Yoane 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu ni njia ya kwenda kwa Baba 1 Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Musifazaike; mumwamini Mungu, na muniamini mimi vilevile. 2 Ndani ya nyumba ya Baba yangu kuna nafasi nyingi za kukaa. Isingekuwa hivi singewaambia kwamba ninakwenda kuwatayarishia nafasi. 3 Nami nitakapokwisha kuwatayarishia ninyi nafasi, nitarudi tena na kuja kuwatwaa, kusudi pahali nitakapokuwa, ninyi mupate kuwa pale vilevile. 4 Munajua njia ya kufika pahali ninapokwenda.” 5 Toma akamwambia: “Bwana, hatujui pahali unapokwenda, basi namna gani tutajua njia?” 6 Yesu akamujibu: “Mimi ni njia, ukweli na uzima. Mutu hawezi kufika kwa Baba asipopitia kwangu. 7 Kama mungenijua mimi, mungemujua Baba yangu vilevile. Na tangu sasa mumemujua, na mumemwona.” 8 Filipo akamwambia: “Bwana, utuonyeshe Baba, na ile itatutoshelea.” 9 Yesu akajibu: “Filipo, nimekwisha kuwa nanyi siku nyingi sasa, nawe haujanijua bado? Aliyeniona mimi amemwona Baba. Basi sababu gani unasema: ‘Utuonyeshe Baba?’ 10 Hauamini kwamba mimi na baba ni mumoja, yeye ni ndani yangu na mimi ndani yake? Maneno ninayowaambia siyasemi kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini Baba anayekaa ndani yangu ndiye anayefanya kazi zake. 11 Muniamini wakati ninaposema kama mimi ni ndani ya Baba na Baba ni ndani yangu. Kama si vile, mwamini kwa sababu ya matendo niliyofanya. 12 Kweli, kweli ninawaambia: yeye anayeniamini atafanya vilevile matendo ninayofanya. Na zaidi ya ile atafanya matendo makubwa kuliko haya, kwa sababu ninakwenda kwa Baba. 13 Nami nitafanya chochote mutakachoomba kwa jina langu, kusudi Baba atukuzwe kwa njia ya Mwana. 14 Kama mukiomba kitu chochote kwa jina langu, nitakifanya. Ahadi ya kutuma Roho Mutakatifu 15 “Kama munanipenda, mutashika amri zangu. 16 Nami nitamwomba Baba awape musaidizi mwingine kwa kukaa nanyi milele; 17 naye ndiye Roho wa ukweli. Dunia haiwezi kumupokea, kwa sababu haimwoni wala haimujui. Lakini munamujua, kwa maana anaishi pamoja nanyi naye anakuwa ndani yenu. 18 “Sitawaacha kama wayatima, nitawarudilia tena. 19 Kunabaki wakati kidogo, dunia haitaniona tena, lakini ninyi mutaniona; na kwa sababu mimi ninaishi, ninyi mutaishi vilevile. 20 Na wakati ule mutafahamu kwamba mimi ni ndani ya Baba yangu, na ninyi ni ndani yangu, na mimi ndani yenu. 21 “Anayekubali amri zangu na kuzitii, ni yeye anayenipenda. Baba yangu atamupenda yule anayenipenda, na mimi nitamupenda vilevile na nitajitambulisha kwake.” 22 Yuda (si yule Yuda Iskariota) akamwuliza: “Bwana, namna gani utajitambulisha mwenyewe kwetu wala si kwa dunia?” 23 Yesu akamujibu: “Anayenipenda, atashika maneno yangu. Baba yangu atamupenda, naye Baba pamoja nami tutaingia ndani yake na kukaa ndani yake. 24 Asiyenipenda hashiki maneno yangu. Na neno munalosikia nikisema halitoki kwangu, lakini linatoka kwa Baba yangu aliyenituma. 25 “Nimewaambia maneno haya kwa maana ningali sasa pamoja nanyi. 26 Lakini Musaidizi, ndiye Roho Mutakatifu, yule Baba atakayemutuma kwa jina langu, atawafundisha maneno yote na kuwakumbusha yote niliyowaambia. 27 “Ninawaachia amani; ninawapa amani yangu. Siwapatii ninyi amani hii kama dunia inavyoitoa. Musifazaike wala musiogope. 28 Mumesikia jinsi nilivyowaambia kwamba ninajiendea, lakini nitawarudilia tena. Kama mungenipenda, mungefurahia kujua kwamba ninakwenda kwa Baba, kwa maana Baba ni mukubwa kuliko mimi. 29 Nimewaambia maneno haya sasa mbele hayajatokea, kusudi wakati yatakapotokea, mupate kuamini. 30 Sitasema nanyi maneno mengi tena, kwa sababu mutawala wa dunia hii anakuja. Yeye hana uwezo juu yangu, 31 lakini sherti dunia ijue kama ninamupenda Baba, nami ninafanya kama alivyoniagiza. “Musimame, tutoke hapa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo