Yoshua 22 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Makabila ya upande wa mashariki yanarudi kwao 1 Basi, Yoshua akawaita watu wa kabila la Rubeni, la Gadi na watu wa nusu ya kabila la Manase 2 akawaambia: “Ninyi mumefuata yale yote Musa, mutumishi wa Yawe, aliyowaamuru na mumetii maagizo niliyowaamuru. 3 Wala hamukuwaacha wandugu zenu kwa muda ule wote murefu mpaka leo, lakini mumefuata kwa uangalifu amri ya Yawe, Mungu wenu. 4 Sasa Yawe, Mungu wenu, amewapa wandugu zenu amani, kama vile alivyoahidi, basi, murudie kwenu katika inchi ambayo mulipewa na Musa mutumishi wa Yawe, ikuwe mali yenu, ni kusema ngambo ya muto Yordani. 5 Mukuwe waangalifu kutii amri na sheria ambazo Musa, mutumishi wa Yawe, aliwaamuru: mumupende Yawe, Mungu wenu, mufuate anachotaka na kushika amri zake, mukae pamoja naye na kumutumikia kwa moyo wote na roho yote.” 6 Basi, Yoshua akawabariki na kuwaruhusu waende zao akawaambia: 7-8 “Murudie kwenu na utajiri mwingi; ngombe wenu wote, feza, zahabu, shaba, chuma na nguo nyingi. Mugawanyane na wandugu zenu vitu vyote mulivyonyanganya kutoka kwa waadui zenu.” Musa alikuwa amepatia nusu ya kabila la Manase sehemu yao kule Basani. Naye Yoshua akaipatia nusu ya pili ya kabila lile sehemu yao kule upande wa magaribi wa muto Yordani kama vile alivyoyapatia makabila yale mengine. Mazabahu karibu na Yordani 9 Basi, watu wa Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase wakaachana na watu wa makabila mengine ya Israeli kule Shilo katika inchi ya Kanana, wakarudi kwao katika inchi ya Gileadi, inchi yao wenyewe walioirizi kwa amri ya Yawe kama vile alivyomwagiza Musa. 10 Walipofika kwenye muto Yordani wakiwa bado katika inchi ya Kanana, wakajenga mazabahu kubwa sana karibu na muto huo. 11 Basi, habari zikawafikia watu wa makabila mengine ya Israeli kwamba makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase yalikuwa yamejenga mazabahu kubwa karibu na muto Yordani katika inchi ya Kanana, ni kusema ndani ya eneo lao. 12 Waliposikia hivyo, Waisraeli walikusanyika wote kule Shilo kwenda kupigana vita na hayo makabila ya upande wa mashariki. 13 Basi, watu wa Israeli wakamutuma Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, kule Gileadi kwa makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase. 14 Finehasi akaondoka pamoja na wakubwa kumi, kila mumoja akiwa mukubwa wa jamaa katika kabila lake. 15 Nao wakawaendea watu wa makabila ya Rubeni, Gadi na nusu ya kabila la Manase kule Gileadi wakawaambia: 16 “Watu wote wa Yawe wanauliza hivi: ‘Ni udanganyifu gani huu mumemufanyia Mungu wa Israeli? Mbona mumemwasi Yawe kwa kujenga mazabahu hii? 17 Zambi tulizotenda kule Peori hazitoshi? Hamwoni kwamba bado hatujajitakasa na kwamba mateso yake bado yanaisumbua watu wa Yawe? 18 Kwa nini, basi, mumeacha kumufuata Yawe? Mukimwasi Yawe leo, kesho atakasirikia sana Waisraeli wote pamoja. 19 Basi, ikiwa inchi yenu muliorizi ni chafu, mukuje katika inchi ya Yawe ambako hema yake iko na kujitwalia sehemu kule pamoja nasi; lakini tu musimwasi Yawe na kutufanya sisi wote waasi kwa kujijengea ninyi wenyewe mazabahu isiyokuwa ya Yawe, Mungu wetu. 20 Akana mwana wa Zera alipokosa uaminifu katika vitu vitakatifu, kasirani haikuangukia Waisraeli wote pamoja? Tena Akana hakukufa tu yeye peke yake kwa sababu ya uovu wake.’ ” 21 Hapo watu wa makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase wakawajibu viongozi wa jamaa za Waisraeli: 22 “Mungu wa miungu ndiye Yawe! Mungu wa miungu ndiye Yawe! Yeye anajua kwa nini tumefanya hivyo. Na Waisraeli wote watajua vilevile! Kama huu ni uasi au ni ukosefu wa imani kwa Yawe basi, yeye aache kutuokoa leo. 23 Kama tumemwacha Yawe tukajenga mazabahu yetu wenyewe kusudi tutoe sadaka za kuteketezwa kwa moto, za unga au za amani, basi Yawe atulipize kisasi. 24 Lakini sivyo inavyokuwa. Tuliijenga kwa kuogopa kwamba labda katika siku zinazokuja watoto wenu watawaambia watoto wetu: ‘Ninyi muko na uhusiano gani na Yawe, Mungu wa Israeli? 25 Hamwoni kwamba Yawe ameweka muto wa Yordani kuwa mupaka kati yenu na sisi? Ninyi makabila ya Rubeni na kabila la Gadi hamuna fungu lolote lenu kwa Yawe.’ Hivyo watoto wenu wangeweza kisha kusababisha watoto wetu waache kumwabudu Yawe. 26 Ndiyo maana tuliamua kujenga mazabahu hii, lakini si kwa ajili ya kutolea juu yake sadaka za kuteketezwa kwa moto wala sadaka zingine, 27 lakini tulitaka mazabahu hii ikuwe ushuhuda kati yetu na ninyi na vizazi vyetu vinavyokuja kwamba sisi tuna haki ya kumutumikia Yawe kwa sadaka zetu za kuteketezwa kwa moto na sadaka zetu zingine, na kwa sadaka zetu za amani, kusudi watoto wenu wasipate kuwaambia watoto wetu kwamba hawana fungu lolote lao kwa Yawe. 28 Tena tulifikiri kwamba ikiwa jambo kama hilo litasemwa juu yetu au juu ya wazao wetu katika siku zinazokuja, tutasema: ‘Muangalie mufano wa mazabahu ya Yawe ambayo wazee wetu waliijenga; sio kwa ajili ya kutolea juu yake sadaka za kuteketezwa kwa moto au sadaka zingine lakini kama ushuhuda kati yetu na ninyi’. 29 Sisi hatukuwa na nia ya kumwasi sasa Yawe hata kidogo na kumwacha kwa kujenga mazabahu ya kutolea sadaka za kuteketezwa kwa moto au sadaka za unga au sadaka zingine. Hatupendi kutolea sadaka pahali pengine isipokuwa juu ya mazabahu ya Yawe, Mungu wetu, inayokuwa katika makao yake.” 30 Kuhani Finehasi na wakubwa wa jamaa za Waisraeli waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno hayo ya watu wa makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase, wakafurahi. 31 Naye Finehasi mwana wa kuhani Eleazari, akayaambia makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase: “Leo tumejua kwamba Yawe yuko kati yenu maana hamukumufanyia Mungu uasi. Sasa mumewaokoa Waisraeli wasiazibiwe na Yawe.” 32 Basi, Finehasi mwana wa kuhani Eleazari pamoja na viongozi wenzake wakawaaga watu wa makabila ya Rubeni na Gadi wakaondoka katika inchi ya Gileadi, wakarudi Kanana kwa Waisraeli na kuwapa habari hizo. 33 Habari hiyo ikawafurahisha Waisraeli, wakamushukuru Yawe na kuacha mipango yao ya vita na kusudi lao la kuharibu kabisa inchi iliyokuwa ya makabila ya Rubeni na Gadi. 34 Watu wa makabila ya Rubeni na Gadi wakaiita ile mazabahu “Ushuhuda”, maana walisema: “Mazabahu hii ni ushuhuda wetu kwamba Yawe ndiye Mungu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo