Yobu 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kisha Yobu akajibu: 2 Kweli ninajua kama ni hivi. Lakini mutu anaweza namna gani kuwa haki mbele ya Mungu? 3 Kama mutu angesubutu kushindana naye, hataweza kufika mbali, hata kujibu ulizo moja kati ya elfu. 4 Yeye ni mwenye hekima sana na nguvu nyingi. Nani aliyepingana naye, akashinda? 5 Yeye anahamisha milima bila yenyewe kutambua, anaipindua mbali kwa hasira yake. 6 Yeye anaitikisa dunia kutoka pahali pake, na nguzo zake zinatetemeka. 7 Anaamuru jua lisipande, anafunika nyota zisiangaze. 8 Yeye peke yake alitandaza mbingu, na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. 9 Yeye aliweka makundi ya nyota katika anga: Dubu, Orioni, Kilimia, na Vyumba vya Kusini. 10 Ndiye anayetenda mambo makubwa yasiyoeleweka, mambo ya ajabu yasiyokuwa na hesabu. 11 Anapita karibu nami lakini simwoni, kisha anajiendea zake bila mimi kumutambua. 12 Yeye akitwaa kitu kwa rafla, nani anayeweza kumuzuia? Nani anayeweza kumwuliza: “Unafanya nini?” 13 Mungu hatazuia hasira yake; Rahabu na wasaidizi wake wanainama chini mbele yake. 14 Nitaweza namna gani basi kumujibu Mungu? Nitachagua wapi maneno ya kumwambia? 15 Ingawa sina kosa, siwezi kumujibu. Ninapaswa kumwomba mwamuzi wangu huruma. 16 Hata kama ningemwita naye akijibu, nisingeweza kuamini kwamba ananisikiliza. 17 Yeye ananiponda kwa zoruba, anaongeza vidonda vyangu bila sababu. 18 Haniachi hata nipumue; maisha yangu anayajaza uchungu. 19 Kama ni kushindana, yeye ana nguvu sana! Na kama ni kutafuta juu ya haki, nani atakayemuleta mbele ya tribinali? 20 Ingawa sina kosa, maneno yangu yenyewe yangenihukumu. Ingawa mimi ni mukamilifu, yangehakikisha kwamba mimi ni mupotovu. 21 Mimi ni mukamilifu. Siangalii nafsi yangu. Ninachukia maisha yangu. 22 Yote ni mamoja, kwa hiyo ninasema: Mungu anawaangamiza wakamilifu na waovu. 23 Musiba unapoleta kifo cha rafla, anachekelea hasara ya wasiokuwa na kosa. 24 Inchi ikitiwa katika utawala wa mwovu, Mungu anafunga macho ya waamuzi wake! Kama si yeye anayefanya hivyo, ni nani basi? 25 Siku zangu zinaenda mbio kuliko mukimbiaji, zinakimbia bila kuona faida. 26 Zinapita mbio kama mashua ya matete, kama tai anayerukia mawindo yake. 27 Ninasema: “Nitasahau malalamiko yangu, niondoe uso wangu wa huzuni na kuwa na furaha!” 28 Lakini ninaogopa maumivu yangu yote, maana ninajua Mungu hataniona kuwa sina kosa. 29 Ikiwa nitahukumiwa kuwa na kosa, kwa nini basi nijisumbue bure? 30 Hata kama nikinawa na teluji, na kujitakasa mikono kwa sabuni, 31 hata hivyo, atanitumbukiza katika shimo kwenye uchafu, na nguo zangu zitanichukia. 32 Mungu si mutu kama mimi nipate kumujibu, hata tuweze kwenda katika tribinali pamoja. 33 Hakuna mwamuzi kati yetu ambaye angetuamua sisi wawili. 34 Mungu aniondolee hiyo fimbo ya kunipiga, na kitisho chake kisinitie hofu! 35 Halafu ningeweza kusema bila kumwogopa; maana si vile ninavyokuwa ndani yangu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo