Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yeremia 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yeremia anahubiri katika hekalu

1 Yawe akamutolea Yeremia ujumbe, akisema: Kwenda kusimama

2 kwenye mulango wa hekalu lake na kutangaza ujumbe huu: Musikilize neno la Yawe enyi watu wa Yuda munaoingia humu kwa kumwabudu Yawe.

3 Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Mugeuze mwenendo wenu na matendo yenu, nami nitawaacha muendelee kukaa pahali hapa.

4 Musitumainie maneno haya ya udanganyifu mukisema: Hili ni hekalu la Yawe, hekalu la Yawe, hakika hili ni hekalu la Yawe.

5 Lakini mugeuze mwenendo wenu na matendo yenu. Mufuate sheria yangu kati yenu.

6 Musiwatese wageni, wayatima au wajane au kuwaua watu wasiokuwa na kosa katika inchi hii. Musijiangamize wenyewe kwa kuabudu miungu mingine.

7 Mukifanya hivyo, mimi nitawaacha mukae siku zote pahali hapa, katika inchi niliyowapa babu wenu tangu zamani.

8 Lakini kumbe, munatumainia maneno ya udanganyifu yasiyokuwa na faida kwenu.

9 Munaiba, munaua, munafanya uzinzi, munaapa kwa uongo, munamufukizia mungu Bali ubani na kuabudu miungu mingine ambayo hamujapata kuijua.

10 Kisha, mutakuja na kusimama mbele yangu katika hekalu hili linalojulikana kwa jina langu na kusema “Tuko salama”, ingawa munaendelea kufanya mambo hayo yanayonichukiza.

11 Munazani kwamba hekalu hili linalojulikana kwa jina langu limekuwa kimbilio la wanyanganyi? Mujue kwamba mimi nimeona yote munayofanya! –Ni ujumbe wa Yawe.–

12 Muende kwenye pahali pangu kule Shilo, nafasi nilipochagua kwa kuabudiwa mara ya kwanza, muone maangamizi niliyofanya kule kwa sababu ya uovu wa watu wangu, Israeli.

13 Ninyi mumefanya mambo hayo yote. –Ni ujumbe wa Yawe.– Na hata niliposema nanyi tena na tena hamukunisikiliza. Nilipowaita hamukuitika.

14 Kwa hiyo, kama vile nilivyoutendea muji wa Shilo, ndivyo nitakavyolitendea hekalu hili linalojulikana kwa jina langu, hekalu ambalo ninyi munalitegemea; ndiyo pahali hapa ambapo niliwapa ninyi na babu zenu.

15 Nitawafukuza ninyi mbali nami kama nilivyowatupilia mbali wandugu zenu, wote wa uzao wa Efuraimu.


Kutokutii kwa watu

16 Nawe Yeremia, usiwaombee watu hawa, usinililie kwa ajili yao, usinililie kwa ajili yao wala kunisihi kwa ajili yao, maana sitakusikiliza.

17 Wewe hauoni mambo wanayofanya katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalema?

18 Watoto wanaokota kuni, wababa wanawakisha moto na wamama wanaponda unga kwa ajili ya kutengeneza mikate ya kumutambikia mungu wa kike, wanayemwita malkia wa mbinguni. Tena wananikasirikisha kwa kuitolea miungu mingine sadaka ya divai.

19 Lakini ni nani wanayemukasirikisha? Mimi? Hata kidogo! Wanajikasirikisha wao wenyewe na kujifezehesha! –Ni ujumbe wa Yawe.

20 Kwa hiyo, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Nitaimwanga hasira yangu juu ya pahali hapa, juu ya wanadamu na nyama, miti katika mashamba na juu ya mazao ya inchi. Nayo nafasi hii itawaka moto wala hautaweza kuzimishwa.

21 Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Muongeze sadaka zenu za kuteketezwa kwa moto juu ya sadaka zenu zingine, nanyi mujikulie nyama zile!

22 Maana, siku nilipowaondoa babu zenu katika inchi ya Misri, sikuwaambia kitu wala kuwapa amri yoyote juu ya sadaka za kuteketezwa na sadaka zingine.

23 Lakini niliwapa amri kwamba waitii sauti yangu kusudi nikuwe Mungu wao, nao wakuwe watu wangu. Niliwaamuru vilevile waishi kama nilivyowaagiza, kusudi wapate uheri.

24 Lakini wao hawakunitii wala kunitegea sikio. Lakini wakafuata mashauri yao wenyewe na ugumu wa mioyo yao, wakarudi nyuma pahali pa kusonga mbele.

25 Tangu siku ile babu zenu walipotoka Misri mpaka leo, sikuchoka kuwatuma kwenu manabii wote, watumishi wangu.

26 Lakini hawakunisikiliza wala kunitegea sikio, lakini wakazidi kufanya vichwa vyao kuwa vigumu na kuasi kuliko hata babu zenu.

27 Sasa wewe Yeremia utawaambia maneno haya yote, lakini wao hawatakusikiliza. Utawaita, lakini hawatakuitikia.

28 Basi utawaambia: Ninyi ni taifa ambalo halikutii sauti ya Yawe, Mungu wao, wala kukubali maonyo yake. Kwenu uaminifu umekufa; umetoweka kabisa katika vinywa vyenu.


Maovu katika Bonde la Hinomu

29 Munyoe nywele zenu na kuzitupa, enyi wakaaji wa Yerusalema: mufanye maombolezo juu ya vichwa vya milima, maana, mimi Yawe nimewakataa ninyi, nimewatupilia ninyi kizazi kilichosababisha hasira yangu!

30 Watu wa Yuda wametenda maovu mbele yangu. Wameweka sanamu zenye kuchukiza ndani ya nyumba hii inayojulikana kwa jina langu na kuichafua.

31 Wamejenga mazabahu inayoitwa “Tofeti” huko kwenye bonde la Mwana wa Hinomu, kwa kuwatolea wana na wabinti kuwa sadaka ya kuteketezwa kwa moto. Mimi sikukuwa nimewaamuru kufanya jambo hilo, wala halikunifikia katika mafikiri.

32 Kwa sababu hiyo, siku zinakuja ambapo hawataliita tena “Tofeti”, au “bonde la Mwana wa Hinomu”, lakini wataliita “bonde la Mauaji”. –Ni ujumbe wa Yawe.– Huko ndiko watakakozika watu, kwa sababu hapatakuwa pahali pengine pa kuzikia.

33 Maiti za watu hao zitakuwa chakula cha ndege na nyama wa pori, na hapatakuwa mutu atakayewafukuza.

34 Inchi itakuwa jangwa na katika miji ya Yuda na barabara za Yerusalema nitakomesha sauti zote za furaha na shangwe, nazo nyimbo za wenye kufanya ndoa, kwa sababu inchi itakuwa ukiwa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan