Yoeli 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maonyo juu ya siku ya Yawe 1 Mupige baragumu kule Sayuni; mupige kelele la kujulisha hatari kule juu ya mulima mutakatifu! Mutetemeke enyi wakaaji wa Yuda, maana siku ya Yawe inakuja, siku hiyo iko karibu! 2 Hiyo ni siku ya giza na huzuni; siku ya mawingu na giza nene. Jeshi kubwa linakaribia kama giza linalofunikia milima. Namna hiyo haijapata kuwa hata kidogo wala haitaonekana tena katika vizazi vyote vinavyokuja. 3 Kama vile moto unavyoteketeza, Jeshi hilo linaharibu kila kitu mbele yake na kuacha nyuma kila kitu kinateketezwa; mbele ya kupita kwao, inchi ni kama bustani ya Edeni, lakini wakisha kupita, ni jangwa tupu. Hakuna kinachoweza kuponyoka! 4 Wanaonekana kama farasi, wanashambulia kama farasi wa vita. 5 Wanaporukaruka kwenye vilele vya milima, wananguruma kama magari yenye kukokotwa na farasi, wanavuma kama moto wa majani yenye kukauka. Wamejipanga kama kundi kubwa la waaskari tayari kabisa kufanya vita. 6 Wanapokaribia, watu wanajaa hofu, nyuso zao zinawaivya. 7 Wanashambulia kama mashujaa wa vita; wanapanda juu ya kuta kama waaskari. Wote wanakwenda mbele moja kwa moja, bila hata mumoja wao kubadilisha njia. 8 Hakuna anayemusukuma mwenzake; kila mumoja anafuata njia yake. Wanapita kati ya vizuizi vya silaha, wala hakuna kinachoweza kuwazuia. 9 Wanashambulia muji, wanakimbia juu ya ukuta; wanapanda juu ya nyumba na kuingia, wanapenya katika madirisha kama wezi. 10 Inchi inatetemeka mbele yao, mbingu zinatikisika. Jua na mwezi vinatiwa giza, nazo nyota zinaacha kuangaza. 11 Yawe anaamuru kundi lake kwa sauti; waaskari wake ni wengi sana, wanaomutii hawahesabiki. Siku ya Yawe kweli ni kubwa na ya kutisha sana! Nani atakayeweza kuivumilia? Mwito wa kumurudilia Yawe 12 Lakini hata sasa, munirudilie kwa moyo wote, kwa kufunga kula, kwa kulia na kuomboleza. –Ni ujumbe wa Yawe.– 13 Munapasua nguo zenu kwa kuonyesha huzuni, lakini inafaa mioyo yenu ipasuke vilevile. Murudilie Yawe, Mungu wenu. Yeye amejaa huruma na rehema, hakasiriki upesi, ni mwingi wa wema, na tayari kubadilisha nia zake kusudi asiazibu. 14 Labda Yawe, Mungu wenu, atabadilisha nia na kuwapa baraka ya mazao, mutaweza kumutolea sadaka za chakula na kinywaji. 15 Mupige baragumu kule Sayuni! Mutoe amri watu wafunge kula; muwaalike kuja kwa mukutano wa kidini. 16 Muwakusanye watu wote, muwatakase watu. Muwalete wazee, muwakusanye watoto, hata watoto wanaonyonya. Bwana-arusi na bibi-arusi watoke katika vyumba vyao. 17 Kati ya mazabahu na mulango wa hekalu, makuhani wanaomutumikia Yawe, walie na kuomba wakisema: Uwahurumie watu wako, ee Yawe. Usiyaache mataifa mengine yatuzarau na kutuchekelea yakisema: Yuko wapi basi Mungu wao? Mungu ataifanikisha inchi 18 Yawe anaipenda inchi yake anawahurumia watu wake. 19 Alisikiliza, akajibu maombi yao, akasema: Sasa nitawapa tena ngano, divai na mafuta, nanyi mutashiba navyo. Sitawafanya muzarauliwe tena na mataifa. 20 Nitawaondoa hao waadui wanaotoka kaskazini, nitawafukuza mpaka katika jangwa; waaskari wa mbele nitawatupa katika bahari ya Chumvi na wale wa nyuma katika bahari ya Mediteranea. Watatoa uvundo na harufu mbaya, hao ambao wamefanya maovu makubwa. 21 Usiogope, ewe inchi, lakini ufurahi na kushangilia, maana Yawe ametenda mambo makubwa. 22 Musiogope, enyi nyama, malisho katika mbuga yamekuwa mazuri, miti inazaa matunda yake, mizabibu na mitini zinazaa kwa wingi. 23 Mufurahi, enyi watu wa Sayuni, mushangilie kwa sababu ya Yawe, Mungu wenu, maana amewapa mvua zinazowafalia, amewapa mvua ya kutosha: mvua za kwanza na mvua za katikati kama pale mbele. 24 Nafasi ya kupepetea itajaa ngano, vikamulio vitafurika divai na mafuta. 25 Nitawarudishia miaka ile iliyokuliwa na nzige, kila kitu kilichokuliwa na tunutu, parare na panzi, hilo kundi kubwa nililowaletea! 26 Mutapata chakula kingi na kutosheka; mutalisifu jina la Yawe, Mungu wenu, aliyewatendea mambo ya ajabu. Watu wangu, hawatazarauliwa tena hata kidogo. 27 Mutatambua kwamba mimi niko kati yenu, enyi Waisraeli; na kwamba mimi Yawe, ndimi Mungu wenu wala hakuna mwingine. Watu wangu, hawatazarauliwa tena hata kidogo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo