Yeremia 52 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maangamizi ya Yerusalema ( 2 Fal 24.18–25.7 ) 1 Zedekia alikuwa na umri wa miaka makumi mbili na mumoja alipoanza kutawala. Alitawala kwa muda wa miaka kumi na mumoja akiwa kule Yerusalema. Mama yake aliitwa Hamutali binti wa Yeremia, mukaaji wa muji wa Libuna. 2 Alitenda maovu mbele ya Yawe akifuata yote Yoyakimu aliyofanya. 3 Yawe aliwakasirikia sana watu wa Yerusalema na Yuda hata akawafukuza mbali naye. Zedekia alimwasi mufalme wa Babeli. 4 Ikakuwa katika siku ya kumi ya mwezi wa kumi, mwaka wa kenda wa utawala wa Zedekia, Nebukadneza mufalme wa Babeli, alifika na waaskari wake wote kuushambulia Yerusalema, wakauzunguka kila upande. 5 Muji uliendelea kuzungukwa mpaka mwaka wa kumi na mumoja wa utawala wa Zedekia. 6 Katika siku ya kenda ya mwezi wa ine, njaa ilikuwa kali sana katika muji hata hakukukuwa chakula chochote kwa ajili ya wakaaji wake. 7 Basi, sehemu ya ukuta wa muji ilibomolewa na waaskari walikimbia. Wakatoka inje ya muji wakati wa usiku wakipitia njia ya mulango katikati ya kuta mbili, kwenye bustani ya mufalme, ingawa Wakaldea walikuwa wameuzunguka muji wote. Wakakimbia kuelekea bonde la muto Yordani. 8 Lakini kundi la Wakaldea lilimufuatilia mufalme na kumukamata katika bonde la Yeriko, waaskari wake wote wakatawanyika na kumwacha. 9 Basi Wakaldea walimukamata mufalme, wakamupeleka kwa mufalme wa Babeli kule Ribla, katika inchi ya Hamati, naye akamuhukumu. 10 Kulekule Ribla, mufalme wa Babeli aliwaua wana wa Zedekia mbele ya baba yao. Aliwaua vilevile wakubwa wote wa inchi ya Yuda. 11 Kisha aliyaongoa macho ya Zedekia na kumufunga minyororo, akamupeleka Zedekia Babeli na kumutia katika kifungo mpaka siku alipokufa. Kuharibiwa kwa hekalu ( 2 Fal 25.8-17 ) 12 Katika siku ya kumi ya mwezi wa tano, mwaka wa kumi na kenda wa utawala wa Nebukadneza, mufalme wa Babeli, Nebuzaradani mukubwa wa waaskari wa mufalme ambaye alimutumikia mufalme wa Babeli, aliingia Yerusalema. 13 Aliteketeza kwa moto nyumba ya Yawe, nyumba ya kifalme na nyumba zote za Yerusalema; kila nyumba kubwa ilichomwa kwa moto. 14 Waaskari wote wa Wakaldea waliokuwa pamoja na mukubwa wa waaskari, walizibomoa kuta zote zilizouzunguka Yerusalema. 15 Nebuzaradani mukubwa wa waaskari wa mufalme, aliwapeleka katika uhamisho watu waliokuwa wamebakia katika muji na wale waliojitoa wenyewe kwa mufalme wa Babeli pamoja na wafundi. 16 Lakini Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, aliwaacha watu wamoja waliokuwa wamasikini kabisa katika inchi, wakuwe watunza mizabibu na walimaji. 17 Wakaldea walivunja vipandevipande nguzo za shaba nyeusi ambazo zilikuwa katika nyumba ya Yawe pamoja na misingi ya birika kubwa la shaba nyeusi lililokuwa katika nyumba ya Yawe, wakapeleka shaba nyeusi yote mpaka Babeli. 18 Vilevile, walipeleka vyungu, majembe, makasi, makarai, vijiko vikubwa na vyombo vyote vya shaba nyeusi vilivyotumiwa katika kazi ya hekalu. 19 Yule mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme alipeleka vibakuli, vyetezo, mabeseni, vyungu, vinara vya taa, vijiko vikubwa na mabakuli ya sadaka za vinywaji, vyombo hivyo vikiwa vya zahabu au vya feza. 20 Juu ya vitu Solomono alivyotengeneza: nguzo mbili, birika kubwa moja na sanamu za ngombe dume kumi na mbili za shaba nyeusi ambazo zilikuwa chini ya hilo birika kubwa pamoja na misingi, shaba nyeusi ya vitu hivi vyote ilikuwa na uzito mwingi sana. 21 Kila moja ya nguzo hizo mbili ilikuwa na urefu wa metre nane, muzunguko wake metre tano na sentimetre makumi tatu, na unene wa sentimetre saba na nusu, zote zilikuwa wazi ndani. 22 Juu ya kila nguzo kulikuwa kichwa cha shaba nyeusi; urefu wa kila kichwa ulikuwa metre mbili na sentimetre makumi mbili. Kila kichwa kilizungushiwa mapambo ya makomamanga, yote ya shaba nyeusi. 23 Kulikuwa makomamanga makumi kenda na sita kwenye ubavu wa nguzo hizo; jumla ya makomamanga yote ilikuwa mia moja na mapambo kandokando yake. Watu wa inchi ya Yuda wanapelekwa Babeli ( 2 Fal 25.18-21 , 27-30 ) 24 Kisha Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, alimukamata Seraya Kuhani Mukubwa, na Zefania kuhani wa pili, pamoja na walinda mulango watatu; 25 na kutoka katika muji alimukamata mukubwa mumoja ambaye alikuwa akiongoza waaskari katika vita, pamoja na watu saba washauri wa mufalme ambao aliwakuta katika muji. Alimukamata vilevile katibu wa jemadari mukubwa wa waaskari ambaye alishugulika na kazi ya kuandika waaskari wapya, pamoja na watu wakubwa makumi sita ambao aliwakuta katika muji Yerusalema. 26 Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, aliwakamata watu hao na kuwapeleka kwa mufalme wa Babeli kule Ribla. 27 Mufalme Nebukadneza wa Babeli aliwapiga na kuwaua watu hao kule Ribla katika inchi ya Hamati. Basi, hivi ndivyo watu wa Yuda walikwenda katika uhamisho inje ya inchi yao. 28 Hii ndiyo hesabu ya watu ambao Nebukadneza aliowapeleka katika uhamisho kwa mwaka wa saba wa utawala wake: Wayuda elfu tatu na makumi mbili na watatu. 29 Mwaka wa kumi na nane na utawala wake, alipeleka kutoka Yerusalema watu mia nane makumi tatu na wawili. 30 Mwaka wa makumi mbili na tatu wa utawala wa Nebukadneza, Nebuzaradani mukubwa wa waaskari walinzi wa mufalme, aliwapeleka Wayuda mia saba na makumi ine na watano. Jumla ya watu wote ilikuwa watu elfu ine mia sita. 31 Katika mwaka wa makumi tatu na saba tangu Yoyakinu mufalme wa Yuda alipopelekwa katika uhamisho, siku ya makumi mbili na tano ya mwezi wa kumi na mbili, Ewili-Merodaki akakuwa mufalme wa Babeli. Mwaka uleule alipofanywa mufalme, alimusamehe Yoyakinu mufalme wa Yuda, akamwondoa katika kifungo. 32 Aliongea naye vizuri na kumupatia nafasi ya heshima kuliko wafalme wengine waliokuwa pamoja naye katika uhamisho kule Babeli. 33 Basi, Yoyakinu alibadilisha nguo zake za wafungwa, akakuwa anapata chakula chake siku zote kwenye meza ya mufalme. 34 Siku zote alipewa posho na mufalme wa Babeli kulingana na mahitaji yake ya kila siku, mpaka alipokufa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo