Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yoane 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mufano wa muchungaji na kondoo

1 Yesu akasema: “Kweli, kweli ninawaambia: mutu asiyeingia kwa mulango wa upango wa kondoo, lakini anapandia na kuingilia nafasi ingine, yeye ni mwizi na munyanganyi.

2 Lakini anayeingia kwa mulango ni muchungaji wa kondoo.

3 Zamu anamufungulia mulango na kondoo wanasikia sauti yake. Naye anawaita kondoo wake kila mumoja kwa jina lake na kuwapeleka inje.

4 Anapokwisha kuwatia hao kondoo wake inje, anawatangulia, nao wanamufuata kwa sababu wanajua sauti yake.

5 Kondoo wale hawawezi kumufuata mugeni; lakini watamukimbia, kwa sababu hawajui sauti ya mugeni.”

6 Yesu aliwaambia mufano huu, lakini hawakuelewa maneno aliyosema.


Yesu ni muchungaji mwema

7 Basi Yesu akaongeza kusema: “Kweli, kweli ninawaambia: mimi ni mulango wa upango wa kondoo.

8 Wote waliokuja mbele sijafika ni wizi na wanyanganyi; lakini kondoo hawakuwasikia.

9 Mimi ni mulango. Mutu akiingia kwa kupitia kwangu, ataokoka, ataingia na kutoka, naye atapata chakula.

10 Mwizi anakuja tu kwa kuiba, kuua na kuharibu. Mimi nimekuja kusudi watu wapate uzima, ndio uzima wa kweli kabisa.

11 “Mimi ni muchungaji mwema. Muchungaji mwema anatoa maisha yake kwa ajili ya kondoo wake.

12 Lakini mutumishi wa mushahara si muchungaji, wala kondoo si wake. Kwa sababu hii wakati anapoona imbwa wa pori anakuja, anaacha kondoo na kukimbia. Na halafu imbwa wa pori anawakamata na kuwasambaza.

13 Yeye hashuguliki na kondoo kwa sababu anatumikia mushahara tu.

14 Mimi ni muchungaji mwema. Ninajua kondoo wangu na kondoo wangu wananijua,

15 kama vile Baba anavyonijua mimi, na mimi ninavyomujua Baba. Vilevile mimi ninatoa maisha yangu kwa ajili ya kondoo wangu.

16 Niko na kondoo wengine wasiokuwa wa kundi hili. Ninapaswa vilevile kuwaleta, nao watasikia sauti yangu, na kutakuwa kundi moja na muchungaji mumoja.

17 “Baba ananipenda kwa sababu mimi mwenyewe ninajitoa kufa, kusudi nipate kuwa muzima tena.

18 Hakuna mutu anayeweza kunionodoa uzima, lakini ninajitoa mwenyewe kufa kwa mapenzi yangu. Niko na uwezo wa kujitoa kufa na niko na uwezo wa kuwa tena muzima. Ni vile Baba yangu alivyoniagiza kufanya.”

19 Kwa sababu ya maneno haya kukatokea tena mikorogano kati ya Wayuda.

20 Wengi kati yao wakasema: “Yuko na pepo! Kweli ni mwenda-wazimu! Sababu gani munamusikiliza?”

21 Lakini wengine wakasema: “Mutu anayekuwa na pepo hawezi kusema hivi. Pepo zinaweza kuponyesha macho ya vipofu?”


Wayuda wanamukataa Yesu

22 Siku moja, katika nyakati za mvua kubwa, kukakuwa sikukuu ya Kukumbuka Muzinduo wa hekalu katika Yerusalema.

23 Yesu alikuwa akitembea ndani ya hekalu katika baraza iliyoitwa baraza ya Solomono.

24 Halafu Wayuda wakamuzunguka, na kumwambia: “Mpaka wakati gani utatuzungusha kichwa? Kama wewe ni Kristo, utuambie waziwazi.”

25 Yesu akawajibu: “Nimekwisha kuwaambia ninyi, lakini hamusadiki. Matendo ninayofanya kwa mamlaka ya Baba yananishuhudia mimi.

26 Lakini ninyi hamusadiki kwa sababu ninyi si kondoo wangu.

27 Kondoo wangu wanasikia sauti yangu, ninawajua, nao wananifuata.

28 Mimi ninawapa uzima wa milele, nao hawatapotea hata milele, wala hakuna mutu anayeweza kuwanyanganya toka katika mukono wangu.

29 Baba yangu aliyenipa kondoo hawa ni mukubwa kuliko wote, na hakuna mutu anayeweza kuwanyanganya toka kwa Baba yangu.

30 Mimi na Baba yangu tuko mumoja.”

31 Halafu Wayuda wakaokota tena mawe kwa kumutupia.

32 Yesu akawaambia tena: “Nimewaonyesha matendo mengi mazuri kwa uwezo wa Baba. Ni kwa sababu ya tendo gani kati ya hayo munataka kunitupia mawe?”

33 Wayuda wakamujibu: “Hatutaki kukutupia mawe kwa ajili ya tendo zuri, lakini kwa sababu unamutukana Mungu. Wewe ni mutu tu, lakini unajifanya kuwa Mungu!”

34 Yesu akawajibu: “Imeandikwa katika sheria yenu kwamba Mungu amesema: ‘Ninyi ni miungu.’

35 Maandiko Matakatifu hayawezi kuvunjwa. Mungu aliwaita ‘miungu’ wale walioambiwa neno lake.

36 Kwa upande wangu, nilichaguliwa na Mungu na kutumwa naye katika dunia. Basi namna gani munasema kwamba ninamutukana Mungu kwa sababu nilisema kwamba mimi ni Mwana wa Mungu?

37 Kama sifanyi matendo ambayo Baba yangu ananiamuru, musiniamini.

38 Lakini kama nikiyatenda, hata ikiwa hamuniamini mimi, basi mwamini matendo yangu, kusudi mupate kujua kabisa kwamba mimi na Baba ni mumoja, yeye ni ndani yangu, nami ndani yake.”

39 Wakajaribu tena kumufunga Yesu, lakini akawaponyoka.

40 Halafu Yesu akaenda tena ngambo ingine ya Yordani, pahali Yoane alipobatiza watu zamani, na kubaki kule.

41 Watu wengi wakamufikia na kusema: “Yoane hakuonyesha hata kitambulisho kimoja, lakini maneno yote aliyoyasema juu ya mutu huyu yalikuwa ya kweli.”

42 Na kule watu wengi wakamwamini Yesu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan