Yobu 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Halafu Yobu akajibu: 2 Hakika! Ninyi ni watu wa hekima. Hekima itakufa wakati ule mutakapokufa. 3 Mimi nami nina ufahamu kama ninyi. Mimi si mutu wa akili ndogo kuliko ninyi. Yote muliyosema kila mutu anajua. 4 Nilikuwa mutu wa kumwomba Mungu na kupata jibu lake. Sasa, watu wananichekelea. Wanachekelea mutu mukamilifu, mwenye haki. 5 Mutu mwenye raha anazarau taabu; taabu ni kwa wale wanaoteleza. 6 Makao ya wanyanganyi yana amani. Wenye kumuchokoza Mungu wako salama; nguvu yao ni mungu wao. 7 Lakini uulize nyama nao watakufundisha; uulize ndege nao watakuambia. 8 Au uulize mimea nayo itakufundisha; sema na samaki nao watakuarifu. 9 Nani kati ya viumbe hivyo, asiyejua kwamba Yawe ametenda yale? 10 Uzima wa kila kiumbe, pumzi ya kila mwanadamu, viko katika mikono yake. 11 Sikio halipimi maneno kama vile ulimi unavyoonja chakula? 12 Hekima iko kwa watu wazee, maarifa kwa walioishi muda murefu. 13 Lakini hekima na uwezo ni vya Mungu. Yeye ana maarifa na ujuzi. 14 Akibomoa, hakuna anayeweza kujenga upya; akifunga mutu, hakuna anayeweza kumufungua. 15 Akizuia mvua, inchi inakauka; akiifungulia, inchi inaharibika. 16 Yeye ana nguvu na hekima. Wanaodanganywa na wanaodanganya ni wake. 17 Anawatembeza washauri miguu wazi, anawafanya waamuzi kuwa wapumbafu. 18 Anavua wafalme mikaba yao, na kuwafunga kamba za wafungwa katika viuno. 19 Anaacha makuhani watembee uchi; na kuwaangusha wenye nguvu. 20 Ananyanganya washauri zawadi yao ya kusema, anaondolea wazee ufahamu wao. 21 Anamwagia wakubwa mazarau, anawaondolea wenye uwezo nguvu yao. 22 Anafunua vilindi vya giza, na kuleta katika mwangaza mambo yaliyokuwa katika giza. 23 Anayaongeza mataifa kisha anayaangamiza, anayafanya yapanuke kisha anayatawanya. 24 Anaondolea viongozi wa watu ujuzi wao, anawafanya watangetange katika jangwa kusikokuwa njia, 25 wakipapasapapasa katika giza kusikokuwa mwangaza; na kuwafanya wapepesuke kama walevi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo