Yeremia 49 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Neno la Mungu juu ya Waamoni 1 Juu ya Waamoni, Yawe anasema hivi: Israeli hana watoto? Hana warizi? Mbona basi mungu Milkomu ametwaa Gadi na watu wake wanafanya makao yao katika miji yake? 2 Kwa hiyo, siku zinakuja ambapo nitavumisha sauti ya vita juu ya Raba muji wa Waamoni. –Ni ujumbe wa Yawe.– Raba utakuwa lundo la uharibifu, vijiji vyake vitateketezwa kwa moto. Halafu Israeli atatwaa tena urizi wake. Ni Yawe anayesema hivyo. 3 Muomboleze, enyi watu wa Hesiboni, maana muji Ai umeharibika! Mulie, enyi wabinti wa Raba! Muvae magunia, muomboleze na kukimbia huko na huko ndani ya ukuta wenu! Maana mungu Milkomu atapelekwa katika uhamisho, pamoja na makuhani wake na watumishi wake. 4 Mbona munajivunia mabonde yenu, enyi musiokuwa waaminifu, ninyi watu muliotegemea mali zenu, mukisema: Nani atasubutu kupigana nasi? 5 Basi, mimi nitawaletea vitisho. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe wa majeshi.– Hivi vitisho vitatoka kwa wajirani zenu wote, nanyi mutafukuzwa inje, kila mutu kwa njia yake, wala hakuna mutu atakayekusanya wakimbizi. 6 Lakini kisha nitawarudisha tena Waamoni katika hali yao. –Ni ujumbe wa Yawe. Neno la Mungu juu ya Edomu 7 Juu ya Edomu, Yawe wa majeshi anasema hivi: Hakuna tena hekima katika muji wa Temani? Wenye hekima wao hawana shauri tena? Hekima imetoweka kabisa? 8 Mukimbie, enyi wakaaji wa Dedani, mugeuke na kujificha ndani ya mapango! Maana nitawaletea maangamizi, enyi wazao wa Esau; wakati wa kuwaazibu umefika. 9 Wachuma zabibu watakapokuja kwenu, hawataacha hata zabibu moja. Usiku ule wizi watakapofika, wataharibu kila kitu mpaka watosheke. 10 Lakini nimemunyanganya Esau kila kitu, nimeyafunua maficho yake, wala hawezi kujificha tena. Watoto, wandugu na jirani zake wameangamizwa; hakuna hata mumoja aliyebaki. 11 Muniachie watoto wenu wayatima nami nitawatunza; muwaache wajane wenu wanitegemee. 12 Yawe anasema hivi: Ikiwa wale ambao hawakustahili kunywa kikombe cha azabu ni lazima wakikunywe, basi, wewe utaachwa bila kuazibiwa? Hapana! Hautakosa kuazibiwa; ni lazima ukunywe hicho kikombe! 13 Maana nimeapa kwa nafsi yangu kwamba muji wa Bosira utakuwa kitisho na mushangao, utakuwa uharibifu na kutumiwa kama mufano wa laana; vijiji vyote vitakuwa mabomoko siku zote. –Ni ujumbe wa Yawe. 14 Nimepata habari kutoka kwa Yawe, na mujumbe ametumwa ayatangazie mataifa: Mujikusanye pamoja juu ya Edomu; musimame muende kushambulia! 15 Mimi Yawe nitakufanya wewe Edomu kuwa mudogo kuliko mataifa yote. Ulimwengu wote utakuzarau. 16 Vitisho unavyotoa na kiburi chako vimekudanganya, ewe unayekaa katika mapango ya mawe, unayeishi juu ya kilele cha mulima! Ingawa unaweka makao yako juu kama ya tai, mimi nitakuporomosha kutoka huko unakokuwa. –Ni ujumbe wa Yawe. 17 Inchi ya Edomu itakuwa kitisho na kila mutu atakayepita karibu yake atashangaa, na kuizomea kwa sababu ya hasara itakayoipata. 18 Kama vile Sodoma na Gomora na miji jirani yake ilivyoangamizwa, hakutakuwa mutu yeyote atakayeishi Edomu wala kufanya mashauri humo. –Ni Yawe anayesema.– 19 Kama vile simba anavyochomoka kutoka ndani ya vichaka vya muto Yordani na kuingia kwenye mbuga, ndivyo nitakavyowafukuza kwa rafla Waedomu toka katika inchi yao. Nami nitamuweka huko mutawala yeyote nitakayemuchagua. Maana, ni nani anayeweza kulinganishwa nami? Nani anayeweza kunishitaki? Ni muchungaji gani anayeweza kunipinga? 20 Kwa hiyo, musikilize mupango ambao mimi Yawe nimepanga juu ya Edomu pamoja na mambo niliyokusudia kuwafanyia wakaaji wa Temani: Hakika, watoto wao wadogo watakokotwa na kukamatwa; kweli kutakuwa mushangao mukubwa katika makao yao! 21 Kwa kishindo cha kuanguka kwao, dunia itatetemeka, na kilio chao kitasikilika mpaka kwenye bahari Nyekundu. 22 Adui atapanda juu na kuruka kama tai na kutandaza mabawa yake juu ya Bosira. Siku hiyo moyo wa mashujaa wa Edomu utakuwa kama vile moyo wa mwanamuke anayezaa. Neno la Mungu juu ya Damasiki 23 Hii ni juu ya Damasiki: Miji ya Hamati na Arpadi, imejaa wasiwasi kwa kufikiwa na habari mbaya; mioyo ya watu wake inayeyuka kwa hofu, imefazaika kama bahari isiyoweza kutulia. 24 Watu wa Damasiki wamevunjika moyo; wamegeuka kusudi wapate kukimbia; hofu kubwa imewashika, uchungu na huzuni vimewapata, kama mwanamuke anayezaa. 25 Namna gani muji wenye sifa umeachwa, muji uliokuwa umejaa furaha! 26 Basi vijana wake wataanguka katika viwanja vyake, waaskari wake wote wataangamizwa siku hiyo. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi. 27 Nitawasha moto katika kuta za Damasiki, nao utateketeza nyumba nzuri za mufalme Beni-Hadadi. Neno la Mungu juu ya makabila ya Kedari na Hazori 28 Juu ya Kedari na falme za Hazori ambazo Nebukadneza mufalme wa Babeli alizishambulia na kuzishinda, Yawe anasema hivi: Simama uende kulishambulia kabila la Kedari! Uwaangamize watu wa mashariki! 29 Hema zao na kondoo wao vitakamatwa, vilevile na mapazia yao na mali yao yote; watanyanganywa ngamia wao, na kilio kitasikilika: Kitisho kila upande! 30 Mukimbie, muende mbali, mukae ndani ya mashimo. Enyi wakaaji wa Hazori, mukimbie, mutangetange na kujificha mbali! –Ni ujumbe wa Yawe.– Maana Nebukadneza mufalme wa Babeli, amefanya mupango juu yenu, amekusudia kuja kuwashambulia. 31 Simama uende kulishambulia taifa linalostarehe, taifa linaloishi kwa usalama. –Ni ujumbe wa Yawe.– Taifa hilo halina milango wala vifungio vya chuma; ni taifa ambalo liko peke yake. 32 Ngamia wao watatekwa, makundi yao ya nyama yatanyanganywa. Nitawasambaza kila upande, watu wale wanaonyoa nywele zote za pembenipembeni ya kichwa. Nitawaletea hasara kutoka kila upande. –Ni ujumbe wa Yawe. 33 Muji wa Hazori utakuwa makao ya mbweha, utakuwa jangwa siku zote; hakuna mutu atakayekaa humo, wala atakayeishi humo. Neno la Mungu juu ya Elamu 34 Yawe akamutolea nabii Yeremia ujumbe huu juu ya Elamu, kwa mwanzo wa utawala wa Zedekia, mufalme wa Yuda. 35 Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitavunja upinde wa watu wa Elamu unaokuwa musingi wa nguvu zao. 36 Nitaleta upepo kutoka pande zote za mbingu; nitawatawanya kila pahali, wala hakutakuwa taifa lolote ambalo halitakuwa na wakimbizi wa Elamu. 37 Nitawafazaisha watu wa Elamu mbele ya waadui zao na mbele ya wale wanaotaka kuyaangamiza maisha yao. Nitawaletea hasara na hasira yangu kali. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitawashambulia kwa upanga mpaka niwaangamize kabisa. 38 Nitaweka kiti changu cha kifalme huko Elamu na kumwangamiza mufalme wao pamoja na wakubwa wao. –Ni ujumbe wa Yawe! 39 Lakini katika siku za mwisho, nitaurudishia muji wa Elamu hali yake. –Ni ujumbe wa Yawe! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo