Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoane 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu na mwanamuke Musamaria

1 Yesu akatambua kwamba Wafarisayo wamepata habari kama yeye anapata wanafunzi wengi zaidi kuliko Yoane na kuwabatiza.

2 (Hakika Yesu mwenyewe hakubatiza mutu lakini ni wanafunzi wake.)

3 Basi, Yesu akaondoka Yudea na kurudi Galilaya.

4 Kwa kufika kule ilimupasa apite katika Samaria.

5 Akafika karibu na muji mumoja wa Samaria unaoitwa Sikari, uliokuwa karibu na shamba lile Yakobo alilomupa mwana wake Yosefu.

6 Pale kulikuwa kisima kilichokuwa cha Yakobo. Yesu akaikaa kwa ukingo wa kisima, kwa sababu alikuwa amechoka na safari. Ilikuwa karibu na saa sita za muchana.

7 Halafu mwanamuke mumoja Musamaria akakuja kuteka maji. Na Yesu akamwambia: “Unipe maji ya kunywa.”

8 (Wakati ule wanafunzi wake walikuwa wamekwenda katika muji kununua vyakula.)

9 Basi yule mwanamuke Musamaria akamwambia Yesu: “Namna gani wewe Muyuda unaweza kuniomba mimi Musamaria maji ya kunywa?” (Wayuda hawakukuwa na ushirika na Wasamaria.)

10 Yesu akamujibu: “Kama ungejua kitu Mungu anachoweza kukupatia, na ni nani anayekuomba maji ya kunywa, wewe ndiwe ungemwomba, naye angekupa maji ya uzima.”

11 Yule mwanamuke akamwambia: “Bwana, hauna chombo cha kutekea, na kisima ni kirefu sana. Basi umepata wapi maji ya uzima?

12 Babu yetu Yakobo ndiye aliyetupa sisi kisima hiki, hata yeye mwenyewe pamoja na wana wake na nyama wake walikunywa maji yake. Wewe unajiona kuwa mukubwa kuliko Yakobo?”

13 Yesu akamujibu: “Kila mutu anayekunywa maji haya atasikia kiu tena;

14 lakini yeyote atakayekunywa maji yale nitakayomupa, hatasikia kiu tena hata kidogo. Maji nitakayomupa yatakuwa ndani yake kama chemichemi inayotiririka maji ya uzima wa milele.”

15 Mwanamuke yule akamwambia: “Bwana, unipe basi maji yale, kusudi nisisikie kiu tena. Hivi sitahitaji kuja tena hapa kuteka maji.”

16 Yesu akamwambia: “Uende kumwita mume wako na urudi naye hapa.”

17 Yule mwanamuke akamujibu: “Sina mume.” Na Yesu akamwambia: “Unasema kweli kwamba hauna mume;

18 kwa maana ulikuwa na wanaume watano, na yule unayeishi naye sasa si mume wako. Hivi unasema ukweli.”

19 Halafu mwanamuke yule akamwambia: “Bwana, ninaona kama wewe ni nabii.

20 Babu zetu walimwabudu Mungu juu ya mulima huu, lakini ninyi Wayuda munasema kama Yerusalema ni pahali pa kumwabudia Mungu.”

21 Yesu akamwambia: “Ee mama, unisadiki; kutakuwa wakati hamutamwabudu Baba juu ya mulima huu wala Yerusalema.

22 Ninyi Wasamaria hamujui munachokiabudu; sisi tunajua tunachokiabudu kwa sababu wokovu unatokea kwa njia ya Wayuda.

23 Lakini kutakuwa wakati, nao umekwisha kutimia, wale wanaoabudu kwa kweli watakapomwabudu Baba katika roho na ukweli; kwa maana Baba anataka watu wanaoabudu kwa namna ile.

24 Mungu ni roho, nao wanaomwabudu wanapaswa kumwabudu katika roho na ukweli.”

25 Mwanamuke yule akamwambia: “Ninajua kwamba Masiya anayeitwa Kristo, atakuja. Na wakati atakapokuja atatuelezea maneno yote.”

26 Yesu akamujibu: “Mimi ninayesema nawe, ndiye.”

27 Saa ile ile wanafunzi wa Yesu wakarudi, nao wakashangaa kumwona akisemezana na mwanamuke. Lakini hakuna mumoja wao aliyemwuliza yule mwanamuke kwamba anataka nini au kumwuliza Yesu kwamba sababu gani anasema naye.

28 Basi mwanamuke yule akaacha mutungi wake wa maji pale, akarudi katika muji na kuwaambia watu:

29 “Mukuje mumwone mutu aliyeniambia maneno yote niliyotenda. Huyu si Kristo?”

30 Basi wakatoka katika muji na kumwendea Yesu.

31 Wakati ule wanafunzi wa Yesu walimusihi, wakisema: “Mwalimu, kula chakula.”

32 Lakini akawajibu: “Mimi nina chakula musichokijua.”

33 Basi wanafunzi wakaanza kuulizana: “Kuna mutu aliyemuletea chakula?”

34 Yesu akawaambia: “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma na kutimiza kazi yake.

35 Si ninyi munazoea kusema: ‘Kunabaki miezi mine kuwe mavuno’? Lakini mimi ninawaambia, muinue macho, muangalie mashamba; mimea imekomaa, nayo ni tayari kwa kuvunwa.

36 Muvunaji anakwisha kupokea mushahara, naye anakusanya mavuno kwa ajili ya uzima wa milele, kusudi mupandaji na muvunaji wafurahi pamoja.

37 Kwa maana neno hili ni kweli: ‘Mutu mumoja anapanda na mwingine anavuna.’

38 Mimi niliwatuma ninyi katika shamba kuvuna mavuno ambayo hamukusumbukia; wengine waliyasumbukia, nanyi mumepata faida ya kazi yao.”

39 Wasamaria wengi wa muji ule walimwamini Yesu kwa sababu ya maneno ya yule mwanamuke aliposhuhudia hivi: “Aliniambia mambo yote niliyotenda.”

40 Na Wasamaria walipomufikia Yesu, walimusihi akae pamoja nao, naye akakaa kule muda wa siku mbili.

41 Wengine wengi zaidi waliamini kwa sababu ya maneno yake mwenyewe,

42 nao wakamwambia yule mwanamuke: “Sasa tunaamini, si kwa sababu ya maneno uliyotuambia tu, lakini kwa sababu tumesikia sisi wenyewe na tunajua hakika kwamba huyu ni Mwokozi wa dunia.”


Yesu anamuponyesha mwana wa mukubwa mumoja

43 Siku mbili zilipopita, Yesu akaondoka kule, akaenda Galilaya.

44 Yesu mwenyewe alikuwa ameshuhudia kwamba nabii haheshimiwi katika inchi yake mwenyewe,

45 lakini alipofika Galilaya, wakaaji wa kule wakamupokea, kwa maana wao vilevile walikuwa Yerusalema kwa sikukuu ya Pasaka, nao waliona mambo yote aliyofanya kule.

46 Basi Yesu akarudi tena Galilaya katika muji Kana, pahali alipogeuza maji kuwa divai. Kule kulikuwa mukubwa mumoja wa serikali, aliyekuwa na mwana mugonjwa katika muji Kapernaumu.

47 Wakati aliposikia kwamba Yesu amefika Galilaya toka Yudea, mukubwa huyu akamwendea, akamusihi aende Kapernaumu kumuponyesha mwana wake, aliyekuwa karibu kufa.

48 Basi Yesu akamwambia: “Ninyi hamuwezi kuamini hata kidogo kama musipoona vitambulisho na maajabu.”

49 Yule mukubwa wa serikali akamujibu: “Bwana, ninakuomba ufike kwangu mbele mutoto wangu hajakufa.”

50 Yesu akamwambia: “Kwenda tu, mwana wako ni muzima.” Mutu yule akaamini neno Yesu alilosema, naye akaondoka.

51 Alipokuwa katika njia akirudi kwake, watumishi wake wakakuja kukutana naye na kumwambia kwamba mutoto wake ni muzima.

52 Halafu akawauliza saa gani mutoto alipoanza kujisikia vizuri. Nao wakamujibu: “Yeye alipona homa jana muchana saa saba.”

53 Basi baba yule akatambua kama ilikuwa ni saa ile ile Yesu alipomwambia kwamba mwana wake ni muzima. Basi yeye na jamaa yake yote wakamwamini Yesu.

54 Hiki ndicho kitambulisho cha pili Yesu alichoonyesha. Ilikuwa wakati aliporudi Galilaya akitoka Yudea.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan