Yoane 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu anaponyesha mugonjwa wa Betesaida 1 Nyuma ya maneno hayo, Yesu akaenda Yerusalema kwa sikukuu ya Wayuda. 2 Kule Yerusalema, karibu na mulango wa muji huu unaoitwa “Mulango wa Kondoo,” kuna kisima chenye viingilio vitano vyenye paa. Kisima kile kinaitwa katika Kiebrania “Betesaida.” 3 Wagonjwa wengi walikuwa wakilala katika viingilio vile; kulikuwa vipofu, vilema na wenye kupooza. [Walikuwa wakingoja maji yatikiswe, 4 kwa sababu malaika wa Bwana alishuka mara kwa mara ndani ya kile kisima na kutikisa maji. Na mugonjwa wa kwanza aliyeingia ndani ya maji kisha kuyatikisa, alipona ugonjwa wowote aliokuwa nao.] 5 Pale kulikuwa mutu mumoja aliyekuwa mugonjwa tangia miaka makumi tatu na minane. 6 Wakati Yesu alipomwona akilala na kutambua kwamba amekuwa mugonjwa kwa muda wa siku nyingi, akamwuliza: “Unataka kupona?” 7 Yule mugonjwa akamujibu: “Bwana, sina mutu wa kuniingiza katika kisima wakati maji yanapotikiswa, nami ninapojaribu kuingia ndani ya maji, mutu mwingine anaingia mbele yangu.” 8 Yesu akamwambia: “Simama, utwae kipoyi chako na uende.” 9 Mara moja mutu yule akapona, akatwaa kipoyi chake na kuanza kutembea. Siku ile ilikuwa siku ya Sabato, 10 kwa hiyo Wayuda wakamwambia mutu yule aliyeponyeshwa: “Leo ni siku ya Sabato, na Sheria haikuruhusu kubeba kipoyi chako.” 11 Akawajibu: “Yule aliyeniponyesha ndiye aliyeniambia: ‘Twaa kipoyi chako na uende.’ ” 12 Basi wakamwuliza kwamba ni nani aliyemwambia kwamba atwae kipoyi wake na aende. 13 Lakini mutu yule aliyeponyeshwa hakujua ni nani, kwa maana Yesu alikuwa amekwisha kuondoka katikati ya kundi kubwa la watu waliokuwa pale. 14 Kisha Yesu akamukuta mutu yule ndani ya hekalu, akamwambia: “Angalia, sasa umepona. Basi usifanye zambi tena, kusudi jambo baya zaidi lisikufikie.” 15 Yule mutu akaenda kuwaambia Wayuda kwamba Yesu ndiye aliyemuponyesha. 16 Kwa sababu ile Wayuda wakaanza kumufuatilia Yesu kwa kuwa alifanya mambo haya kwa siku ya Sabato. 17 Lakini Yesu akawajibu: “Baba yangu anatumika wakati wote, nami ninatumika vilevile.” 18 Kwa ajili ya neno hili Wayuda walitaka tena zaidi kumwua; si kwa sababu ya kuvunja Sheria ya siku ya Sabato tu, lakini vilevile kwa sababu alisema kwamba Mungu ni Baba yake, akijifanya hivi kuwa sawasawa na Mungu. Mamlaka ya Mwana wa Mungu 19 Basi Yesu akaongeza kuwaambia Wayuda: “Kweli, kweli, ninawaambia: Mwana hawezi kufanya kitu kwa mafikiri yake mwenyewe; anafanya tu kile ambacho anaona Baba akifanya. Na mambo yote Baba anayofanya, Mwana anayafanya vilevile. 20 Kwa maana Baba anamupenda Mwana, anamwonyesha yote anayofanya yeye mwenyewe. Atamwonyesha mambo makubwa zaidi kuliko haya kusudi mupate kushangaa. 21 Kwa maana kama vile Baba anavyofufua wafu na kuwarudishia uzima, vile vile Mwana anawapa uzima wale anaowataka. 22 Na zaidi ya hii Baba hahukumu hata mutu mumoja, lakini amemupa Mwana uwezo wote wa kuhukumu, 23 kusudi watu wote wamuheshimu Mwana kama vile wanavyomuheshimu Baba. Asiyemuheshimu Mwana, hamuheshimu Baba aliyemutuma. 24 “Kweli, kweli ninawaambia: anayesikia neno langu na kumwamini yule aliyenituma, anapata uzima wa milele. Yeye hatahukumiwa, lakini ameponyoka lufu na kupata uzima. 25 Kweli, kweli ninawaambia: kutakuwa wakati, nao umekwisha kutimia, wafu watakaposikia sauti ya Mwana wa Mungu, na wale wanaoisikia, wataishi. 26 Kama vile Baba ana uwezo wa kupana uzima, ndivyo vilevile amemupa Mwana uwezo wa kupana uzima. 27 Vilevile amemupa Mwana mamlaka ya kuhukumu, kwa sababu yeye ni Mwana wa Mutu. 28 Musishangae kwa ajili ya maneno haya, kwa sababu kutakuwa wakati wafu wote wanaokuwa ndani ya makaburi watakaposikia sauti yake 29 na kutoka ndani ya makaburi yao. Waliotenda mema watafufuka na kupata uzima, lakini waliotenda mabaya watafufuka na kuhukumiwa. Washuhuda wa mamlaka ya Yesu 30 “Siwezi kufanya kitu kwa mafikiri yangu mwenyewe. Ninahukumu tu kama vile Mungu anavyoniambia na hukumu yangu ni ya haki, kwa sababu sitafuti kufanya mapenzi yangu, lakini mapenzi ya yule aliyenituma. 31 Kama nikijishuhudia mimi mwenyewe, ushuhuda wangu hauwezi kukubaliwa kuwa wa kweli. 32 Lakini kuna mwingine anayenishuhudia, nami ninajua kwamba ushuhuda anaoutoa juu yangu ni wa kweli. 33 Ninyi mulituma wajumbe kwa Yoane, naye alishuhudia ukweli. 34 Kweli mimi sihitaji kushuhudiwa na mutu, lakini ninasema maneno haya kusudi mupate kuokolewa. 35 Yoane alikuwa kama taa inayowaka na kuangaza, na ninyi mulipendezwa kufurahishwa na mwangaza wake kwa muda. 36 Lakini mimi nina ushuhuda mukubwa zaidi kuliko ule uliotolewa na Yoane. Maana sasa mambo ninayofanya ndiyo Baba aliyoniamuru kutimiza, nayo yananishuhudia na kuonyesha kwamba yeye amenituma. 37 Na Baba aliyenituma amenishuhudia vilevile. Ninyi hamujasikia sauti yake wakati wowote wala hamujaona sura yake. 38 Ninyi hamuchungi neno lake ndani yenu, kwa sababu ninyi hamumwamini yule aliyetumwa naye. 39 Munachunguza Maandiko Matakatifu, kwa maana munazani kuwa ndani yao mutapata uzima wa milele. Maandiko hayo ndiyo yanayonishuhudia, 40 lakini ninyi hamutaki kuja kwangu mupate uzima. 41 “Mimi sipokei sifa kutoka kwa watu. 42 Lakini ninawajua ninyi kwamba hamumupendi Mungu. 43 Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu, nanyi hamutaki kunipokea. Lakini ikiwa mwingine anakuja kwa jina lake mwenyewe, ninyi mutamupokea. 44 Basi namna gani mutaweza kuamini, ninyi munaopokea sifa kutoka wamoja kwa wengine, lakini hamutafuti sifa inayotoka kwake anayekuwa Mungu peke yake? 45 Musizanie kwamba mimi nitawashitaki kwa Baba. Atakayewashitaki ninyi ni Musa, ambaye mulimutumainia. 46 Kama mungemusadiki Musa, mungenisadiki mimi vilevile, kwa sababu yeye aliandika habari juu yangu. 47 Lakini ikiwa hamusadiki yale Musa aliyoandika, namna gani mutasadiki maneno ninayosema?” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo