Yobu 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Halafu Bildadi wa inchi ya Suhi akamujibu Yobu: 2 Utasema mambo haya mpaka wakati gani? Mpaka wakati gani maneno yako yatakuwa matupu kama upepo? 3 Maana, unazani Mungu anapotosha sheria? Au, Mungu Mwenye Uwezo anapotosha haki? 4 Kama watoto wako wamemukosea Mungu, yeye amewalipiza matokeo ya makosa yao. 5 Kama utamutafuta Mungu na kumusihi yule Mungu Mwenye Uwezo, 6 kama wewe uko safi ndani ya moyo na wa usawa, kweli Mungu atakuja kukusaidia, na kukujalia makao unayostahili. 7 Na ingawa ulianza kuishi kwa uzaifu, maisha yako ya mwisho yatakuwa bora zaidi. 8 Tafazali, ujifunze kwa wale waliotutangulia; shika mambo ambayo wazee walitambua. 9 Sisi ni watu wa juzijuzi tu, hatujui kitu; siku zetu katika dunia ni kivuli kinachopita. 10 Lakini wao watakufundisha na kukuambia mambo waliyopata kuyatoa katika maarifa yao. 11 Nyasi zinaota tu penye tingitingi, matete yanastawi pahali panapokuwa maji. 12 Hata kama yamechanua na bila kukatwa, yakikosa maji yananyauka mbele ya mimea mingine. 13 Ndivyo wote wanaomusahau Mungu wanavyokuwa. Tumaini la wasiomwamini Mungu litapotea. 14 Tegemeo lao linavunjika, tumaini lao ni utando wa buibui. 15 Wanaegemea nyumba yao lakini haitasimama, wanaishikilia lakini haidumu. 16 Wako kama ua ambalo jua linapotoka linastawi; linaeneza matawi yake katika bustani yake, 17 mizizi yake inajisokotasokota kwenye mawe, nalo linaenda kuchunguza ndani ya jiwe. 18 Lakini likiangamizwa kutoka makao yake, hayo yatalikana yakisema: “Sijakuona bado.” 19 Ile ndiyo furaha ya mwisho wake, na pahali pake patachipuka mengine. 20 Sikia! Mungu hatakataa mutu mukamilifu, wala hatasaidia waovu. 21 Lakini atajaza kinywa chako kicheko, na midomo yako sauti ya furaha. 22 Wale wanaokuchukia watapata haya, makao ya waovu yatatoweka kabisa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo