Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoane 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yesu anapakaliwa marasi
( Mat 26.6-13 ; Mk 14.3-9 )

1 Siku sita mbele ya Pasaka, Yesu alifika Betania, kwao Lazaro, yule mutu Yesu aliyemufufua.

2 Kule wakamutayarishia chakula cha magaribi. Marta aliwashugulikia, na Lazaro alikuwa mumoja wa wale waliokula pamoja na Yesu.

3 Halafu Maria akatwaa nusu ya litre ya marasi ya bei kali, yaliyotengenezwa na maua ya nardo safi. Akaipakaa kwa miguu ya Yesu na kuipanguza na nywele zake. Nyumba yote ikajaa harufu ya marasi.

4 Lakini Yuda Iskariota, mumoja wa wanafunzi wa Yesu, yule atakayemutoa, akasema:

5 “Kwa sababu gani marasi hii ya bei kali haikuuzishwa kwa bei ya vikoroti mia tatu vya feza na kuwagawanyia wamasikini mali ile?”

6 (Hakusema maneno haya kwa sababu aliwasikilia wamasikini huruma, lakini kwa sababu alikuwa mwizi. Ni yeye aliyekuwa akichunga mufuko wa feza, naye alikuwa akijitwalia mali toka ndani yake.)

7 Lakini Yesu akasema: “Umwache kimya, kwa maana alikuwa ameweka marasi hii kwa ajili ya siku ya maziko yangu.

8 Mutakuwa na wamasikini pamoja nanyi siku zote, lakini hamutakuwa nami siku zote.”


Shauri la kumwua Lazaro

9 Kundi kubwa la Wayuda wakapata habari kwamba Yesu yuko Betania. Kwa hiyo wakaenda kule, si kwa sababu ya Yesu tu, lakini vilevile kwa kumwona Lazaro aliyefufuliwa naye.

10 Basi wakubwa wa makuhani wakakata shauri la kumwua Lazaro vilevile,

11 kwa maana kwa ajili yake Wayuda wengi walijitenga nao na kumwamini Yesu.


Yesu anaingia Yerusalema
( Mat 21.1-11 ; Mk 11.1-11 ; Lk 19.28-40 )

12 Kesho yake lile kundi kubwa la watu waliofika kwa sikukuu ya Pasaka wakasikia kwamba Yesu alikuwa katika njia kuja Yerusalema.

13 Basi wakatwaa matawi ya ngazi na kwenda kumupokea, wakilalamika kwa sauti kubwa, wakisema: “Mungu asifiwe! Abarikiwe huyu anayekuja kwa jina la Bwana! Abarikiwe mufalme wa Waisraeli!”

14 Yesu akapata mwana-punda na kupanda juu yake, kama vile inavyosemwa katika Maandiko haya Matakatifu:

15 “Musiogope ninyi wakaaji wa Sayuni! Angalia, mufalme wenu anakuja, akipanda juu ya mwana-punda.”

16 Wanafunzi wake hawakuelewa maneno haya kwanza, lakini wakati Yesu alipokwisha kutukuzwa, wakakumbuka kwamba maneno haya yameandikwa juu yake na ni vile walivyomutendea.

17 Wale watu wote waliokuwa pamoja na Yesu wakati alipomwita Lazaro toka ndani ya kaburi na kumufufua walishuhudia mambo yaliyofanyika.

18 Kwa sababu hii watu wengi walikwenda kumupokea, kwa maana walikuwa wamesikia kwamba ameonyesha kitambulisho hicho.

19 Basi Wafarisayo wakasemezana hivi: “Hamwoni kwamba hatuwezi kufanya kitu? Angalia, dunia nzima inamufuata!”


Wagriki wanamutafuta Yesu

20 Kulikuwa Wagriki wamoja kati ya wale watu waliofika Yerusalema kuabudu wakati wa sikukuu.

21 Basi wakamwendea Filipo wa kijiji cha Betesaida ya Galilaya na kumwambia: “Bwana, tunataka kuonana na Yesu.”

22 Filipo akaenda kumwambia Andrea, na kisha wote wawili wakaenda kumwelezea Yesu.

23 Yesu akawajibu: “Saa ya kutukuzwa kwa Mwana wa Mutu imetimia.

24 Kweli, kweli, ninawaambia: punje ya ngano inabaki peke yake tu, isipokuwa kama yenye kufa na kuzikwa ndani ya udongo. Lakini kama ikiwa yenye kufa, inatoa matunda mengi.

25 Anayependelea maisha yake atayapoteza, lakini asiyeyashugulikia katika dunia hii, atayachunga hata atakapopata uzima wa milele.

26 Kama mutu akitaka kunitumikia, anapaswa kunifuata, na hivi mutumishi wangu atakuwa popote nitakapokuwa. Mutu akinitumikia, Baba yangu atamupa heshima.


Yesu anatangaza kufa kwake

27 “Sasa roho yangu inafazaika. Nami sijui niseme nini. Nimwombe Baba, aniokoe toka mambo yale yatakayofika saa hii? Hapana, kwa sababu nimefika kwa ajili ya yale yatakayofanyika saa hii.

28 Baba, utukuze jina lako!” Halafu sauti ikasikilika toka mbinguni ikisema: “Nimelitukuza, nami nitalitukuza tena.”

29 Kundi la watu waliosimama pale na waliosikia sauti ile wakasema: “Ile ilikuwa ngurumo ya radi!” Wengine wakasema: “Ni malaika aliyekuwa akisema naye!”

30 Lakini Yesu akawaambia: “Sauti hii haikusikilika kwa ajili yangu, lakini kwa ajili yenu.

31 Sasa ni wakati wa dunia hii kuhukumiwa; sasa mutawala wa dunia hii atashindwa.

32 Lakini mimi, nitakaponyanyuliwa toka katika dunia, nitawavuta watu wote kuja kwangu.”

33 (Alisema hivi kwa kuonyesha ni kifo gani atakachokufa.)

34 Na lile kundi la watu wakamujibu: “Sisi tumesikia katika maandiko ya Sheria kwamba Kristo ataishi milele. Basi namna gani unaweza kusema kama Mwana wa Mutu anapaswa kunyanyuliwa juu? Na huyu Mwana wa Mutu ni nani?”

35 Yesu akawaambia: “Mwangaza ungali kati yenu kwa muda kidogo. Mutembee wakati mungali na mwangaza, kusudi giza lisiwafunike, kwa sababu anayetembea katika giza hajui pahali anapokwenda.

36 Basi muaminie mwangaza ule wakati mungali nao, kusudi mukuwe watu wa mwangaza.” Yesu alipokwisha kusema maneno hayo, akajiendea na kujificha mbali na lile kundi.


Kutokuamini kwa Wayuda

37 Ingawa vitambulisho vyote alivyoonyesha mbele yao, hawakumwamini,

38 kusudi maneno haya yaliyosemwa na nabii Isaya yatimie: “Bwana, ni nani aliyeamini habari tuliyopasha? Nani aliyefunuliwa matendo ya uwezo ya Bwana?”

39 Hawangeweza vilevile kuamini, kufuatana na maneno haya Mungu aliyomwambia Isaya tena:

40 “Mungu amepofusha macho yao, kusudi yasipate kuona. Ameifanya mioyo yao kuwa migumu, wala wasipate kunigeukia nami ningewaponyesha.”

41 Isaya alisema maneno haya kwa sababu aliona kwa mbali utukufu wa Yesu, naye alisema habari zake.

42 Hata hivi wengi kati ya wakubwa wa Wayuda wakamwamini Yesu. Lakini kwa sababu ya Wafarisayo, hawakushuhudia kwamba wameamini. Waliogopa kwamba watatengwa wasiingie katika nyumba ya kuabudia.

43 Wao walipenda kusifiwa na watu kuliko kupata sifa inayotoka kwa Mungu.


Hukumu ya kutokushika maneno ya Yesu

44 Halafu Yesu akasema hivi kwa sauti: “Anayeniamini haniamini mimi tu, lakini anamwamini vilevile yule aliyenituma.

45 Anayeniona amemwona vilevile yule aliyenituma.

46 Mimi nimekuja katika dunia kama mwangaza, kusudi mutu yeyote anayeniamini asikae katika giza.

47 Mutu akisikia maneno yangu pasipo kuyashika, si mimi nitakayemuhukumu. Kwa maana sikukuja kuhukumu dunia, lakini nilikuja kuiokoa.

48 Yule anayenikataa na asiyekubali maneno yangu atahukumiwa kufuatana nayo. Ni lile neno nililosema ndilo litakalomuhukumu siku ya mwisho.

49 Kwa maana sikusema kwa mamlaka yangu mwenyewe, lakini Baba aliyenituma ndiye aliyeniagiza maneno nitakayosema na kuyafundisha.

50 Nami ninajua kama amri yake inaleta uzima wa milele. Ni kwa hiyo maneno ninayosema, ninayasema tu kama vile Baba alivyoniagiza.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan