Yobu 38 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anamujibu Yobu 1 Halafu Yawe akamujibu Yobu kutoka katika zoruba: 2 Nani wewe unayevuruga mipango yangu kwa maneno yasiyokuwa na akili? 3 Ujikaze kama mwanaume, nami nitakuuliza nawe utanijibu. 4 Ulikuwa wapi nilipoiweka misingi ya dunia? Uniambie, kama una maarifa. 5 Ni nani aliyeweka vipimo vyake, unajua bila shaka! Au nani aliyenyoosha kamba juu yake kwa kuipima? 6 Nguzo za dunia zimesimikwa juu ya nini, au nani aliyeliweka jiwe lake la musingi, 7 nyota za asubui zilipokuwa zikiimba pamoja, na wana wa Mungu wakapiga vigelegele vya shangwe? 8 Ni nani aliyefunga mafuriko ya bahari wakati yalipozuka na kuvuma kutoka katika vilindi? 9 Ni nani aliyefunika bahari kwa mawingu na kuiviringishia giza kubwa, 10 aliyeiwekea bahari mipaka na kuizuia kwa vifungio na milango 11 na kuiambia: “Mwisho wako ni hapa, si zaidi! Mawimbi yako ya nguvu yatakomea hapa!” 12 Yobu, tangu uzaliwe umekwisha kuamuru kupambazuke na kufanya mapambazuko yajue pahali pake, 13 kusudi yapate kukamata dunia kwa pembe zake na kuwatikisa watenda mabaya? 14 Dunia inageuka na kupata rangi kama nguo; kama udongo wa mufinyanzi unavyogeuzwa na muhuri. 15 Lakini waovu watanyimwa mwangaza wao, mukono wanaonyoosha kwa kupiga watu utavunjwa. 16 Umepata kufika kwenye chemichemi za bahari au kutembea juu ya sakafu ya kilindi cha bahari? 17 Umekwisha kuonyeshwa milango ya kifo au kuona milango ya makao ya giza kubwa? 18 Unajua ukubwa wa dunia? Uniambie kama unajua haya yote. 19 Makao ya mwangaza yako wapi? Kwenye nyumba ya giza ni wapi, 20 kusudi upate kupeleka kwenye makao yake, na kuifahamu njia ya kwenda kule kwake. 21 Wewe unapaswa kujua, wewe ambaye umekwisha ishi miaka mingi! 22 Umekwisha kuingia katika akiba za teluji, au kuona akiba za mvua ya mawe 23 ambavyo nimeviweka kwa ajili ya wakati wa fujo, kwa ajili ya siku ya mapigano na vita? 24 Unajua mwangaza unagawanywa kwa njia gani, au namna gani upepo wa mashariki unavyosambazwa katika dunia? 25 Nani aliyechora katika anga njia kwa ajili ya mvua? Nani aliyeonyesha radi njia yake katika mawingu, 26 nayo ikasababisha mvua kunyesha katika inchi kusikoishi mutu na katika jangwa ambako hakuna mutu, 27 kusudi ikunyweshe inchi kavu na yenye kukauka na kuifanya ioteshe majani? 28 Mvua ina baba? Au nani amezaa matone ya umande? 29 Barafu ilitoka katika tumbo la nani? Nani aliyezaa teluji? 30 Maji yanageuka kuwa magumu kama jiwe, na uso wa bahari unaganda. 31 Angalia makundi ya nyota: Unaweza kuifunga minyororo Kilimia, au kuviregeza vifungo vya Orioni? 32 Unaweza kuongoza nyota kwa wakati wake, au kumwongoza Dubu pamoja na vitoto vyake? 33 Unayajua maagizo ya mbingu? Unaweza kuzipangia utaratibu wao katika dunia? 34 Unaweza kupiga vigelegele na kuyaamuru mawingu yakufunike kwa mutiririko wa mvua? 35 Wewe ukiamuru umeme uangaze, utakufikia na kusema: “Nipo hapa”? 36 Ni nani aliyemujulisha kwarara kujaa kwa muto Nili au aliyemwambia jogoo kwamba mvua inakuja? 37 Nani mwenye akili ya kuweza kuhesabu mawingu au kuinamisha vibuyu vya maji kule katika mbingu 38 kusudi mavumbi katika dunia yagandamane na udongo ushikamane na kuwa matope? 39 Unaweza kumwindia simba dike au kuishibisha hamu ya simba wakali 40 wanapojificha ndani ya matundu yao, au kulala katika maficho wakivizia? 41 Ni nani anayewapa vibombobombo chakula chao, vitoto vyao vinaponililia mimi Mungu, na kurukaruka huku na kule kwa njaa? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo