Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoane 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mwanamuke muzinzi

1 Yesu vilevile akajiendea kwa mulima wa Mizeituni.

2 Na kesho yake asubui mapema akarudi tena katika hekalu. Watu wote wakamufikia, naye alipoikaa, akaanza kuwafundisha.

3 Halafu walimu wa Sheria pamoja na Wafarisayo wakaleta mbele yake mwanamuke mumoja aliyekamatwa katika uzinzi. Wakamusimamisha mbele ya watu wote

4 na kumwambia Yesu: “Mwalimu, mwanamuke huyu amekamatwa akizini.

5 Kufuatana na Sheria, Musa alituamuru kuwaua kwa mawe wanawake wa namna hii. Sasa, wewe unasema nini?”

6 Wao walisema hivi kwa kumupima, kusudi wapate sababu ya kumushitaki. Lakini Yesu akainama na kuandika juu ya udongo kwa kidole chake.

7 Nao walipozidi kumwuliza, Yesu akainuka na kuwaambia: “Mutu asiyekuwa na zambi kati yenu, akuwe wa kwanza kumutupia jiwe.”

8 Kisha akainama tena na kuandika juu ya udongo.

9 Wakati waliposikia maneno haya, wakaondoka wote mumoja kwa mumoja, wakianzia kwa wazee. Yesu akabaki pale peke yake pamoja na yule mwanamuke aliyekuwa akisimama mbele yake.

10 Na Yesu alipoinuka, akamwuliza: “Mama, wale watu wako wapi sasa? Hakuna hata mumoja kwa kukuhukumu?”

11 Mwanamuke yule akamujibu: “Bwana, hakuna mutu.” Basi Yesu akamwambia: “Mimi vilevile sikuhukumu. Ujiendee, lakini usifanye zambi tena.”]


Yesu ni mwangaza wa dunia

12 Yesu akawaambia watu tena: “Mimi ni mwangaza wa dunia. Yeye anayenifuata hatatembea katika giza hata kidogo, lakini atakuwa na mwangaza wa uzima.”

13 Kwa hiyo Wafarisayo wakamwambia: “Ushuhuda wako si wa kweli, kwa kuwa unajishuhudia wewe mwenyewe.”

14 Yesu akawajibu: “Hata nikijishuhudia mimi mwenyewe, ushuhuda wangu ni wa kweli, kwa sababu ninajua pahali nilipotoka na pahali ninapokwenda. Lakini ninyi hamujui pahali nilipotoka wala pahali ninapokwenda.

15 Ninyi munahukumu kwa kufuatana na mafikiri ya kimutu; lakini mimi simuhukumu mutu.

16 Lakini hata ningehukumu, hukumu yangu ingekuwa ya kweli, kwa sababu sihukumu peke yangu, lakini Baba aliyenituma ni pamoja nami.

17 Na imeandikwa hata katika Sheria yenu kama ushuhuda wa watu wawili ni wa kweli.

18 Ninajishuhudia mimi mwenyewe na Baba aliyenituma ananishuhudia vilevile.”

19 Basi wakamwuliza: “Baba yako yuko wapi?” Yesu akajibu: “Hamunijui mimi wala hamumujui Baba yangu. Kama mungenijua mimi, mungemujua Baba yangu vilevile.”

20 Yesu alisema maneno haya wakati alipokuwa akifundisha katika hekalu, kwenye sanduku za kuwekea matoleo. Hakuna mutu aliyemufunga, kwa sababu wakati wake ulikuwa haujatimia.


Hamuwezi kwenda pahali ninapokwenda

21 Yesu akawaambia watu tena: “Mimi ninajiendea, nanyi mutanitafuta, lakini mutakufa katika zambi zenu. Na zaidi ya hii hamuwezi kufika pahali ninapokwenda.”

22 Wakubwa wa Wayuda wakaulizana: “Yeye anasema kwamba hatuwezi kufika pahali anapokwenda; maana yake atakwenda kujiua?”

23 Yesu akawajibu: “Ninyi munatoka hapa chini, lakini mimi nimetoka juu. Ninyi ni wa dunia hii, lakini mimi si wa dunia hii.

24 Ni kwa sababu hii niliwaambia ninyi kama mutakufa katika zambi zenu. Musipoamini kwamba ‘Mimi Ndimi’, hakika mutakufa katika zambi zenu.”

25 Basi wakamwuliza: “Wewe ni nani?” Yesu akawajibu: “Mimi ni yule niliyewaambia tangu mwanzo.

26 Nina maneno mengi ya kusema juu yenu na ya kuwahukumu. Lakini yule aliyenituma ni wa kweli, nami ninajulisha dunia maneno yale niliyosikia kwake.”

27 Hawakujua kama alisema juu ya Baba yake.

28 Halafu Yesu akawaambia: “Wakati mutakapomunyanyua Mwana wa Mutu juu, mutafahamu kwamba ‘Mimi Ndimi.’ Na zaidi ya hii mutatambua kwamba sifanyi neno lolote kwa mapenzi yangu, lakini ninasema tu yale niliyofundishwa na Baba.

29 Yule aliyenituma ni pamoja nami; hakuniacha peke yangu, kwa sababu siku zote ninafanya maneno yanayomupendeza.”

30 Alipokuwa akisema maneno haya, watu wengi wakamwamini.


Uhuru wa kweli

31 Basi Yesu akawaambia wale Wayuda waliomwamini: “Kama mukitii mafundisho yangu, ninyi ni wanafunzi wangu hakika.

32 Halafu mutajua ukweli, na ukweli utawaweka huru.”

33 Wakamujibu: “Sisi ni wa uzao wa Abrahamu, wala hatujakuwa watumwa wa mutu hata siku moja. Namna gani basi unaweza kutuambia kwamba tutapata uhuru?”

34 Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: kila mutu anayefanya zambi ni mutumwa wa zambi.

35 Mutumwa hahesabiwi kuwa mumoja wa jamaa siku zote, lakini mwana anahesabiwa kuwa mumoja wa jamaa siku zote.

36 Kama Mwana akiwapatia uhuru, basi mutapata uhuru wa kweli.

37 Ninajua kwamba ninyi ni uzao wa Abrahamu. Lakini munatafuta kuniua, kwa sababu munakataa kukubali mafundisho yangu.

38 Mimi ninasema yale niliyoona kwa Baba yangu, lakini ninyi munafanya yale muliyosikia kutoka kwa baba yenu.”

39 Wakamujibu: “Baba yetu ni Abrahamu.” Yesu akawaambia: “Kama mungekuwa watoto wa Abrahamu, basi mungefanya matendo yale Abrahamu aliyofanya.

40 Lakini sasa munatafuta kuniua ijapokuwa nimewaambia ukweli niliousikia kutoka kwa Mungu. Abrahamu hakufanya vile.

41 Ninyi munafanya matendo yale baba yenu anayofanya.” Wakamujibu: “Sisi si watoto wa haramu. Tuko na baba mumoja, naye ndiye Mungu.”

42 Yesu akawaambia: “Kama Mungu angekuwa Baba yenu, mungenipenda, kwa maana nimetoka kwa Mungu na sasa niko hapa. Sikukuja kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini yeye ndiye aliyenituma.

43 Kwa sababu gani hamuelewi maneno ninayowaambia? Ni kwa sababu hamutaki kusikia maneno yangu.

44 Baba yenu ni Shetani, nanyi munataka kutimiza sawa vile huyo baba yenu anavyotamani. Yeye ni mwuaji siku zote, naye hajasimama katika ukweli, kwa sababu ndani yake hakuna ukweli. Wakati anaposema uongo, masemi yake yanatokana na tabia yake, kwa sababu yeye ni mwongo na baba ya uongo.

45 Na kwa ngambo yangu, ninyi hamuniamini kwa maana ninasema ukweli.

46 Nani kati yenu anaweza kuhakikisha kwamba nimefanya zambi? Ikiwa ninasema ukweli, kwa sababu gani hamuniamini?

47 Anayekuwa mutu wa Mungu anasikia maneno ya Mungu. Hamusikii, kwa sababu ninyi si watu wa Mungu.”


Yesu na Abrahamu

48 Wayuda wakamujibu: “Sisi tulikuwa na haki ya kusema kwamba wewe ni Musamaria na kwamba uko na pepo.”

49 Yesu akajibu: “Mimi sina pepo, lakini ninamuheshimu Baba yangu, nanyi munanikosea heshima.

50 Mimi sijitafutii sifa yangu mwenyewe, lakini kuna mumoja anayeitafuta kwa ajili yangu, naye ndiye mwenye uwezo wa kuhukumu.

51 Kweli, kweli ninawaambia: kama mutu akishika maneno yangu, hatakufa hata milele.”

52 Halafu Wayuda wakamwambia: “Sasa tunajua hakika kwamba uko na pepo! Abrahamu amekufa, na manabii wamekufa vilevile, nawe unasema kwamba mutu akishika maneno yako, hatakufa hata milele.

53 Wewe ni mukubwa kuliko babu yetu Abrahamu? Yeye alikufa, na manabii walikufa vilevile. Wewe unajiona kuwa nani?”

54 Yesu akajibu: “Kama nikijitafutia sifa yangu mwenyewe, sifa ile haina maana. Baba yangu ndiye anayenisifu, yule munayejidai kwamba ni Mungu wenu!

55 Ninyi hamumujui, lakini mimi ninamujua. Kama ningesema kwamba simujui, ningekuwa mwongo kama ninyi. Lakini ninamujua na ninashika neno lake.

56 Baba yenu Abrahamu alishangilia akitumainia kuona siku ya kuja kwangu; na wakati alipoiona, alifurahi.”

57 Halafu Wayuda wakamwambia: “Wewe haujaeneza umri wa miaka makumi tano, nawe umemwona Abrahamu?”

58 Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: mbele Abrahamu hajazaliwa, mimi nilikuwa niko.”

59 Kwa ajili ya hii, wakaokota mawe kwa kumutupia. Lakini Yesu akajificha na kutoka ndani ya hekalu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan