Yobu 15 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Sehemu ya pili ya Mazungumuzo ( 15.1–21.34 ) Masemi ya pili ya Elifasi 1 Kisha Elifasi wa inchi ya Temani, akajibu: 2 Mwenye hekima anajibu bila kufikiri na kujaa maneno ya burebure? 3 Anajitetea kwa maneno yasiyofaa na yasiyokuwa na maana? 4 Lakini wewe, woga wa Mungu si ndani yako; nawe unakataa kufikiri mbele ya Mungu. 5 Uovu wako ndio unaongoza kinywa chako, nawe unachagua kusema kama wadanganyifu. 6 Maneno yako mwenyewe yanakuhukumu, sio mimi; masemi yako yanashuhudia juu yako. 7 Wewe ndiwe mutu wa kwanza kuzaliwa? Wewe ulizaliwa mbele ya kuwa kwa vilima? 8 Ulipata kuwa katika shauri la Mungu? Wewe ndiwe peke yako mwenye hekima? 9 Unajua kitu gani tusichokijua sisi? Unafahamu kitu gani tusichokifahamu sisi? 10 Kati yetu kuna wazee wenye hekima, wenye miaka mingi kuliko baba yako. 11 Faraja Mungu anazokupa ni ndogo sana? Au neno lake la upole kwako si kitu? 12 Mbona moyo unakusukuma kukasirika na kutoa macho makali, 13 hata kumwasi Mungu na kusema maneno mabaya kama yale? 14 Mutu ni nini hata aweze kuwa na moyo safi? Yule aliyezaliwa na mwanamuke atapata kuwa mwenye haki? 15 Ikiwa Mungu hawaaminii hata wamalaika wake, nazo mbingu si safi mbele yake, 16 kefu sasa mwanadamu anayekuwa chukizo na mupotovu, mwanadamu anayetenda uovu kama kunywa maji! 17 Sasa unisikilize, nami nitakuonyesha, nitakuambia yale niliyoona, 18 mafundisho ya wenye hekima, mambo ambayo wazee wao hawakuficha, 19 ambao Mungu aliwapa hiyo inchi peke yao, wala hakuna mugeni aliyepita kati yao. 20 Mwovu atateseka kwa maumivu siku zote, miaka yote watesaji waliyopangiwa. 21 Sauti za vitisho zitamupigia kelele katika masikio. Anapozani amestawi, mwangamizi atamushambulia. 22 Mwovu hana tumaini la kutoka katika giza; mwisho wake ni kufa kwa upanga. 23 Anatangatanga kutafuta chakula, akisema: “Kiko wapi?” Anajua kwamba siku ya giza inamukaribia. 24 Taabu na uchungu, vinamutisha; vinamushambulia kama jeshi la mufalme anayekuwa tayari kwa vita 25 kwa sababu amenyoosha mukono wake apigane na Mungu na kujivuna kumupinga yule Mungu Mwenye Uwezo. 26 Anakimbia kwa kiburi kwa kumushambulia, akiwa na ngao yenye mafundo makubwa. 27 Uso wake umenona kwa mafuta, na kiuno chake kimenenepa. 28 Ameishi katika miji iliyoachwa wazi, katika nyumba zisizokaliwa na mutu, nyumba zilizotakiwa zikuwe lundo la uharibifu. 29 Mutu yule hatakuwa tajiri hata kidogo; wala utajiri wake hautadumu katika dunia. 30 Hataponyoka giza la kifo. Ndimi za moto zitakausha vichipukizi vyake, maua yake yatapeperushwa na upepo. 31 Aache kutumainia udanganyifu, maana udanganyifu ndio utakaokuwa zawadi yake. 32 Atalipwa kikamilifu mbele ya kufa kwake, na wazao wake hawatadumu. 33 Atakuwa kama muzabibu unaoangusha zabibu mbichi, kama muzeituni unaopoteza maua yake. 34 Wote wasiomwogopa Mungu hawatapata watoto, moto utateketeza mahema ya wanaokula kituliro. 35 Wanatunga udanganyifu na kuzaa uovu. Mioyo yao inapanga udanganyifu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo