Yeremia 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yawe anawaita Waisraeli watubu 1 Yawe anasema hivi: Ukitaka kurudi, ee Israeli, unirudilie mimi. –Ni ujumbe wa Yawe.– Ukiviondoa vitu vyako vya kuchukiza mbele yangu, usipotangatanga huko na huko, 2 ukiapa kwa ukweli, kwa kufuatana na sheria, na kwa haki, kwa kusema “Kama vile Yawe anavyoishi”, halafu mataifa yatapata baraka kutoka kwangu, na kutukuzwa kwa sababu yangu. 3 Yawe anawaambia hivi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema: Mulime mashamba yenu mapya; musipande mbegu zenu penye miiba. 4 Enyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema, mujitahiri, mukiondoa govi za mioyo yenu, mupate kujitoa kwa Yawe. Kama si vile, kasirani yangu itawaka kama moto, nayo itaunguza wala hakuna atakayeizimisha, kwa sababu ya matendo yenu maovu. Watu wa Yuda wako katika hatari 5 Mutoe tangazo, mupashe habari huko Yerusalema! Mupige baragumu kila pahali katika inchi! Mulalamike, mukisema: Mukusanyike pamoja! Mukimbilie katika miji yenye kuzungukwa na kuta! 6 Muinue bendera ya vita kuelekea Sayuni, kusudi mukimbie, wala musisitesite! Yawe analeta hasara, analeta maangamizi makubwa kutoka kaskazini. 7 Kama simba anavyotoka kwenye maficho yake, mwangamizaji wa mataifa ameanza kuja, anakuja kutoka pahali pake, kusudi aharibu inchi yenu. Miji yenu itabaki mabomoko matupu, bila kukaliwa na mutu yeyote. 8 Kwa hiyo, muvae gunia, muomboleze na kulia; kwa maana Yawe hajaondoa hasira yake kali kwenu. 9 Siku hiyo, mufalme na wakubwa wataregea moyo. Makuhani watapigwa na bumbuazi, na manabii watashangaa. –Ni ujumbe wa Yawe. 10 Kisha nikasema: Ee, Bwana wangu Yawe, hakika umewadanganya kabisa watu hawa, nao Yerusalema! Uliwaambia mambo yataongoka vizuri kwao, kumbe maisha yao yako katika hatari kabisa! 11 Wakati huo, wataambiwa hivi watu hawa pamoja na muji Yerusalema: Upepo wenye kuunguza kutoka vilele vya milima katika jangwa utawavumia watu wangu. Huo si upepo mudogo wa kupepeta ngano, 12 lakini ni upepo mukali sana unaotoka kwangu. Ni mimi Yawe nitakayetoa hukumu juu yao. Yuda inazungukwa na waadui 13 Angalia! Adui anakuja akivuma kama mawingu. Magari yake ya vita ni kama zoruba, nao farasi wake wa vita wanaruka mbio kuliko tai. Ole kwetu! Tumeangamia! 14 Wewe Yerusalema, usafishe maovu ya moyo wako, kusudi upate kuokolewa. Mpaka wakati gani utaendelea kuchunga maovu? 15 Sauti kutoka Dani inatoa tangazo; inatangaza hasara kutoka vilima vya Efuraimu. 16 Inayaarifu mataifa, inaitangazia Yerusalema maneno haya: Washambulizi wanakuja kutoka inchi ya mbali, wanaitisha miji ya Yuda, 17 wanauzunguka Yerusalema kama walinzi wanavyozunguka mashamba, kwa sababu watu wake wameniasi. –Ni ujumbe wa Yawe. 18 Wewe Yuda, hayo yote yamekupata kwa ajili ya mwenendo na matendo yako. Hiyo ndiyo hasara inayokufikia, tena ni yenye uchungu; yamepenya mpaka ndani ya moyo wako. Yeremia anawasikitikia watu wake 19 Uchungu, uchungu! Ninagaagaa kwa uchungu! Moyo wangu unapigapiga vibaya. Wala siwezi kukaa kimya. Maana ninaogopa mulio wa baragumu, ninasikia kelele la vita. 20 Wanatangaza hasara zisizokoma; inchi yote imeharibiwa. Kwa rafla mahema yetu yameharibiwa, mapazia yao yamepasuka kwa dakika moja. 21 Mpaka wakati gani nitaendelea kuona bendera za vita na kusikia mulio wa baragumu? 22 Yawe anasema: Watu wangu ni wapumbafu, hawanijui mimi. Wao ni watoto wajinga; hawana ufahamu. Wao wanaelewa vizuri kutenda maovu, lakini hawajui kutenda mema. Ono la Yeremia juu ya maangamizi 23 Niliangalia dunia, nikaona imekuwa ukiwa na tupu; niliangalia mbingu, nazo hazikukuwa na mwangaza. 24 Niliangalia milima, nikaiona ikitetemeka, navyo vilima vyote vilikuwa vikiyumbayumba. 25 Niliangalia wala sikuona mutu; hata ndege katika anga walikuwa wametoweka. 26 Niliona inchi yote yenye mboleo imegeuka jangwa, nayo miji yake yote imebaki mabomoko matupu, kwa sababu ya hasira kali ya Yawe. 27 Maana Yawe anasema hivi: Inchi nzima itakuwa jangwa tupu; lakini sitaiharibu kabisa. 28 Kwa hiyo, inchi itaomboleza, na mbingu zitakuwa nyeusi. Maana nimesema nami sitabadilisha nia yangu; nimeamua, wala sitarudi nyuma. 29 Kelele la waaskari wapanda-farasi na la wapiga mishale litakaposikilika, watu wote watakimbia. Wamoja wao watakimbilia katika vichaka, wengine watajificha katikati ya mawe. Kila muji utaachwa tupu; hakuna mutu atakayekaa ndani yake. 30 Nawe Yerusalema uliyeachwa tupu, kwa nini sasa unavaa nguo nzuri nyekundu? Kwa nini kujipamba kwa zahabu, na kujipakaa wanja kwenye macho? Unajipamba bure! Wapenzi wako wanakuzarau sana; wanatafuta kukuua tu. 31 Nilisikia sauti kama ya mwanamuke anayezaa, malalamiko kama ya mwenye kuzaa mutoto wa kwanza. Ilikuwa sauti ya Yerusalema akipumuapumua kwa uchungu, na kuinyooshanyoosha mikono yake, akisema: Ole wangu! Wanakuja kuniua! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo