Yoeli 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Vita kati ya inchi ya Yuda na ya Israeli 1 Hili ni neno la Yawe lililomufikia Yoeli mwana wa Petueli. Watu wanaomboleza juu ya mimea 2 Musikilize kitu hiki, enyi wazee; mutege sikio, ninyi wakaaji wote wa Yuda! Jambo kama hili limekwisha kutokea katika maisha yenu, au nyakati za babu zenu? 3 Muwaelezee watoto wenu jambo hili, nao wawaelezee watoto wao, na watoto wao wakielezee kizazi kinachofuata. 4 Nzige, makundi kwa makundi, wameishambulia mimea; kilichoachwa na nzige kimekuliwa na tunutu, kilichoachwa na tunutu kimekuliwa na parare, kilichoachwa na parare kimeliwa na panzi. 5 Enyi walevi, muamuke na kulia; enyi walevi wa divai, mulalamike; zabibu zote za kutengeneza divai mupya zimeharibiwa. 6 Jeshi la nzige limeishambulia inchi yetu; lina nguvu na ni kubwa ajabu; meno yake ni kama ya simba, na mataya yake ni kama ya simba dike. 7 Limeiharibu mizabibu yetu, na kuitafuna mitini yetu. Limeyabandua maganda yake na kuyatupa chini, na matawi yake yameachwa meupe. 8 Mulie kama vile binti aliyevaa gunia akiombolezea kifo cha muchumba wake. 9 Sadaka za vyakula na za kinywaji zimetoweka katika nyumba ya Yawe. Makuhani, watumishi wa Yawe, wanaomboleza. 10 Mashamba yamebaki matupu. Inchi inaomboleza, maana ngano imeharibiwa, divai imetoweka, mafuta yamekosekana. 11 Muomboleze, enyi walimaji; mulalamike, enyi watunza mizabibu. Ngano na shayiri zimeharibika, mavuno yote katika shamba yameangamia. 12 Mizabibu imenyauka, mitini imekauka, miti yote ya matunda imekauka. Furaha imetoweka kati ya watu. 13 Enyi makuhani, muvae magunia kwa kuomboleza, mulie, enyi munaotumika kwenye mazabahu. Muingie katika hekalu muomboleze usiku kucha! Sadaka za chakula na kinywaji zimetoweka katika nyumba ya Mungu. 14 Mutoe amri watu wafunge kula chakula; muwaalike watu kuja kwa mukutano wa kidini. Mukusanye wazee na wakaaji wote wa inchi, katika nyumba ya Yawe, Mungu wenu, na mule mumulilie Yawe. 15 Ole kwetu kwa ile siku ya Yawe, siku hiyo ya Yawe inakaribia; inakuja pamoja na maangamizi, kutoka kwa Mungu Mukubwa. 16 Mazao yetu yameharibiwa mbele ya macho yetu. Furaha na kicheko vimetoweka katika nyumba ya Mungu wetu. 17 Mbegu zinaoza ndani ya udongo; gala zimebaki bila kitu, vibanda vya kuwekea mavuno vimebomoka, kwa maana hakuna tena ngano. 18 Angalia jinsi nyama wanavyolia kwa huzuni! Makundi ya ngombe yanahangaika, kwa sababu yamekosa malisho; hata makundi ya kondoo yanateswa. 19 Ninakulilia wewe, ee Yawe, moto umemaliza malisho katika mbuga, ndimi za moto zimeteketeza miti katika mashamba. 20 Hata nyama wa pori wanakulilia wewe, maana, vijito vya maji vimekauka, moto umemaliza malisho katika mbuga. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo