Yobu 23 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kisha Yobu akajibu: 2 Hata leo malalamiko yangu ni ya uchungu. Ninapata maumivu na kuugua. 3 Heri ningejua pahali nitakapomupata Mungu! Ningeweza kwenda hata karibu naye. 4 Ningeleta maneno yangu mbele yake, na kumutolea utetezi wangu. 5 Ningeweza kujua atakachonijibu, na kuelewa atakachoniambia. 6 Angeshindana nami kwa nguvu zake zote? Hapana! Bila shaka angenisikiliza. 7 Pale, mutu wa usawa anaweza kujitetea. Mungu, mwamuzi wangu angeamua kuwa sina kosa milele. 8 Ninakwenda mbele, lakini simupati; ninarudi nyuma, lakini siwezi kumwona. 9 Ninamutafuta upande wa kushoto lakini simwoni; ninageukia upande wa kuume, lakini siwezi kumwona. 10 Lakini yeye anajua njia ninayofuata; atakapomaliza kunipima nitatoka mule safi kama zahabu. 11 Ninamufuata kabisa; njia yake nimeishikilia wala sikugeuka pembeni. 12 Sijaacha hata kidogo kushika amri yake; maneno yake nimeyatunza ndani ya moyo wangu. 13 Lakini yeye habadiliki, nani anayeweza kumugeuza? Kitu anachotaka, ndicho anachofanya! 14 Anatimiza yote aliyonipangia; na mengi kama hayo yako katika akili yake. 15 Kwa hivyo, ninatetemeka kwa hofu mbele yake; hata nikifikiri tu ninapatwa na woga. 16 Mungu amefanya moyo wangu uregee, Mungu Mwenye Uwezo amenitia hofu. 17 Maana nimepatwa na giza, na giza kubwa limetanda katika uso wangu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo