Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Zaburi 107 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


SEHEMU YA TANO (Zaburi 107–150 ) Sifa kwa Mungu mwema

1 Mumushukuru Yawe kwa sababu ni muzuri! Wema wake unadumu milele!

2 Museme hivyo, enyi muliokombolewa na Yawe, watu ambao aliwaokoa katika taabu,

3 akawakusanya kutoka inchi za kigeni: kutoka mashariki na magaribi, kutoka kaskazini na kusini.

4 Wamoja walitangatanga katika jangwa tupu, hawakuweza kufikia katika muji wa kukaa.

5 Walisikia njaa na kiu; wakavunjika moyo kabisa.

6 Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao.

7 Aliwaongoza katika njia iliyonyooka, mpaka wakafika katika muji wa kukaa.

8 Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu.

9 Yeye anakunywesha wenye kiu; na anashibisha wenye njaa mazuri.

10 Wengine waliishi katika giza na ukiwa, wafungwa katika mateso na minyororo,

11 kwa sababu waliasi maagizo ya Mungu, na kuzarau mashauri ya Mungu Mukubwa.

12 Walikuwa tabani kwa kazi ngumu, wakaanguka chini, wala hawakuwa na wa kuwasaidia.

13 Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao.

14 Aliwatoa katika giza na ukiwa, na minyororo yao akaivunjavunja.

15 Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu.

16 Yeye anavunja na kufungua milango ya shaba, na kukatakata vifungio vya chuma.

17 Wengine walipumbazika kwa sababu ya zambi zao, waliteseka kwa sababu ya uovu wao;

18 walichukizwa na chakula, walikuwa karibu kufa.

19 Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao.

20 Kwa neno lake aliwaponyesha, akawaokoa wasiangamie.

21 Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu.

22 Wamutolee sadaka za shukrani; waeleze matendo yake kwa nyimbo za shangwe.

23 Wengine walisafiri katika bahari ndani ya mashua, na kufanya shuguli zao humo juu ya bahari.

24 Waliona matendo ya Yawe, mambo ya ajabu aliyotenda huko.

25 Aliamuru, akavumisha zoruba kali, ikarusha juu mawimbi ya bahari.

26 Walitupwa juu angani, kisha chini ndani ya shimo; uhodari wao ukawaishia katika tukio lile.

27 Waliyumbayumba na kuwayawaya kama walevi; ufundi wao ukawaishia.

28 Halafu katika taabu yao wakamulilia Yawe, naye akawaokoa katika mateso yao.

29 Alituliza ile zoruba kali, nayo mawimbi yakanyamaza.

30 Hapo wakafurahi kwa kupata utulivu; akawafikisha kwenye kivuko walichokiendea.

31 Mumushukuru Yawe kwa wema wake na maajabu yake kwa wanadamu.

32 Mumutukuze katika mukutano wa watu, na kumusifu katika baraza la wazee.

33 Mungu aligeuza mito kuwa jangwa, chemichemi akazikausha kabisa.

34 Udongo wenye mboleo akaugeuza kuwa udongo usioweza kutoa, kwa sababu ya uovu wa wakaaji wake.

35 Aligeuza jangwa kuwa ziwa, na inchi ya kukauka kuwa chemichemi za maji.

36 Akawahamishia wenye njaa kule, nao wakajenga muji wa kukaa humo.

37 Walilima mashamba na kupanda mizabibu, wakavuna mazao kwa wingi.

38 Aliwabariki watu wake, wakaongezeka; na hesabu ya wanyama wao akaizidisha.

39 Kisha walipopunguka na kuwa wazaifu, kwa kugandamizwa, kuteswa na huzuni,

40 aliwazarau wakubwa waliowatesa, akawazungusha katika jangwa lisilokuwa na njia.

41 Lakini aliwaokoa wakosefu katika taabu zao, akaongeza jamaa zao kama kundi la kondoo.

42 Watu wa usawa wanapoona jambo hilo wanafurahi, lakini waovu wote wananyamazishwa.

43 Wenye hekima wafikiri juu ya mambo haya, watambue wema wa Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan