Yobu 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Jaribu la pili 1 Ikatokea tena siku ingine, wamalaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Yawe. Shetani akakuja kuwa pamoja nao. 2 Yawe akamwuliza Shetani: “Unatoka wapi wewe?” Naye Shetani akamujibu Yawe: “Ninatoka kutembeatembea na kuzungukazunguka katika dunia.” 3 Yawe akamwambia Shetani: “Umemwona vizuri mutumishi wangu Yobu? Katika dunia hakuna mwingine anayekuwa kama yeye. Yeye ni mutu mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu. Yeye anadumu katika ukamilifu, ingawa wewe umenisukuma nimwangamize bure.” 4 Shetani akamujibu Yawe: “Ngozi kwa ngozi! Mutu anatoa kila kitu anachokuwa nacho kusudi aokoe maisha yake. 5 Lakini sasa, unyooshe mukono wako umuguse mwili wake. Utaona namna atakutukana waziwazi.” 6 Yawe akamwambia Shetani: “Basi, unaweza kumufanya vile unavyotaka, lakini usimwue tu.” 7 Kwa hiyo Shetani akaondoka mbele ya Yawe, akamutesa Yobu kwa vidonda vikali tangia kwenye miguu yake mpaka kwenye kichwa chake. 8 Yobu akatwaa kigae, akajikuna nacho na kuikaa kwenye majivu. 9 Muke wake akamwambia: “Unaendelea kushikilia ukamilifu wako? Umutukane Mungu, ukufe.” 10 Akamujibu: “Wewe unasema kama wanawake wapumbafu. Tukipokea mazuri kutoka kwa Mungu, kwa nini tukatae kupokea vilevile mabaya kutoka kwake?” Katika mambo hayo yote, Yobu hakusema neno lolote la kumukosea Mungu. Warafiki watatu wa Yobu wanafika 11 Warafiki watatu wa Yobu walisikia juu ya hasara zote zilizomupata Yobu, wakaamua kwa pamoja waende kumupa pole na kumufariji. Majina yao ni: Elifasi kutoka inchi ya Temani, Bildadi wa inchi ya Suhi na Zofari wa inchi ya Namati. 12 Walipomwona kwa mbali hawakumutambua. Basi, wakaanza kulalamika na kulia. Wakapasua nguo zao, wakarusha mavumbi katika anga na juu ya vichwa vyao. 13 Kisha wakaikaa kwenye udongo pamoja na Yobu kwa siku saba, muchana na usiku, bila kumwambia neno lolote maana waliona mateso yake kuwa makubwa sana. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo