Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoane 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu anaponyesha mutu aliyezaliwa kipofu

1 Yesu alipokuwa akipita katika njia, akaona mutu mumoja aliyekuwa kipofu tangu kuzaliwa kwake.

2 Wanafunzi wake wakamwuliza: “Mwalimu, kwa sababu gani mutu huyu alizaliwa kipofu? Ni kwa ajili ya malipizi ya zambi yake mwenyewe au zambi ya wazazi wake?”

3 Yesu akajibu: “Mutu huyu hakuzaliwa kipofu kwa ajili ya zambi yake wala zambi ya wazazi wake. Lakini amekuwa hivi kusudi matendo ya Mungu yaonekane kwa njia yake.

4 Imetupasa kufanya kazi za yule aliyenituma wakati kungali muchana, kwa sababu usiku unakaribia, wakati mutu asipoweza kutumika.

5 Wakati nikingali katika dunia, mimi ni mwangaza wa dunia.”

6 Yesu alipokwisha kusema vile, akatema mate chini, akayavuruga pamoja na mavumbi na kufanya matope kidogo, akayapakaa kwa macho ya yule kipofu

7 na kumwambia: “Kwenda unawe uso katika kisima cha Siloamu” (maana ya jina hili ni “Aliyetumwa”). Basi yule kipofu akaenda na kunawa uso, akarudi akiwa mwenye kuona.

8 Jirani zake na wale waliomwona zamani akiwa mwenye kuombaomba, wakasema: “Si mutu huyu ndiye yule aliyekuwa akiikaa chini na kuombaomba?”

9 Wamoja wakasema: “Ni yeye.” Lakini wengine wakasema: “Hapana, si yeye, anafanana naye tu.” Lakini yeye mwenyewe akasema: “Ni mimi.”

10 Basi wakamwuliza: “Macho yako yaliponyeshwa namna gani?”

11 Akajibu: “Mutu yule anayeitwa Yesu alifanya matope kidogo na kuyapakaa kwa macho yangu, na kuniambia kwamba niende kunawa uso katika kisima cha Siloamu. Nami nikaenda, nikanawa, na halafu nikapata kuona.”

12 Nao wakamwuliza tena: “Yule mutu yuko wapi?” Akajibu: “Sijui.”


Wafarisayo wanapeleleza habari za kipofu aliyeponyeshwa

13 Wakamupeleka yule mutu aliyekuwa kipofu kwa Wafarisayo.

14 Na siku ile Yesu alipofanya matope na kuponyesha macho ya mutu yule, ilikuwa siku ya Sabato.

15 Kwa hiyo Wafarisayo nao wakamwuliza namna gani alivyopata kuona. Naye akawaambia: “Alinipakaa matope kidogo kwa macho, nami nikanawa uso na sasa ninaona.”

16 Wafarisayo wamoja wakasema: “Mutu huyu hakutoka kwa Mungu kwa sababu hashiki sheria ya siku ya Sabato.” Lakini wengine wakasema: “Mutu mwenye zambi anaweza kuonyesha kitambulisho kama hiki?” Basi kukatokea mikorogano kati yao.

17 Wafarisayo wakamwuliza tena yule aliyekuwa kipofu: “Na wewe unasema nini juu ya yule aliyekuponyesha macho?” Akajibu: “Yeye ni nabii.”

18 Lakini wakubwa wa Wayuda hawakusadiki kama alikuwa kipofu na kwamba alikuwa sasa akiona mpaka walipowaita wazazi wake

19 na kuwauliza: “Huyu ndiye mwana wenu munayesema kama alizaliwa kipofu? Namna gani anaona?”

20 Wazazi wake wakawajibu: “Tunajua hakika kwamba huyu ni mwana wetu na kwamba alizaliwa kipofu.

21 Lakini hatujui kilichotokea hata anaona sasa, wala hatujui ni nani aliyemuponyesha macho. Yeye ni mutu muzima. Mumwulize yeye mwenyewe, naye atawaelezea maneno yake.”

22 Wazazi wake walisema hivi kwa sababu waliogopa wakubwa wa Wayuda. Wakubwa wale walikuwa wamekwisha kupatana kwamba mutu yeyote anayesadiki kuwa Yesu ndiye Kristo, atatengwa asiingie katika nyumba ya kuabudia.

23 Na hiyo ndiyo sababu wazazi wake walisema kwamba yeye ni mutu muzima, wamwulize.

24 Halafu wakubwa wa Wayuda wakamwita yule aliyekuwa kipofu kwa mara ya pili na kumwambia: “Sema ukweli mbele ya Mungu! Kwa ngambo yetu tunajua kwamba mutu yule ni mwenye zambi.”

25 Yeye akajibu: “Kama yeye ni mwenye zambi, mimi sijui. Neno moja ninalojua ni kwamba mimi nilikuwa kipofu na sasa ninaona.”

26 Wakamwuliza tena: “Yeye alikufanyia nini? Namna gani alikuponyesha macho?”

27 Naye akawajibu: “Nimekwisha kuwaelezea lakini hamupendi kusikia. Kwa sababu gani munataka niwaambie tena? Ninyi vilevile munataka kuwa wanafunzi wake?”

28 Wakamutukana, wakimwambia: “Wewe ndiwe mwanafunzi wa mutu yule! Sisi ni wanafunzi wa Musa.

29 Tunajua kwamba Mungu alisema na Musa, lakini hatujui pahali mutu yule anapotoka!”

30 Naye akawajibu: “Kweli neno hili ni la kushangaza kusema kwamba hamujui pahali alipotoka, ijapokuwa ameniponyesha macho.

31 Tunajua kwamba Mungu hasikilizi maombi ya wenye zambi, lakini anamusikiliza mutu yule anayemuheshimu na kufanya sawa anavyotaka.

32 Hatujasikia wakisema hata siku moja kwamba kuna mutu aliyeponyesha macho ya mutu aliyezaliwa kipofu.

33 Kama mutu huyu asingetoka kwa Mungu, hangeweza kufanya kitu.”

34 Wakamujibu: “Wewe, uko mwenye zambi kabisa tangu kuzaliwa kwako! Unataka kutufundisha?” Halafu wakamufukuza inje.


Kipofu aliyeponyeshwa anamwamini Yesu

35 Yesu akapata habari kwamba yule aliyekuwa kipofu amefukuzwa. Yesu alipokutana naye, akamwuliza: “Unamwamini Mwana wa Mutu?”

36 Yule mutu akamujibu: “Bwana, unielezee yeye ni nani, kusudi nipate kumwamini.”

37 Yesu akamwambia: “Umemwona, na ni yeye anayesema nawe sasa.”

38 Basi yule mutu akasema: “Bwana, ninaamini.” Naye akamwabudu Yesu.

39 Kisha Yesu akasema: “Nimekuja katika dunia kusudi hukumu ipate kufanyika; maana yake vipofu wapate kuona, nao wanaoona wapate kuwa vipofu.”

40 Wafarisayo wamoja waliokuwa pamoja naye waliposikia maneno haya, wakamwuliza: “Ni kusema sisi ni vipofu vilevile?”

41 Yesu akawajibu: “Mungekuwa vipofu, hamungekuwa na zambi. Lakini kwa maana munajidai kwamba munaona, mungali katika zambi.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan