberiti; upepo mukali utakuwa ndio azabu yao. 7 Yawe ni wa haki na anapenda watu watende kwa haki. Watu wa usawa wataona uso wake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo