Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoane 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kutokuamini kwa wandugu za Yesu

1 Kisha mambo hayo, Yesu akatembea katika Galilaya. Hakutaka kutembea katika Yudea, kwa sababu Wayuda walitaka kumwua.

2 Sikukuu moja ya Wayuda inayoitwa Sikukuu ya Vibanda ilipokuwa karibu,

3 wandugu za Yesu wakamwambia: “Ondoka hapa, uende Yudea kusudi wanafunzi wako waone matendo unayofanya.

4 Hakuna mutu anayefanya kitu kwa uficho, ikiwa anataka kujulikana waziwazi. Basi kwa kuwa unafanya matendo kama hayo, ujionyeshe mbele ya watu wote.”

5 (Hata wandugu zake vilevile hawakumwamini.)

6 Na Yesu akawaambia: “Wakati unaofaa kwangu haujatimia; lakini wakati wowote unafaa kwenu.

7 Watu wa dunia hawawezi kuwachukia ninyi, lakini wananichukia mimi kwa sababu ninashuhudia kwamba matendo yao ni mabaya.

8 Ninyi muende kwa sikukuu. Mimi sijaenda bado kwa sikukuu hii, kwa sababu wakati unaofaa kwangu haujatimia.”

9 Alipokwisha kuwaambia maneno hayo, akabaki Galilaya.


Yesu anahuzuria katika sikukuu ya Vibanda

10 Wandugu zake walipokwisha kwenda kwa sikukuu ile, Yesu akaenda kule vilevile, lakini alienda kwa siri bila kujionyesha waziwazi.

11 Wayuda walikuwa wakimutafuta kwenye sikukuu ile na kuuliza kwamba yeye yuko wapi.

12 Katika kundi lile kulikuwa manunguniko mengi juu yake. Wamoja walisema: “Yeye ni mutu muzuri.” Wengine walisema: “Hapana, si vile, yeye anawadanganya watu.”

13 Lakini hakuna mutu aliyesema juu yake waziwazi, kwa sababu waliwaogopa wakubwa wa Wayuda.

14 Halafu katikati ya sikukuu, Yesu akaingia ndani ya hekalu na kuanza kufundisha.

15 Wayuda wakashangaa, wakisema: “Mutu huyu amepata elimu kama hii namna gani, naye hakufundishwa?”

16 Yesu akawajibu: “Mafundisho ninayotoa si yangu, lakini ni ya yule aliyenituma.

17 Kama mutu akitaka kufanya mapenzi ya Mungu, atajua kama mafundisho yangu yanatoka kwa Mungu, au kama ninasema kwa mamlaka yangu mwenyewe.

18 Mutu anayesema kwa mamlaka yake mwenyewe, anajitafutia sifa yake mwenyewe. Lakini yeye anayetafuta sifa ya yule aliyemutuma, huyu ni mwenye ukweli wala hana ubaya wowote.

19 Musa hakuwapa ninyi Sheria? Ingawa hivyo hakuna mumoja wenu anayetii Sheria. Na sasa sababu gani munatafuta kuniua?”

20 Watu wale wakajibu: “Wewe uko na pepo. Nani anatafuta kukuua?”

21 Yesu akawajibu: “Nilifanya jambo moja, nalo limewashangaza ninyi wote.

22 Ninyi munatahiri watu hata kwa siku ya Sabato kwa sababu Musa aliwatolea ninyi amri ya kutahiri, (kwa hakika haikutoka kwa Musa, lakini kwa babu zenu).

23 Basi, kama munaweza kutahiri mutu kwa siku ya Sabato, kusudi musivunje Sheria ya Musa, kwa nini munanikasirikia kwa sababu nimemuponyesha mutu kabisa kwa siku ya Sabato?

24 Muache kuhukumu kufuatana na hali ya inje, lakini muhukumu kwa haki.”


Yesu ni Kristo?

25 Halafu watu wamoja wa Yerusalema wakasema: “Huyu si mutu yule wanayetafuta kumwua?

26 Angalia, anasema waziwazi wala hawamwambii neno! Labda wakubwa nao wametambua kweli kuwa huyu ndiye Kristo.

27 Lakini tunajua pahali mutu huyu anapotoka. Kristo atakapokuja, hakuna mutu atakayejua pahali atakapotokea.”

28 Basi Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu akasema hivi kwa sauti: “Ndiyo, ninyi munajidai kwamba munanijua na munajua pahali ninapotoka. Sikukuja kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini aliyenituma ni mwenye ukweli. Ninyi hamumujui,

29 lakini mimi ninamujua sababu nilitoka kwake, naye ndiye aliyenituma.”

30 Basi wakatafuta kumufunga, lakini hakuna mutu aliyemukamata, kwa sababu saa yake ilikuwa haijatimia.

31 Watu wengi katika kundi lililokuwa pale wakamwamini, wakisema: “Kristo atakapokuja, ataonyesha vitambulisho zaidi kuliko mutu huyu?”


Walinzi wanatumwa kumukamata Yesu

32 Wafarisayo wakasikia maneno hayo watu waliyosemasema juu ya Yesu. Basi wakubwa wa makuhani na Wafarisayo wakatuma walinzi wao kumufunga.

33 Yesu akasema: “Ningali pamoja nanyi kwa wakati kidogo na kisha nitarudi kwa yule aliyenituma.

34 Mutanitafuta, lakini hamutaniona, kwa maana hamuwezi kufika pahali nitakapokuwa.”

35 Wayuda wakaulizana hivi wao kwa wao: “Mutu huyu atakwenda wapi sisi tusipoweza kumwona? Ataenda kwa Wayuda waliosambazwa kati ya Wagriki na kuwafundisha Wagriki?

36 Yeye anasema kwamba tutamutafuta, lakini hatutamwona, na kwamba hatuwezi kufika pahali atakapokwenda. Maana ya maneno haya ni gani?”


Mito ya maji ya uzima

37 Siku ya mwisho ya sikukuu ile iliyokuwa siku kubwa, Yesu akasimama na kusema hivi kwa sauti: “Mutu akiwa na kiu, akuje kwangu akunywe.

38 Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: ‘Mito ya maji ya uzima yatatiririka toka ndani ya yule anayeniamini.’ ”

39 (Alisema vile juu ya Roho atakayepokelewa na wale wanaomwamini Yesu. Kwa wakati ule Roho alikuwa hajatumwa bado, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.)


Kundi linakorogana juu ya Yesu

40 Watu wamoja katika kundi lile waliposikia maneno hayo, wakasema: “Hakika mutu huyu ndiye Nabii aliyepaswa kuja!”

41 Wengine wakasema: “Huyu ni Kristo.” Lakini wengine wakasema: “Basi Kristo angeweza kutokea Galilaya?

42 Maandiko Matakatifu hayakusema kwamba Kristo atazaliwa katika ukoo wa mufalme Daudi na katika muji Betelehemu, pahali Daudi alipoishi?”

43 Basi kukatokea mikorogano katika kundi juu ya Yesu.

44 Wengine katikati yao walitaka kumufunga, lakini hakuna mutu aliyemukamata.


Kutokuamini kwa wakubwa wa Wayuda

45 Kisha wale walinzi wakarudi kwa wakubwa wa makuhani na Wafarisayo. Nao wakawauliza walinzi: “Sababu gani hamukuleta Yesu?”

46 Walinzi wakajibu: “Hatujasikia mutu akisema sawasawa na mutu yule!”

47 Basi Wafarisayo wakawauliza: “Na ninyi vilevile mumedanganywa?

48 Ni nani kati ya wakubwa wetu au kati ya Wafarisayo aliyemwamini?

49 Lakini watu hawa wasiojua Sheria ya Musa wamelaaniwa.”

50 Nikodemo, yule aliyekuwa amemwendea Yesu mbele, alikuwa mumoja wa Wafarisayo waliokuwa pale. Akawaambia:

51 “Kufuatana na Sheria, hatuwezi kumuhukumu mutu mbele ya kumusikiliza na kujua yale aliyofanya.”

52 Wakamujibu: “Na wewe vilevile umetoka Galilaya? Uchunguze Maandiko Matakatifu, nawe utaona kwamba Galilaya hakutoki nabii.” [

53 Kisha kila mumoja akarudi kwake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan