Yoane 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anakulisha watu elfu tano ( Mat 14.13-21 ; Mk 6.30-44 ; Lk 9.10-17 ) 1 Nyuma ya maneno hayo, Yesu akavuka ziwa la Galilaya (linaloitwa vilevile Tiberia). 2 Kundi kubwa la watu wakamufuata, kwa sababu watu hao waliona vitambulisho alivyoonyesha kwa kuponyesha wagonjwa. 3 Yesu akapanda kwenye kilima, na kuikaa kule pamoja na wanafunzi wake. 4 Na Pasaka, ambayo ni moja ya sikukuu za Wayuda, ilikuwa karibu. 5 Wakati Yesu alipoinua macho, akaona kundi kubwa la watu wakimufikia. Halafu akamwuliza Filipo: “Wapi tunaweza kununua vyakula kwa kulisha watu hawa?” 6 (Alisema vile kusudi amupime Filipo, kwa sababu yeye mwenyewe alijua atakavyofanya.) 7 Filipo akamujibu: “Hata tukinunua mikate kwa bei ya vikoroti mia mbili vya feza, haitatosha kwa kumupa kila mutu hata kidogo tu.” 8 Mwanafunzi wake mwingine mumoja anayeitwa Andrea, ndugu ya Simoni Petro, akamwambia: 9 “Hapa kuna mutoto mumoja anayekuwa na mikate mitano ya shayiri pamoja na samaki mbili. Lakini chakula hiki hakitawafalia kitu watu wengi kama hawa.” 10 Yesu akasema: “Muwaambie watu waikae chini.” (Pale kulikuwa majani mengi.) Basi wakaikaa chini; na hesabu ya wanaume tu ilikuwa yapata elfu tano. 11 Kisha Yesu akatwaa ile mikate, akamushukuru Mungu na kuigawanya kwa watu walioikaa pale. Akawapa samaki vilevile kwa kadiri walivyotaka. 12 Walipokwisha kushiba, Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Mukusanye vipande vinavyobaki, kusudi kusipotee kitu.” 13 Basi wakavikusanya, wakajaza vitunga kumi na viwili na vipande vilivyobaki vya ile mikate mitano ya shayiri waliyokula. 14 Watu walipoona kile kitambulisho Yesu alichoonyesha, wakasema: “Hakika mutu huyu ndiye yule nabii aliyepaswa kuja katika dunia!” 15 Wakati Yesu alipotambua kama walitaka kuja kumutwaa kwa nguvu na kumuweka kuwa mufalme, akaondoka na kwenda tena kwa kilima peke yake. Yesu anatembea juu ya maji ( Mat 14.22-33 ; Mk 6.45-52 ) 16 Ilipokuwa magaribi, wanafunzi wake wakashuka kwenda kwenye ziwa. 17 Wakaingia ndani ya chombo, wakaanza kuvuka ziwa kwa kwenda Kapernaumu. Giza lilikuwa limekwisha kuwa, na Yesu alikuwa hajarudi kukutanana nao. 18 Ziwa likaanza kuchafuka sana; kwa sababu upepo ulikuwa ukivuma kwa nguvu. 19 Walipofika umbali wa kadiri ya kilometre tano au sita, wakamwona Yesu anakaribia chombo, akitembea juu ya maji; kwa hiyo wakaogopa. 20 Lakini Yesu akawaambia: “Ni mimi, musiogope!” 21 Wao walitaka kumupandisha ndani ya chombo lakini mara moja chombo kikafikia inchi kavu, pahali walipokuwa wakienda. Watu wanamutafuta Yesu 22 Kesho yake watu waliobaki kule ngambo ya ziwa wakatambua kwamba kulikuwa tu chombo kimoja pale. Walijua vilevile kwamba Yesu hakuingia ndani ya chombo pamoja na wanafunzi wake, lakini wanafunzi wake walikwenda peke yao. 23 Na vilevile vyombo vingine vilivyotoka katika muji Tiberia vilifika karibu na pahali pale walipokula mikate, Bwana alipokuwa amekwisha kushukuru Mungu. 24 Wakati walipoona kama Yesu hakukuwa pale wala wanafunzi wake, wakajiingilia ndani ya vyombo vile na kwenda Kapernaumu kumutafuta Yesu. Yesu ni mukate wa uzima 25 Watu wale wakamukuta Yesu kule ngambo ya ziwa na kumwuliza: “Mwalimu, ulifika hapa wakati gani?” 26 Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: hamunitafuti kwa sababu muliona vitambulisho nilivyoonyesha, lakini kwa sababu mulikula mikate na kushiba. 27 Musitumikie chakula kinachoharibika, lakini mutumikie chakula kinachodumu na kuleta uzima wa milele. Mwana wa Mutu atawapa ninyi chakula hiki, kwa sababu Mungu Baba ametoa uhakikisho juu yake.” 28 Basi wakamwuliza: “Tufanye nini kusudi tupate kutumika kazi ya Mungu?” 29 Yesu akawajibu: “Hii ndiyo kazi ya Mungu: mumwamini yule aliyemutuma.” 30 Wakamwuliza: “Basi utatuonyesha kitambulisho gani kusudi tupate kukiona na kukuamini? Utafanya jambo gani? 31 Babu zetu walikula mana katika jangwa, kama ilivyoandikwa katika Maandiko Matakatifu yanayosema: ‘Aliwakulisha kwa mukate uliotoka mbinguni.’ ” 32 Yesu akawajibu: “Kweli, kweli ninawaambia: Musa hakuwapa ninyi mukate wa mbinguni, lakini ni Baba yangu anayewapa ninyi mukate wa kweli wa mbinguni. 33 Maana mukate Mungu anaoupana ni yule anayeshuka toka mbinguni na kuleta uzima katika dunia.” 34 Basi wakamwambia: “Bwana, utupatie mukate ule siku zote.” 35 Yesu akawaambia: “Mimi ni mukate wa uzima. Anayenikubali hatasikia njaa hata kidogo, na yule anayeniamini hatasikia kiu hata kidogo. 36 Lakini kama nilivyowaambia: mumeniona, lakini ijapokuwa vile hamuamini. 37 Wote Baba anaonipa wanakuja kwangu; nami sitamukataa hata kidogo yule anayekuja kwangu. 38 Kwa sababu nimeshuka toka mbinguni kusudi nifanye mapenzi ya yule aliyenituma, wala si mapenzi yangu. 39 Na mapenzi ya yule aliyenituma ni kwamba nisipoteze hata mumoja wa wale alionipa, lakini nimufufue siku ya mwisho wa dunia. 40 Hakika mapenzi ya Baba yangu ni kwamba kila mutu anayemwona Mwana na kumwamini apate uzima wa milele, nami nitamufufua siku ya mwisho.” 41 Basi Wayuda wakaanza kunungunika kwa sababu Yesu alisema kwamba yeye ni mukate ulioshuka toka mbinguni. 42 Nao wakasema: “Huyu si Yesu mwana wa Yosefu? Si tunawajua baba yake na mama yake? Namna gani anaweza kusema sasa kwamba alishuka toka mbinguni?” 43 Yesu akawajibu: “Musikuwe na manunguniko kati yenu. 44 Hakuna mutu anayeweza kuja kwangu, isipokuwa anavutwa na Baba aliyenituma, nami nitamufufua siku ya mwisho. 45 Imeandikwa hivi katika maandiko ya manabii: ‘Wote watafundishwa na Mungu.’ Kila mutu anayemusikia Baba na kufuata mafundisho yake, anakuja kwangu. 46 Si kusema kwamba kuna mutu yeyote aliyemwona Baba isipokuwa yule aliyetoka kwa Mungu; yeye ndiye aliyemwona Baba. 47 Kweli, kweli ninawaambia: anayeamini anapata uzima wa milele. 48 Mimi ni mukate wa uzima. 49 Babu zenu walikula mana katika jangwa, lakini wakakufa. 50 Lakini ule ni mukate ulioshuka toka mbinguni, anayeukula hatakufa. 51 Mimi ni ule mukate wa uzima, ulioshuka toka mbinguni. Kama mutu akikula mukate huu ataishi milele. Na mukate nitakaotoa ni mwili wangu, utakaotolewa kusudi dunia ipate uzima.” 52 Basi Wayuda wakaanza kubishana sana kati yao, wakasema: “Namna gani mutu huyu anaweza kutupatia mwili wake tuukule?” 53 Kwa hiyo Yesu akawaambia: “Kweli, kweli, ninawaambia: musipokula mwili wa Mwana wa Mutu na kunywa damu yake, hamutakuwa na uzima ndani yenu. 54 Anayekula mwili wangu na kunywa damu yangu anapata uzima wa milele, nami nitamufufua siku ya mwisho. 55 Mwili wangu ni chakula cha kweli na damu yangu ni kinywaji cha kweli. 56 Anayekula mwili wangu na kunywa damu yangu anakaa ndani yangu, nami ninakaa ndani yake. 57 Kama vile Baba aliyenituma anavyokuwa muzima, nami ninaishi kwa nguvu zake, vilevile anayenikula ataishi kwa nguvu zangu. 58 Huu ndio mukate ulioshuka toka mbinguni, nao si kama mukate ule babu zenu waliokula katika jangwa na kufa. Anayekula mukate huu ataishi milele.” 59 Yesu alisema maneno haya wakati alipokuwa akifundisha katika nyumba ya kuabudia kule Kapernaumu. 60 Wengi kati ya wanafunzi wake waliposikia maneno haya, wakasema: “Masemi haya ni magumu. Ni nani anayeweza kuyakubali?” 61 Yesu akafahamu kwamba wanafunzi wake wananungunika juu ya neno hili; basi akawauliza: “Neno hili linawakwaza? 62 Basi itakuwa namna gani kama mukimwona Mwana wa Mutu akipanda tena pahali alipokuwa mbele? 63 Roho ndiye anayeleta uzima; mwili hauwezi kufaa kitu. Maneno haya niliyosema nanyi, ndiyo Roho na uzima. 64 Lakini kuna wengine kati yenu wasioamini.” (Yesu alisema vile kwa sababu alijua tangu mwanzo wale wasioamini na yule atakayemutoa.) 65 Yesu akaongeza kusema: “Kwa sababu hii niliwaambia kama hakuna mutu anayeweza kuja kwangu, isipokuwa anawezeshwa na Baba.” 66 Basi kwa sababu ya maneno haya, wengi kati ya wanafunzi wake wakamwacha, nao hawakutembea tena pamoja naye. 67 Kwa hiyo Yesu akawauliza wale wanafunzi kumi na wawili: “Nanyi munataka kwenda vilevile?” 68 Simoni Petro akamujibu: “Bwana, tutakwenda kwa nani? Wewe unasema maneno ya uzima wa milele. 69 Na sasa tunaamini na kujua kwamba wewe ni Mutakatifu wa Mungu.” 70 Yesu akawajibu: “Ni mimi peke niliyewachagua ninyi kumi na wawili, lakini ingawa hivi mumoja wenu ni Shetani!” 71 (Alisema hivi juu ya Yuda mwana wa Simoni Iskariota, kwa maana yeye ndiye atakayemutoa, ijapokuwa alikuwa mumoja wa wale kumi na wawili.) |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo