Yeremia 51 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Yawe anasema hivi: Nitavumisha upepo wa kuangamiza juu ya Babeli na juu ya wakaaji wa Kaldea. 2 Nitawapeleka wapepetaji katika inchi ya Babeli, nao watamupepeta; watamaliza kila kitu katika inchi yake watakapofika kuishambulia toka kila upande wakati wa maangamizi yake. 3 Usiwape nafasi wapiga mushale wa Babeli; usiwaache wavute upinde, wala kuvaa nguo zao za vita. Usiwahurumie vijana wake; uangamize kabisa jeshi lake. 4 Wataanguka na kuuawa katika inchi ya Wakaldea, wataumizwa katika barabara zake. 5 Lakini Israeli na Yuda hawakuachiliwa na Mungu wao, Yawe wa majeshi, ingawa inchi yao imejaa makosa mbele ya Mutakatifu wa Israeli. 6 Mukimbie kutoka Babeli, kila mutu apate kuyaokoa maisha yake! Musiangamizwe katika azabu yake, maana huu ndio wakati wa Mungu wa kulipiza kisasi, anaiazibu Babeli kama inavyostahili. 7 Babeli ilikuwa kikombe cha zahabu katika mukono wa Yawe, ambacho kiliilewesha dunia nzima. Mataifa yalikunywa divai yake; kwa hiyo, yakapata wazimu. 8 Kwa rafla Babeli imeanguka na kuvunjikavunjika; muomboleze kwa ajili yake! Mulete dawa kwa kutuliza maumivu yake; labda utaweza kupona. 9 Tulijaribu kuuponyesha Babeli, lakini hauwezi kupona. Muuache, tujiendee, kila mumoja katika inchi yake. Hukumu yake ni kubwa sana inafika mpaka katika mawingu. 10 Yawe amehakikisha kwamba hatuna kosa. Tuende Sayuni tutangaze matendo ya Yawe, Mungu wetu. 11 Yawe amezichochea roho za wafalme wa Wamedi, kwa maana amekusudia kuiangamiza Babeli. Kweli, hicho ndicho kisasi cha Yawe; analipiza kisasi kwa ajili ya hekalu lake. Munoe mishale yenu! Mutwae ngao! 12 Mupandishe bendera ya vita kwa kushambulia kuta za Babeli. Muimarishe walinzi, muweke walinzi, mutayarishe mashambulizi. Yawe amepanga na kutimiza mambo aliyosema juu ya wakaaji wa Babeli. 13 Inchi hiyo imejaa mito na akiba tele, lakini mwisho wake umefika, uzi wa uzima wake umekatwa. 14 Yawe wa majeshi ameapa kwa nafsi yake: Hakika nitakujaza na watu kama vile nzige, nao watapiga vigelegele vya ushindi juu yako. 15 Yawe ndiye aliyeumba dunia kwa nguvu zake, aliyeuimarisha ulimwengu kwa hekima yake, na kwa akili yake akazitandaza mbingu. 16 Anapotoa sauti yake maji yanajikusanya mbinguni, anafanya ukungu upande kutoka mipaka ya dunia. Anafanya umeme upige wakati wa mvua, anavumisha upepo kutoka gala zake. 17 Kila mutu ni mupumbafu bila maarifa, kila mufua vyuma anapatishwa haya na miungu yake; maana sanamu zake ni udanganyifu mutupu, wala hazina pumzi ndani yake. 18 Hazina maana, ni udanganyifu mutupu; wakati watakapoazibiwa, nazo zitaangamia. 19 Mungu anayekuwa hazina ya Yakobo si kama hizo, maana yeye ndiye aliyeviumba vitu vyote, na Israeli ni kabila linalokuwa mali yake; Yawe wa majeshi, ndilo jina lake. Mwisho wa Babeli 20 Yawe anasema hivi: Wewe Babeli ni nyundo na silaha yangu ya vita; ninakutumia kwa kuyavunjavunja mataifa, ninakutumia kwa kuangamiza falme. 21 Ninakutumia kwa kuponda farasi na waaskari wapanda-farasi, magari ya kukokotwa na watembezaji wake. 22 Ninakutumia kwa kuwaponda wanaume na wanawake, wazee na vijana, vijana wanaume na wabinti. 23 Ninakutumia kwa kuponda wachungaji na makundi yao, walimaji na nyama wao wanaotumia kwa kulima, wakubwa na maliwali. 24 Nitaiazibu Babeli na wakaaji wote wa Kaldea mukiona kwa macho yenu wenyewe, kwa sababu ya uovu wote walioufanya katika Sayuni. –Ni ujumbe wa Yawe. 25 Mimi ninapingana nawe, ewe mulima muharibifu, mulima unaoharibu dunia nzima! –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitanyoosha mukono wangu juu yako kwa kukuazibu, nitakuangusha kutoka juu kwenye mawe makubwa na kukufanya kuwa mulima uliochomwa kwa moto. 26 Kwako hakutapatikana jiwe la kujenga, hata jiwe kwa kujenga musingi! Utakuwa kama jangwa milele. –Ni ujumbe wa Yawe!– 27 Pandisha bendera ya vita katika dunia, piga baragumu kati ya mataifa; uyatayarishe mataifa kwa kupigana naye; uziite falme kwa kuishambulia; falme za Ararati, Mini na Askenazi. Weka jemadari juu yake; ulete farasi kama makundi ya nzige. 28 Mutayarishe mataifa kwa kupigana naye vita; muwatayarishe wafalme wa Medi, watawala na maliwali wao, mutayarishe inchi zote katika utawala wao. 29 Inchi inatetemeka na kugaagaa kwa maumivu, maana nia ya Yawe juu ya Babeli ni imara: ataifanya inchi ya Babeli kuwa jangwa, ataifanya ikuwe bila watu. 30 Waaskari wa Babeli wameshindwa kupigana, wamebaki katika makimbilio yao; nguvu zao zimewaishia, wamekuwa kama wanawake. Nyumba za Babeli zimechomwa kwa moto, milango yake ya chuma imevunjwa. 31 Wakimbiaji wanakimbia wakitoleana ujumbe mumoja kwa mwingine kwa kumupasha mufalme wa Babeli habari kwamba muji wake umeshambuliwa kila upande. 32 Vivuko vya muto vimetekwa, makimbilio yamechomwa kwa moto, waaskari wamepatwa na hofu. 33 Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Babeli ni kama uwanja wa kupepetea ngano wakati unapotayarishwa. Lakini bado kidogo tu, wakati wa mavuno utaufikia. 34 Mufalme Nebukadneza wa Babeli aliuharibu na kuuponda Yerusalema aliuacha kama chungu kitupu; aliumeza kama vile nyoka mukubwa. Alijaza tumbo lake vitu vyake vizurivizuri, akautupilia mbali kama matapiko. 35 Watu wa Sayuni watasema: Babeli ulipizwe mateso makali yaleyale tuliyotendewa sisi pamoja na jamaa zetu! Yerusalema itasema: Damu yangu ikuwe juu ya wakaaji wa Kaledea. Yawe atasaidia 36 Kwa hiyo Yawe anasema hivi: Nitawatetea juu ya maneno yenu, na kulipiza kisasi kwa ajili yenu. Nitaikausha bahari ya Babeli na kuvifanya visima vyake vikauke. 37 Babeli itakuwa lundo la mabomoko, itakuwa makao ya mbweha, itakuwa machukizo na kitu cha kuzomewa; hakuna mutu atakayekaa ndani yake. 38 Wababeli watanguruma pamoja kama simba; watalia kama wana-simba. 39 Wakiwa na hamu kubwa nitawatayarishia karamu: nitawalewesha mpaka wapepesuke; nao watalala usingizi wa siku zote na hawataamuka tena. –Ni ujumbe wa Yawe.– 40 Nitawashusha chini kama kondoo wa kuchinjwa, kama vile kondoo dume na beberu. 41 Namna gani Babeli imetekwa; muji uliosifiwa katika dunia yote umekamatwa! Babeli umekuwa ukiwa kati ya mataifa! 42 Bahari imefurika juu ya Babeli, Babeli imefunikwa na mawimbi yaliyochafuka. 43 Miji yake imekuwa ukiwa, inchi yenye kukauka na jangwa, inchi isiyokaliwa na mutu yeyote, wala hakuna mwanadamu yeyote anayepita ndani yake. 44 Nitamwazibu mungu Beli huko Babeli, nitamutapikisha kile alichomeza. Mataifa hayatamwendea tena kwa wingi. Ukuta wa Babeli umebomoka. 45 Mutoke humo, enyi watu wangu! Kila mutu apate kuyaokoa maisha yake, kutoka hasira kali ya Yawe. 46 Musiregee wala musikuwe na hofu, kwa sababu ya habari munazosikia katika inchi. Mwaka huu kuna habari hii, mwaka mwingine habari ingine; habari ya mateso makali katika inchi, mutawala mumoja anapigana na mutawala mwingine. 47 Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitaazibu sanamu za Babeli; inchi yake yote itapata haya, watu wake wote watauawa humohumo. –Ni ujumbe wa Yawe.– 48 Kisha mbingu, dunia na vyote vinavyokuwa ndani yao vitaimba kwa furaha juu ya kuanguka kwa Babeli, wakati waangamizaji watakapofika kutoka upande wa kaskazini kuushambulia. –Ni ujumbe wa Yawe.– 49 Babeli umesababisha vifo katika dunia yote; sasa muji wenyewe utaangamizwa kwa ajili ya mauaji ya Waisraeli. 50 Ninyi mulioponyoka kifo, muondoke sasa, wala musisitesite! Ingawa muko katika inchi ya mbali, mumukumbuke Yawe, muukumbuke vilevile Yerusalema. 51 Ninyi munasema: Tumepatishwa haya na kutukaniwa; haya imefunika nyuso zetu, kwa sababu wageni wameingia katika sehemu takatifu za nyumba ya Yawe. 52 Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitaiazibu miungu ya Babeli, na wenye kuumizwa watalalamika katika inchi yake yote. –Ni ujumbe wa Yawe.– 53 Ingawa Babeli ungepanda mpaka mbinguni, na kuziimarisha kuta zake ndefu, waangamizaji watakuja kutoka kwangu kwa kuuharibu. –Ni ujumbe wa Yawe. Maangamizi zaidi juu ya Babeli 54 Sikiliza! Kilio kinasikilika kutoka Babeli! Kishindo cha maangamizi makubwa kutoka inchi ya Wakaldea! 55 Maana mimi Yawe ninaiangamiza Babeli, na kuikomesha kelele yake kubwa. Waadui wananguruma kama mawimbi ya maji mengi, sauti ya kishindo chao inaongezeka. 56 Kweli, mwangamizaji anashambulia Babeli; waaskari wake wametekwa, pinde zao zimevunjwavunjwa. Mimi Yawe ni Mungu mwenye kuazibu, hakika mimi nitalipiza kisasi kamili. 57 Nitawalewesha wakubwa na wenye hekima wake, watawala wake, maliwali na waaskari wake; watalala usingizi wa milele wala hawataweza tena kuamuka. –Ni ujumbe wa mufalme, jina lake Yawe wa majeshi! 58 Yawe wa majeshi anasema hivi: Ukuta mukubwa wa Babeli utabomolewa mpaka chini, na milango yake mirefu itateketezwa kwa moto. Watu wanafanya juhudi za bure, mataifa yanajichokesha, maana mwisho wao ni katika moto! Ujumbe wa Yeremia unapelekwa Babeli 59 Katika mwaka wa ine wa utawala wake, mufalme Zedekia alikwenda Babeli pamoja na mukubwa wa wasimamizi wa nyumba yake anayeitwa Seraya mwana wa Neria na mujukuu wa Maseya. Wakati huo mimi Yeremia nilimutolea Seraya ujumbe. 60 Nilikuwa nimeandika katika kitabu hasara yote niliyotangaza juu ya Babeli na vilevile maneno mengine juu ya Babeli. 61 Nilimwambia Seraya: Utakapofika Babeli ni lazima uwasomee wote maneno haya. 62 Kisha umalizie na maneno haya: Ee Yawe, wewe umesema kwamba utaharibu nafasi hii hata kusikaliwe na kiumbe chochote, mwanadamu au nyama, na kwamba inchi hii itakuwa jangwa milele. 63 Utakapomaliza kusoma kitabu hiki, ufunge jiwe juu yake, kisha ukitumbukize katikati ya muto Furati, ukisema: 64 Hivi ndivyo Babeli utakavyozama, wala hautainuka tena, kwa sababu ya hasara ambayo Yawe anauletea. Huu ndio mwisho wa maneno ya Yeremia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo