Yoshua 24 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Waisraeli wanaamua kumutumikia Yawe 1 Kisha Yoshua akayakusanya makabila yote ya Waisraeli kule Sekemu. Akawaita wazee, viongozi, waamuzi na wakubwa wa Waisraeli, nao wakakuja mbele ya Mungu. 2 Yoshua akawaambia watu wote: “Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Hapo zamani, wazee wenu waliishi ngambo ya muto Furati, wakaitumikia miungu mingine. Muzee mumoja aliitwa Tera, baba ya Abrahamu na Nahori. 3 Mimi Mungu nilimwondoa babu yenu Abrahamu kutoka kule ngambo ya muto Furati na kumuleta hapa Kanana, ambako nilimupatia wazao wengi. Nilimupa Isaka, 4 naye Isaka nikamupa Yakobo na Esau. Nilimupa Esau milima ya Seiri airizi. Lakini Yakobo na watoto wake walikwenda Misri. 5 Nyuma nikawatuma Musa na Haruni, nikailetea inchi ya Misri mapigo, na kisha nikawatoa ninyi katika inchi ile. 6 Niliwatoa wazee wenu kutoka Misri na kuwaleta mpaka kwenye bahari Nyekundu. Wamisri waliwafuatilia wakiwa na magari na waaskari wapanda-farasi. 7 Waisraeli waliponililia mimi Yawe, niliweka giza kati yao na Wamisri na kuifanya bahari iwafunike Wamisri. Ninyi wenyewe mulijionea yale niliyowatendea Wamisri. Muliishi katika jangwa muda murefu. 8 Kisha niliwaongoza mpaka katika inchi ya Waamori ambao waliishi upande mwingine wa muto Yordani. Walipigana nanyi, lakini mimi niliwapa ushindi juu yao mukawaangamiza na kuiteka inchi yao. 9 Naye Balaka mwana wa Sipori, mufalme wa Moabu, akakuja na kuwashambulia Waisraeli. Akamwalika Balama mwana wa Beori akuje kuwalaani ninyi. 10 Lakini mimi sikumusikiliza Balama, naye akawabariki, nami nikawaokoa ninyi toka mikono ya Balaka. 11 Halafu mukavuka muto Yordani, mukafika Yeriko. Wakaaji wa Yeriko walipigana nanyi, vilevile na Waamori, Waperizi, Wakanana, Wahiti, Wagirgasi, Wahivi na Wayebusi. Hao mimi nikawatia katika mikono yenu. 12 Nilituma nyuki mbele yenu ambazo ziliwafukuza wafalme wawili wa Waamori. Hamukufanya yale kwa kukamata mapanga wala mishale yenu. 13 “Niliwapa mashamba ambayo hamukukuwa mumeyalima, na miji ambayo hamukuijenga ambamo sasa munaishi, na kula matunda ya mizabibu na mizeituni ambayo hamukuipanda. 14 “Sasa, basi, mumutii Yawe na kumutumikia kwa moyo wa haki na uaminifu. Muache kabisa miungu ile ambayo wazee wenu waliiabudu ngambo ya muto Furati na katika inchi ya Misri. Mumutumikie Yawe. 15 Kama hamutaki kumutumikia Yawe, basi muchague leo hii ni nani mutakayemutumikia: kama ni miungu ile ambayo wazee wenu waliitumikia ngambo ya muto Furati, au miungu ya Waamori ambao sasa munaishi katika inchi yao. Lakini mimi na jamaa yangu, tutamutumikia Yawe.” 16 Halafu watu wakamujibu: “Hatutaweza hata kidogo kumwacha Yawe na kuitumikia miungu mingine. 17 Maana, Yawe, Mungu wetu, ndiye aliyetutoa sisi pamoja na wazee wetu katika inchi ya Misri tulikokuwa watumwa, tukayaona kwa macho yetu wenyewe matendo ya ajabu aliyotenda. Akatulinda katika safari zetu zote na kati ya watu wote ambao tulipita kati yao. 18 “Yawe alituondolea watu wote, ni kusema Waamori wote waliokaa katika inchi. Kwa hiyo, nasi tutamutumikia Yawe, maana ndiye Mungu wetu.” 19 Lakini Yoshua akawaambia: “Ninyi hamuwezi kumutumikia Yawe, maana yeye ni Mungu Mutakatifu. Yeye ni Mungu mwenye wivu, naye hatawasamehe makosa na zambi zenu. 20 Mukimwacha Yawe na kuitumikia miungu ya kigeni, atawaazibu na kuwaangamiza ninyi, hata ingawa amewatendea mema haya yote.” 21 Nao watu wakamwambia Yoshua: “Hapana! Sisi tutamutumikia Yawe tu.” 22 Halafu Yoshua akawaambia: “Ninyi ni washuhuda wenu wenyewe kwamba mumechagua kumutumikia Yawe.” Nao wakamujibu: “Sisi ni washuhuda.” 23 Naye akawaambia: “Basi, muondoe miungu ya kigeni munayokuwa nayo, mumufuate Yawe, Mungu wa Israeli, kwa moyo wenu wote.” 24 Nao, wakasema: “Tutamutumikia na kumutii Yawe, Mungu wetu.” 25 Hivyo, Yoshua akafanya agano na Waisraeli kule Sekemu, akawapa masharti na maagizo ya kufuata. 26 Yoshua akayaandika haya yote katika kitabu cha sheria ya Mungu; kisha, akatwaa jiwe kubwa na kulisimika chini ya muti wa mwalo katika hema ya Yawe. 27 Halafu akawaambia watu wote: “Jiwe hili ndilo litakalokuwa ushuhuda kwetu, maana limesikia maneno yote ambayo Yawe ametuambia. Kwa hiyo, litashuhudia juu yenu, kusudi musipate kumwasi Mungu wenu.” 28 Halafu Yoshua akawaruhusu watu waondoke; nao wakaenda kila mumoja kwake. Kifo cha Yoshua 29 Nyuma ya mambo hayo, Yoshua mwana wa Nuni na mutumishi wa Yawe, akakufa akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi. 30 Nao wakamuzika kwenye eneo ambalo alikuwa amegawanyiwa kuwa sehemu yake, kule Timunati-Sera, katika milima ya Efuraimu, upande wa kaskazini wa mulima wa Gasi. 31 Waisraeli walimutumikia Yawe muda wote wa maisha ya Yoshua, na nyuma ya kifo chake, waliendelea kumutumikia kwa muda wa maisha ya wale wazee waliokuwa wameona kwa macho yao mambo yale Yawe aliyowatendea Waisraeli. 32 Mifupa ya Yosefu ambayo Waisraeli walikuwa wameileta kutoka Misri waliizika kule Sekemu katika eneo ambalo Yakobo alikuwa amelinunua kutoka kwa wana wa Hamori, baba ya Sekemu, kwa bei ya vikoroti mia moja vya feza. Eneo lile nalo likakuwa mali yao wazao wa Yosefu. 33 Naye Eleazari mwana wa Haruni, akakufa na kuzikwa Gibea, muji ambao mwana wake Finehasi alikuwa amepewa katika inchi ya milima ya Efuraimu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo