Yobu 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Ita sasa, uone kama kuna wa kukuitikia. Ni nani kati ya watakatifu utakayemwita? 2 Kweli mahangaiko yanamwua mupumbafu, na wivu unamwangamiza mujinga. 3 Nimepata kuona mupumbafu akistawi, lakini kwa rafla nikalaani makao yake. 4 Watoto wake hawana usalama. Wanaonelewa katika tribinali, na hakuna mutu wa kuwatetea. 5 Mazao yake yanakuliwa na wenye njaa, hata ngano iliyoota kati ya miiba. Wenye tamaa wananyanganya utajiri wake. 6 Kwa kawaida mateso hayatoki katika mavumbi, wala matatizo hayachipuki katika udongo. 7 Lakini mwanadamu anazaliwa apate taabu, kama vile cheche za moto zinavyoruka juu. 8 Kwa ngambo yangu, mimi ningemugeukia Mungu, ningemutolea Mungu maneno yangu, 9 yeye anayetenda mambo makubwa yasiyochunguzika, anayetenda maajabu yasiyohesabika. 10 Ananyeshea inchi mvua, anapeleka maji katika mashamba. 11 Anainua juu wanaokuwa zaifu; wenye kuomboleza anawapa usalama. 12 Anavunja mipango ya wadanganyifu, matendo yao yasipate mafanikio. 13 Anawanasa wenye hekima kwa werevu wao, anakomesha mara moja mipango ya waovu. 14 Wao wanapatwa na giza wakati wa muchana; muchana kati wanapapasapapasa kama vile usiku. 15 Lakini Mungu anawaokoa wayatima wasiuawe, anawaponyesha wakosefu toka katika mikono ya wenye nguvu. 16 Hivyo wamasikini wanapata tumaini, nao uovu unakomeshwa. 17 Heri mutu yule anayeazibiwa na Mungu! Hivyo usizarau Mungu Mwenye Uwezo anapokuazibu. 18 Maana yeye anaumiza na tena anatunza, anatia kidonda na kwa mukono wake anaponyesha. 19 Atakuokoa mara sita toka katika magumu; hata mara saba hasara haitakugusa. 20 Atakuepusha toka kifo wakati wa njaa, toka mapigo ya upanga wakati wa vita. 21 Utakingwa salama na mashambulio ya ulimi, wala hautaogopa maangamizi yanapokuja. 22 Maangamizi na njaa vinapokuja, utacheka, wala hautaogopa nyama wakali wa inchi. 23 Nawe utapatana na mawe ya shamba, na nyama wakali watakuwa na amani nawe. 24 Utakaa na amani katika nyumba yako; utachunguza makundi yako ya nyama, utaona yote iko. 25 Utaona vilevile wazao wako watakuwa wengi, wengi kama majani katika mashamba. 26 Utashuka katika kaburi ukiwa na miaka yenye kutimia, kama vile muganda wa ngano uliokomaa vizuri. 27 Basi haya ndiyo mambo tuliyochunguza. Ni hivi tu. Uyasikie na kuyaelewa kwa faida yako. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo