Yobu 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Shetani amujaribu Yobu 1 Kulikuwa mutu mumoja katika inchi ya Usi, aliyeitwa Yobu. Mutu yule alikuwa mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu. 2 Yobu alikuwa na wana saba na wabinti watatu. 3 Alikuwa na mali, kondoo elfu saba, ngamia elfu tatu, ngombe elfu moja, punda dike mia tano, na watumishi wengi sana. Yeye alikuwa wa heshima kuliko watu wote kule upande wa mashariki. 4 Mara kwa mara, wana wa Yobu walifanya karamu katika nyumba ya kila mumoja wakifuatana. Waliwaalika wadada zao kula na kunywa pamoja nao. 5 Kila mara karamu ilipomalizika, Yobu aliita wana wake kusudi awatakase. Aliamuka asubui mapema kisha karamu, akatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto kwa ajili ya kila mumoja wao maana aliwaza: “Labda wana wangu wametenda zambi na kumutukana Mungu ndani ya mioyo yao.” 6 Basi, ikatukia siku moja wamalaika wa Mungu walikwenda kukutana mbele ya Yawe. Shetani akakuja kuwa pamoja nao. 7 Yawe akamwuliza Shetani: “Unatoka wapi wewe?” Shetani akamujibu Yawe: “Ninatoka kutembeatembea na kuzungukazunguka katika dunia.” 8 Yawe akamwambia Shetani: “Umemwona vizuri mutumishi wangu Yobu? Katika dunia hakuna mwingine anayekuwa kama yeye. Yeye ni mutu mukamilifu, wa usawa, mwenye kumwogopa Mungu na mwenye kuepukana na uovu.” 9 Shetani akamujibu Yawe: “Yobu anamwogopa Yawe kwa bure? 10 Si wewe mwenyewe unamulinda pande zote pamoja na jamaa yake na kila kitu anachokuwa nacho? Wewe umemubariki na mali yake imeongezeka katika inchi. 11 Lakini sasa, unyooshe mukono wako uguse mali yake. Utaona namna atakutukana waziwazi!” 12 Yawe akamwambia Shetani: “Basi, unaweza kufanya vile unavyotaka juu ya mali yake. Lakini tu yeye mwenyewe usimuguse.” Basi, Shetani akaondoka mbele ya Yawe. Jaribu la kwanza la Yobu 13 Siku moja, wana na wabinti wa Yobu walikuwa wanakula na kunywa divai pamoja katika nyumba ya kaka yao mukubwa. 14 Basi, mutumishi akafika kwa Yobu, akamwambia: “Tulikuwa tunalima kwa majembe ya kukokotwa na ngombe. Punda nao walikuwa wanakula pale karibu. 15 Basi Wasabea wakatushambulia na kunyanganya nyama na kuua watumishi kwa upanga. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” 16 Alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akafika, akasema: “Umeme wa radi umewachoma na kuwateketeza kondoo na watumishi. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” 17 Yule naye alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akafika, akasema: “Wakaldea walijipanga makundi matatu, wakashambulia ngamia, wakawatwaa, na wakaua watumishi wako kwa upanga! Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” 18 Alipokuwa hajamaliza kusema, mwingine akakuja, akasema: “Wana zako na wabinti zako walikuwa wanakula na kunywa divai katika nyumba ya kwa kaka yao mukubwa. 19 Mara moja upepo mukali ukavuma kutoka katika jangwa, ukaipiga nyumba ile kila upande nayo ikawaangukia, na vijana wote wamekufa. Ni mimi tu peke yangu nimepona kwa kuja kukuletea habari.” 20 Kisha Yobu akasimama, akapasua nguo yake, akanyoa nywele zake, akajitupa chini na kumwabudu Mungu, 21 akisema: Nilikuja uchi katika dunia, nitaondoka uchi katika dunia. Yawe amenipa, Yawe ametwaa. Jina la Yawe litukuzwe. 22 Katika mambo haya yote Yobu hakutenda zambi wala hakumushitaki Mungu kuwa na kosa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo