Zaburi 104 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kumusifu Muumba 1 Umusifu Yawe, ee nafsi yangu! Ee Yawe, Mungu wangu, wewe ni mukubwa kabisa! Umevaa utukufu na mamlaka. 2 Umejifunika mwangaza kama kanzu, umekunjua mbingu kama hema; 3 umejenga makao yako katika mbingu juu ya maji. Umeyafanya mawingu kuwa gari lako nawe unatembea katika anga. 4 Unaufanya upepo kuwa mujumbe wako, moto na ndimi zake kuwa watumishi wako. 5 Umeiweka dunia imara juu ya misingi yake, isitikisike hata milele. 6 Uliifunika dunia kwa bahari kama nguo, na maji yakaimeza milima mirefu. 7 Ulipoyakaripia, yalikimbia; yaliposikia ngurumo yako, yalitelemuka mbio. 8 Yaliporomoka toka milima mpaka katika mabonde, mpaka pahali ulipoyatengenezea. 9 Uliyawekea hayo maji mipaka yasiyoweza kutambuka, kusudi yasifunike tena dunia. 10 Umetokeza chemichemi katika mabonde, na vijito vyao vinapita kati ya vilima. 11 Hivyo vinakunywesha wanyama wote wa pori, na humo punda wa pori wanatulizia kiu chao. 12 Ndege wanajenga chicha zao katika miti ya hapo, wanatua katika matawi yake na kuimba. 13 Toka juu angani, unainyeshea milima mvua, nayo dunia unaishibisha kwa baraka yako. 14 Unaotesha majani kwa ajili ya mifugo, na mimea kwa matumizi ya mwanadamu kusudi naye apate chakula chake toka udongo: 15 apate divai ya kumuchangamusha, mafuta ya muzeituni ya kumwangarisha, na mukate wa kumupa nguvu. 16 Miti mikubwa ya Yawe inapata maji ya kutosha; ndiyo mierezi ya Lebanoni aliyoipanda. 17 Humo, ndege wanajenga chicha zao, korongo wanafanya makao yao katika misunobari. 18 Milima mirefu ni makao ya mbuzi wa pori; makimbilio ya sungura wa pori ni chini ya mawe. 19 Umeumba mwezi kwa kutupimia nyakati, nalo jua linalojua wakati wa kutua. 20 Unaleta giza, nao usiku unaingia; nao wanyama wote wa pori wanatoka: 21 simba wakali wananguruma wanapokosa mawindo yao, wanakungojea wewe Mungu uwape chakula chao. 22 Jua linapopanda, wanarudi kwao, na kujipumzisha ndani ya mapango yao. 23 Hapo mwanadamu naye anaenda kwenye kazi zake; naye anatumika mpaka magaribi. 24 Ee Yawe, matendo yako ni mengi sana! Umeyafanya kwa hekima yote! Dunia imejaa viumbe vyako! 25 Mbali kule kuna bahari kubwa na pana, ambamo kumejaa viumbe visivyokuwa na hesabu, viumbe vizima, vikubwa na vidogo. 26 Mashua zinasafiri humo, na yule nyama mukubwa Leviatani uliyemwumba achezee humo. 27 Hao wote wanakungojea wewe, uwapatie chakula chao kwa wakati wake. 28 Wanaokota kitu chochote unachowapa; ukiwafungulia mukono, wanashiba vyakula vizuri. 29 Ukiwageuzia mugongo, wanaogopa; ukiondoa pumzi yao, wanakufa na kurudi ndani ya mavumbi walimotoka. 30 Ukiwapulizia pumzi yako, wanaumbwa; wewe unafanya vitu vipya katika dunia. 31 Utukufu wa Yawe unadumu hata milele; Yawe anapendezwa na matendo yake mwenyewe. 32 Anaiangalia dunia, nayo inatetemeka; anagusa milima, nayo inatoa moshi! 33 Nitamwimbia Yawe maisha yangu yote; nitamusifu Mungu wangu muda wote nitakaoishi. 34 Upendezwe na hayo mashairi yangu, ee Yawe, maana wewe ndiye furaha yangu. 35 Wenye zambi wote waondolewe katika dunia, waovu wote wasikuwe tena! Umusifu Yawe, ee nafsi yangu! Haleluia! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo