Yobu 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yobu anaomboleza 1 Kisha hayo, Yobu akaamua kusema. Akalaani siku aliyozaliwa. 2 Yobu akasema: 3 Iangamie siku ile niliyozaliwa, usiku ule iliposemwa: “Mimba ya mutoto mwanaume imepatikana.” 4 Siku ile ikuwe giza! Na kutoka juu Mungu asijishugulishe nayo, wala mwangaza wowote usiiangaze! 5 Itawaliwe na giza kubwa sana, mawingu mazito yaifunike. Giza la muchana liitishe! 6 Usiku ule giza kubwa liufunike! Usihesabiwe katika siku za mwaka, usitiwe katika hesabu ya siku za mwezi. 7 Usiku ule ukuwe tasa, sauti ya furaha isiingie ndani yake. 8 Ulaaniwe na wale wanaolaani siku, wale wafundi wanaoamusha Leviatani. 9 Nyota zake za mapambazuko zififie, utamani kupata mwangaza, lakini usipate, wala usione mwangaza wa mapambazuko. 10 Usiku ule ukuwe hivi, kwa sababu haukufunga tumbo la mama, wala kuficha taabu nisizione. 11 Kwa nini sikukufa nilipozaliwa? Kwa nini kutoka tu katika tumbo sikutoweka? 12 Kwa nini mama yangu alinizaa? Kwa nini nilipata kunyonya? 13 Maana ningekuwa nimezikwa, kimya; ningelala na kupumzika 14 pamoja na wafalme na watawala wa dunia waliojijengea upya miji kutoka mabomoko, 15 pamoja na wakubwa waliokuwa na zahabu, waliojaza nyumba zao feza tele. 16 Kwa nini sikukuwa kama mutoto aliyezaliwa mufu ambaye hakuona mwangaza? 17 Kule kwa wafu waovu hawasumbui mutu, kule wanaochoka wanapumzika. 18 Kule wafungwa wanastarehe pamoja, hawasikii hata kidogo sauti ya wasimamizi. 19 Wakubwa na wadogo wako kule, nao watumwa wamepata uhuru mbali na bwana zao. 20 Kwa nini kumujalia mwangaza na uzima yule anayekuwa katika taabu, anayekuwa na huzuni ndani ya moyo, 21 anayetamani kifo lakini hakufi, anayetafuta kifo kuliko hazina iliyofichwa. 22 Mutu kama yule atashangilia sana na kufurahi atakapokufa na kuzikwa! 23 Kwa nini kumujalia uzima mutu ambaye njia zake zimefungwa, mutu ambaye Mungu amemwekea kizuizi? 24 Kuugua ndicho chakula changu. Malalamiko yangu yanatiririka kama maji. 25 Kile ninachoogopa kimenipata; ninachohofu ndicho kilitokea. 26 Sina amani wala utulivu; sipumziki, taabu imenifikia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo