Yoane 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yesu ananawisha miguu ya wanafunzi wake 1 Kulikuwa kumebaki siku moja mbele ya kutimia kwa sikukuu ya Pasaka. Yesu alijua kwamba saa yake ya kutoka katika dunia na kurudi kwa Baba yake imetimia. Yeye alikuwa akiwapenda watu wake waliokuwa katika dunia, na akaendelea kuwapenda mpaka mwisho. 2 Wakati Yesu na wanafunzi wake walipokuwa wakikula chakula cha magaribi, Shetani alikuwa amekwisha kumushawishi Yuda mwana wa Simoni Iskariota kwamba amutoe Yesu. 3 Yesu alijua kwamba Baba yake ameweka vitu vyote chini ya mamlaka yake, na kwamba yeye mwenyewe alitoka kwa Mungu na anarudi kwa Mungu. 4 Basi Yesu akaondoka kwenye chakula, akavua kanzu yake, akajifunga kitambaa katika kiuno. 5 Kisha akatia maji ndani ya bakuli, na kuanza kunawisha miguu ya wanafunzi wake na kuipanguza na kile kitambaa alichokifunga katika kiuno. 6 Alipofika kwenye Simoni Petro, Petro akamwambia: “Bwana, ni kweli wewe utaninawisha miguu?” 7 Yesu akamujibu: “Sasa hauelewi jambo ninalofanya, lakini utalielewa nyuma.” 8 Petro akamwambia: “Hautanawisha miguu yangu hata kidogo!” Yesu akamujibu: “Nisipokunawisha miguu, hauna ushirika pamoja nami.” 9 Simoni Petro akamwambia tena: “Basi Bwana, ikiwa ni vile usininawishe miguu tu, lakini uninawishe mikono na kichwa vilevile.” 10 Yesu akamwambia: “Aliyekwisha kuoga hahitaji kunawa tena, isipokuwa miguu yake tu, kwa maana mwili wake wote ni safi. Na ninyi ni safi, lakini si wote.” 11 (Yesu alijua yule atakayemutoa; ndiyo maana alisema: “Ninyi wote si safi.”) 12 Yesu alipokwisha kuwanawisha miguu, akavaa tena kanzu yake na kurudi kukaa kwenye chakula. Naye akawauliza: “Munaelewa jambo nililowafanyia? 13 Munaniita ‘Mwalimu’ na ‘Bwana,’ na munasema kweli, maana ni vile ninavyokuwa. 14 Basi kama mimi ninayekuwa Bwana na Mwalimu wenu nimewanawisha miguu, ninyi vilevile munapaswa kunawishana miguu. 15 Mimi nimewapa ninyi mufano, mufanye sawasawa nilivyowafanyia. 16 Kweli, kweli ninawaambia: mutumishi si mukubwa kuliko bwana wake, wala mujumbe si mukubwa kuliko yule aliyemutuma. 17 Sasa kwa kuona munajua jambo hili, mutakuwa wenye heri kama mukilifanya. 18 “Sisemi juu ya ninyi wote; ninawajua wale niliowachagua. Lakini inafaa maneno haya yanayosemwa na Maandiko Matakatifu yatimie: ‘Yule aliyechangia chakula nami, amenigeuka.’ 19 Ninawaambia ninyi sasa hayo yote mbele hayajatokea, kusudi wakati yatakapotokea, mwamini kwamba ‘Mimi Ndimi.’ 20 Kweli, kweli ninawaambia: mutu anayemupokea yule ninayemutuma, ananipokea mimi vilevile; na mutu anayenipokea, anamupokea yule aliyenituma.” 21 Yesu alipokwisha kusema maneno hayo, akafazaika na kusema: “Kweli, kweli ninawaambia, mumoja wenu atanitoa.” Yesu anatangaza kwamba Yuda atamutoa ( Mat 26.20-26 ; Mk 14.17-21 ; Lk 22.21-23 ) 22 Wanafunzi wakaangaliana, kwa maana hawakujua ni nani Yesu aliyemusema. 23 Na kulikuwa mumoja wa wanafunzi ambaye Yesu alimupenda, na aliyekuwa akimwegamia Yesu pale kwenye chakula. 24 Basi Simoni Petro akamukonyezea yule mwanafunzi jicho kusudi amwulize Yesu ni nani anayemusema. 25 Halafu yule mwanafunzi akamwegamia Yesu na kumwuliza: “Bwana, ni nani?” 26 Yesu akajibu: “Nitachovya kipande cha mukate. Yule nitakayemupa kipande kile ndiye yeye.” Basi Yesu akachovya kipande cha mukate na kumupa Yuda mwana wa Simoni Iskariota. 27 Yuda alipokwisha kukamata kile kipande cha mukate, Shetani akamwingilia. Basi Yesu akamwambia: “Unayotaka kufanya, uyafanye upesi!” 28 (Hakuna mutu kati ya wale waliokaa kwenye chakula aliyefahamu sababu gani Yesu alimwambia vile. 29 Wamoja walizani kama Yesu amemwambia aende kununua vitu walivyohitaji kwa sikukuu, au aende kuwasaidia wamasikini, kwa sababu Yuda ndiye aliyekuwa akichunga mufuko wa feza.) 30 Wakati Yuda alipokwisha kukamata kile kipande cha mukate, mara moja akatoka inje. Usiku ulikuwa umeingia. Amri mupya 31 Wakati Yuda alipokwisha kutoka, Yesu akasema: “Sasa Mwana wa Mutu ametukuzwa, na Mungu ametukuzwa kwa njia yake. 32 Na ikiwa Mungu ametukuzwa kwa njia yake, basi Mungu vilevile atamutukuza Mwana kwa njia yake mwenyewe, naye atamutukuza bila kukawia. 33 Watoto wangu, ningali pamoja nanyi kwa muda mufupi tu. Mutanitafuta, lakini sawasawa nilivyowaambia Wayuda, ninawaambia ninyi vilevile kwamba hamuwezi kufika pahali ninapokwenda. 34 Ninawapa amri mupya: mupendane ninyi kwa ninyi. Kama mimi nilivyowapenda, nanyi mupendane vilevile. 35 Watu wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, ikiwa munapendana ninyi kwa ninyi.” Yesu anajulisha kama Petro atamukana ( Mat 26.31-35 ; Mk 14.27-31 ; Lk 22.31-34 ) 36 Simoni Petro akamwuliza: “Bwana, unakwenda wapi?” Yesu akamujibu: “Hauwezi kunifuata sasa pahali ninapokwenda, lakini utanifuata nyuma.” 37 Petro akamwuliza: “Bwana, sababu gani siwezi kukufuata sasa? Mimi ni tayari kutoa maisha yangu kwa ajili yako!” 38 Yesu akamujibu: “Hakika wewe ni tayari kutoa maisha yako kwa ajili yangu? Kweli, kweli ninakuambia: mbele jogoo hajawika, utakuwa umekwisha kunikana mara tatu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo