Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yobu 42 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Kisha Yobu akamujibu Yawe:

2 Ninajua kwamba unaweza kila kitu, lolote unalokusudia haliwezi kuzuiliwa.

3 Ulisema kwamba nilivuruga mipango yako bila akili. Kweli nilitamka kitu ambacho sikuelewa, mambo ya ajabu sana kwangu ambayo sikukuwa ninayajua.

4 Uliniambia nisikilize nawe utaniambia; kwamba utaniuliza nami nikujibu.

5 Kweli nilikuwa nimesikia habari zako kwa masikio tu, lakini sasa ninakuona kwa macho yangu mwenyewe.

6 Kwa hiyo ninatubu na kujihukumu; ninajinyenyekeza na kuikaa juu ya mavumbi na majivu.


Mwisho wa habari ya Yobu

7 Yawe alipomaliza kuongea na Yobu, akamwambia Elifasi wa inchi ya Temani: “Kasirani yangu imewaka juu yako na warafiki zako wawili maana hamukusema ukweli juu yangu kama vile mutumishi wangu Yobu alivyofanya.

8 Kwa hiyo mutwae ngombe dume saba na kondoo dume saba, muende kwa mutumishi wangu Yobu, mutoe nyama wale kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa ajili yenu. Naye mutumishi wangu Yobu atawaombea, nami nitaisikiliza maombi yake na kuacha kuwatendea kulingana na upumbafu wenu; maana hamukusema ukweli juu yangu kama mutumishi wangu Yobu alivyofanya.”

9 Basi, Elifasi wa inchi ya Temani, Bildadi wa inchi ya Shua, na Zofari wa inchi ya Namati, wakafanya kama vile Yawe alivyowaambia. Yawe akapokea maombi ya Yobu.

10 Nyuma ya Yobu kuwaombea warafiki zake, Yawe akamurudishia Yobu hali yake ya kwanza. Akamupa mara mbili ya yote aliyokuwa nayo pale mbele.

11 Kisha wandugu zake, wadada zake na warafiki wote waliomufahamu mbele wakamwendea kwake, wakakula chakula pamoja naye. Wakamupa pole na kumufariji kwa ajili ya mateso yote ambayo Yawe alikuwa amemuletea. Kila mumoja wao akamupa Yobu feza na pete ya zahabu.

12 Katika miaka ya Yobu iliyofuata, Yawe alimubariki zaidi kuliko hata alivyokuwa amemubariki pale mbele. Basi Yobu akakuwa na kondoo elfu kumi na ine, ngamia elfu sita, ngombe elfu mbili na punda dike elfu moja.

13 Alikuwa vilevile na watoto wanaume saba na wabinti watatu.

14 Binti yake wa kwanza alimupa jina Yemima, wa pili Kezia, na wa mwisho Kereni-Hapuki.

15 Katika inchi yote hiyo hakukukuwa wanawake waliokuwa wazuri kama vile wabinti wa Yobu. Baba yao akawaachia urizi kama vile alivyowaachia kaka zao.

16 Nyuma ya pale, Yobu aliishi miaka mia moja makumi ine, akawaona vijukuu na vitukuu vyake vyote mpaka kizazi cha ine.

17 Basi, Yobu akakufa akiwa muzee wa miaka mingi.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan