Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoshua 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mungu anamwamuru Yoshua kuiteka inchi ya Kanana

1 Nyuma ya kifo cha Musa mutumishi wa Yawe, Yawe alimwambia Yoshua mwana wa Nuni, musaidizi wa Musa:

2 “Mutumishi wangu Musa amekufa, sasa muvuke muto Yordani, wewe pamoja na Waisraeli wote mpaka kwenye inchi ile ambayo ninawapa.

3 Kila pahali mutakapokanyaga nimewapa ninyi nafasi ile kama nilivyomwahidi Musa.

4 Mipaka ya inchi yenu itakuwa hivi: upande wa kusini ni jangwa, kaskazini ni milima ya Lebanoni, mashariki ni muto ule mukubwa Furati, kupitia inchi yote ya Wahiti mpaka bahari ya Mediteranea upande wa magaribi.

5 Hakuna mutu atakayekushinda siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe kama nilivyokuwa pamoja na Musa. Siku zote nitakuwa nawe wala sitakuacha hata kidogo.

6 Ukuwe imara na hodari kwa sababu wewe utawaongoza watu hawa kuirizi inchi ambayo niliwaahidi kwamba nitawapa wazee wao.

7 Ukuwe tu imara na hodari. Ukuwe mwangalifu na kushika sheria yote mutumishi wangu Musa aliyokuamuru. Fuata kila sehemu ya sheria hiyo nawe utafanikiwa popote utakapoenda.

8 Hakikisha kwamba hautakisahau hata kidogo kitabu hiki cha sheria; lakini kila siku utajifunza kitabu hiki, muchana na usiku, kusudi upate kutimiza yote yaliyoandikwa humu, nawe utastawi na kufanikiwa.

9 Kumbuka kwamba mimi nimekuamuru ukuwe imara na hodari. Usiogope wala usifazaike kwa sababu mimi Yawe, Mungu wako, niko pamoja nawe popote utakapoenda.”


Yoshua anawatayarisha watu kuvuka muto Yordani

10 Kisha Yoshua akawaamuru viongozi wa watu:

11 “Mupite katika kambi na kuwaamuru watu watayarishe chakula, kwa sababu kisha siku tatu mutavuka muto Yordani, kwenda kuirizi inchi ambayo Yawe, Mungu wenu, anawapa ikuwe mali yenu.”

12 Yoshua akawaambia watu wa kabila la Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase:

13 “Mukumbuke lile jambo ambalo Musa, mutumishi wa Yawe, aliwaamuru akisema: ‘Yawe, Mungu wenu, atawapa pahali pa kupumzika, na atawapa inchi hii’.

14 Wake zenu, watoto wenu na nyama wenu wa kufugwa watabaki katika inchi hiyo ambayo Musa aliwapa, ngambo ya muto Yordani. Lakini wanaume wote hodari wakiwa na silaha watavuka muto na kuwatangulia wandugu zenu.

15 Mutawasaidia mpaka Yawe atakapowapa wandugu zenu vilevile pahali pa kupumzika, kama vile alivyowapa ninyi, nao vilevile warizi inchi ambayo wanapewa na Yawe, Mungu wenu. Kisha mutarudi katika inchi ambayo ni mali yenu na kuirizi, inchi ambayo mulipewa na Musa, mutumishi wa Yawe, ngambo ya muto Yordani.”

16 Wakamujibu Yoshua: “Mambo yote uliyotuamuru tutayafanya, na popote utakapotutuma tutakwenda.

17 Kama vile tulivyomutii Musa katika mambo yote, ndivyo tutakavyokutii wewe; Yawe, Mungu wako, akuwe pamoja nawe kama alivyokuwa pamoja na Musa.

18 Mutu yeyote atakayeasi amri yako au kukataa kutii maneno yako au jambo lolote unalomwamuru, atauawa. Lakini, wewe ukuwe na nguvu na kuwa hodari.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan