Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoshua 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Wafalme wote wa Waamori walioishi ngambo ya magaribi ya Yordani, na wafalme wote wa Wakanana waliokuwa kandokando ya bahari ya Mediteranea, waliposikia kwamba Yawe aliyakausha maji ya muto Yordani kwa ajili ya Waisraeli mpaka walipokwisha kuvuka, wakavunjika moyo; wakaishiwa nguvu kabisa kwa kuwaogopa Waisraeli.


Kutahiriwa kwa Waisraeli kule Gilgali

2 Wakati ule, Yawe akamwambia Yoshua: “Tengeneza visu vya jiwe gumu kusudi uwatahiri Waisraeli.”

3 Basi, Yoshua akatengeneza visu hivyo vya jiwe gumu na kuwatahiri Waisraeli kule Gibea-Haraloti.

4 Sababu ya kuwatahiri Waisraeli ni hii: Waisraeli wote, wanaume, waliotoka Misri ambao walikuwa na umri wa kwenda kwa vita, wote walikufa katika safari ndani ya jangwa nyuma ya kutoka katika inchi ya Misri.

5 Hao wote waliotoka Misri walikuwa wametahiriwa, lakini wale wote waliozaliwa katika safari kule katika jangwa kisha kutoka Misri, walikuwa bado hawajatahiriwa.

6 Waisraeli walisafiri kwa muda wa miaka makumi ine katika jangwa hata wanaume wote waliokuwa na umri wa kwenda kwa vita wakaangamia kwa kuwa hawakusikiliza mambo Yawe aliyosema. Yawe alikuwa amewaapia watu hao kwamba hawataiona inchi ile inayotiririka maziwa na asali ambayo yeye aliwaapia baba zao kwamba atawapa.

7 Kwa hiyo ilikuwa watoto wa watu hao ambao Yawe aliowakomalisha kwa pahali pao. Na ni hao ndio Yoshua aliowatahiri, maana hawakukuwa wanatahiriwa wakati ule walipokuwa katika safari ndani ya jangwa.

8 Wanaume wote walipokwisha kutahiriwa walikaa katika kambi mpaka walipopona.

9 Kisha Yawe akamwambia Yoshua: “Leo hii nimewaondolea ile haya ya Misri.” Hivyo pahali pale pakaitwa Gilgali mpaka hivi leo.

10 Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi kule Gilgali wakafanya sikukuu ya Pasaka magaribi ya siku ya kumi na ine ya mwezi katika mabonde ya Yeriko.

11 Kesho yake, ni kusema nyuma ya Pasaka, walikula mikate isiyotiwa chachu na mbegu zenye kukaangwa kutokana na mazao ya inchi ile.

12 Basi, tangu siku hiyo walipokula mazao ya inchi hiyo, Waisraeli hawakupata mana tena. Tangu mwaka ule Waisraeli walikula mazao ya inchi ya Kanana.


Yoshua na jemadari wa jeshi la Yawe

13 Siku moja Yoshua alipokuwa karibu na muji wa Yeriko, aliona kwa rafla mutu mumoja akisimama mbele yake na upanga uliochomolewa katika mukono wake. Yoshua akamwendea, akamwuliza: “Wewe ni wetu au ni wa waadui zetu?”

14 Naye akamujibu: “Wala wenu wala wa waadui zenu! Lakini mimi ni jemadari wa jeshi la Yawe, na sasa nimefika.” Yoshua akainama chini kwa heshima, kisha akamwuliza: “Bwana wangu, unataka mimi mutumishi wako nifanye nini?”

15 Huyo jemadari wa jeshi la Yawe akamwambia: “Vua viatu vyako kwa maana pahali unaposimama ni patakatifu.” Yoshua akafanya hivyo.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan