Yona 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yona anafuata agizo la Mungu 1 Neno la Yawe lilimufikia Yona mara ya pili kusema hivi: 2 Simama, uende Ninawe, ule muji mukubwa, uwatangazie watu ujumbe ninaokupa. 3 Basi, Yona akaondoka, akaenda Ninawe kama vile Yawe alivyomwagiza. Muji wa Ninawe ulikuwa mukubwa sana. Upana wake ulikuwa mwendo wa siku tatu. 4 Alipofika, Yona aliingia katika muji. Kisha kutembea mwendo wa siku nzima, akaanza kutangaza: Kunabaki siku makumi ine tu na muji huu wa Ninawe utaangamizwa! 5 Basi, watu wa Ninawe wakauamini ujumbe wa Mungu, wakatangaza kufunga kula chakula, na kwamba kila mumoja wao, mukubwa kama vile mudogo, avae gunia. 6 Habari hizi zikamufikia mufalme wa Ninawe, naye akaondoka juu ya kiti chake cha kifalme, akavua nguo yake ya kifalme, akavaa gunia na kuikaa katika majivu. 7 Kisha mufalme akawatangazia wakaaji wa Ninawe: Mimi mufalme, pamoja na wakubwa wangu, ninatoa amri hii: Kusikuwe mutu yeyote, ngombe au nyama yeyote wa kufugwa, atakayeonja kitu chochote. Hairuhusiwi kwa mutu yeyote au nyama kula au kunywa. 8 Watu wote na nyama wavae gunia. Kila mutu amwombe Mungu na kumusihi kwa moyo. Kila mumoja aache uovu wake, aache kutenda kwa ukali. 9 Labda Mungu atabadilisha nia yake, na kuacha kutukasirikia, nasi hatutaangamizwa! 10 Mungu alipoona walivyofanya, na jinsi walivyouacha uovu wao, akabadilisha nia yake, akaacha kuwatenda kama alivyokuwa amekusudia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo