Yoane 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu na Nikodemo 1 Kulikuwa mutu mumoja aliyeitwa Nikodemo, mukubwa wa Wayuda, aliyekuwa mumoja wa kundi la Wafarisayo. 2 Alimwendea Yesu usiku na kumwambia: “Mwalimu, tunajua kama Mungu amekutuma kufundisha, kwa maana hakuna mutu anayeweza kuonyesha vitambulisho hivi unavyoonyesha isipokuwa anaongozwa na Mungu.” 3 Yesu akamujibu: “Kweli, kweli ninakuambia: mutu hawezi kuingia katika Ufalme wa Mungu asipozaliwa mara ya pili.” 4 Nikodemo akamwuliza: “Namna gani mutu anaweza kuzaliwa akiwa muzee? Anaweza kurudi ndani ya tumbo la mama yake na kuzaliwa mara ya pili?” 5 Yesu akajibu: “Kweli, kweli ninakuambia: mutu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuingia katika Ufalme wa Mungu. 6 Kinachozaliwa na mutu ni cha kimwili, nacho kinachozaliwa na Roho ni cha kiroho. 7 Usishangae kwa sababu nimekuambia kwamba sherti ninyi muzaliwe mara ya pili. 8 Upepo unavuma pahali unapotaka, nawe unasikia sauti yake, lakini haujui pahali unapotoka wala unapokwenda. Na ni vile inavyokuwa kwa kila mutu anayezaliwa kwa Roho.” 9 Basi Nikodemo akamwuliza: “Maneno haya yanawezekana namna gani?” 10 Yesu akamujibu: “Wewe unayekuwa mwalimu mukubwa katika inchi ya Israeli, haujui maneno haya? 11 Kweli, kweli ninakuambia: tunasema maneno tunayojua na kushuhudia maneno tuliyoona, lakini ninyi hamutaki kupokea ushuhuda wetu. 12 Ikiwa hamwamini wakati ninapowaambia maneno ya dunia, namna gani mutaamini kama nikiwaambia maneno ya mbinguni? 13 Na zaidi ya hii hakuna mutu aliyepanda mbinguni, isipokuwa Mwana wa Mutu aliyeshuka toka mbinguni. 14 Sawa Musa alivyonyanyua nyoka ya shaba juu ya muti katika jangwa, ni hivi vilevile, sherti Mwana wa Mutu anyanyuliwe, 15 kusudi kila mutu anayemwamini apate uzima wa milele. 16 Kwa maana Mungu alipenda sana ulimwengu hata kumutoa Mwana wake wa pekee, kusudi kila mutu anayemwamini asipotee, lakini apate uzima wa milele. 17 Mungu hakumutuma Mwana wake katika ulimwengu kusudi ahukumu ulimwengu, lakini kusudi ulimwengu uokolewe naye. 18 Anayemwamini Mwana hahukumiwi, lakini asiyemwamini amekwisha kuhukumiwa, kwa sababu hakumwamini Mwana wa pekee wa Mungu. 19 Hukumu inatokana na hivi: mwangaza umekuja katika ulimwengu, lakini watu wanapenda giza kuliko mwangaza, kwa sababu matendo yao ni mabaya. 20 Kila mutu anayefanya mabaya anachukia mwangaza, naye anakataa kuja kwenye mwangaza, kusudi matendo yake yasionekane wazi. 21 Lakini anayeshika ukweli, anakuja kwenye mwangaza, kusudi matendo yake yaonekane wazi kwamba yanatendeka sawa Mungu anavyoamuru.” Ushuhuda wa mwisho wa Yoane Mubatizaji 22 Kisha mambo hayo, Yesu na wanafunzi wake wakaenda Yudea. Akabaki kule pamoja nao na kubatiza. 23 Yoane vilevile alikuwa akibatiza kule Ainoni, karibu na Salimu, kwa sababu kule kulikuwa maji mengi. Watu walimwendea, naye akawabatiza. 24 (Wakati ule Yoane alikuwa hajawekwa katika kifungo.) 25 Kulitokea mabishano kati ya wanafunzi wa Yoane na Muyuda mumoja juu ya desturi zao za kujitakasa. 26 Basi wakamwendea Yoane na kumwambia: “Mwalimu, unakumbuka yule mutu aliyekuwa pamoja nawe ngambo ya Yordani, yule uliyemushuhudia? Angalia sasa, yeye anabatiza, na watu wote wanamufikia!” 27 Yoane akawajibu: “Hakuna mutu anayeweza kuwa na kitu isipokuwa amekipewa na Mungu. 28 Ninyi wenyewe ni washuhuda wangu kwamba nilisema: ‘Mimi si Kristo, lakini nimetumwa mbele yake.’ 29 Mwenye bibi arusi ndiye bwana-arusi; lakini rafiki ya bwana arusi anasimama karibu naye na kumusikiliza, anafurahi sana kusikia sauti ya bwana-arusi. Na ni hivi mimi ninafurahi, na furaha yangu imetimia sasa. 30 Sherti utukufu wake uzidi na wangu upunguke. 31 “Anayetoka juu ni juu ya yote; anayekuwa wa dunia ni wa dunia, naye anasema maneno ya dunia. Anayetoka mbinguni ni juu ya yote; 32 anashuhudia yale aliyoyaona na kuyasikia, lakini hakuna mutu anayekubali ushuhuda wake. 33 Yeyote anayekubali ushuhuda wake anahakikisha kama Mungu ni mwenye ukweli. 34 Aliyetumwa na Mungu anasema maneno ya Mungu, kwa sababu Mungu anamujaza Roho wake kwa uwingi. 35 Baba anamupenda Mwana wake, naye ameweka vitu vyote kwa mukono wake. 36 Anayemwamini Mwana yuko na uzima wa milele. Anayekataa kumwamini Mwana hatapata uzima; atakaa akipatwa na kasirani ya Mungu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo