Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yeremia 37 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Zedekia anakwenda kuomba shauri kwa Yeremia

1 Mufalme Nebukadneza wa Babeli alimusimika Zedekia mwana wa Yosia kuwa mufalme wa Yuda pahali pa Konia mwana wa Yoyakimu.

2 Lakini Zedekia na wakubwa wake pamoja na wanainchi wa Yuda hawakusikiliza maonyo Yawe aliyotoa kwa njia ya nabii Yeremia.

3 Mufalme Zedekia aliwatuma Yehukali mwana wa Selemia, pamoja na kuhani Zefania mwana wa Maseya, kwa nabii Yeremia kusema awaombee kwa Yawe, Mungu wao.

4 Wakati huo, Yeremia alikuwa angali na uhuru wa kutembea kati ya watu, maana alikuwa hajatiwa katika kifungo.

5 Tena waaskari wa mufalme wa Misri walikuwa wameondoka Misri, na waaskari wa Wakaldea walikuwa wameuzunguka Yerusalema waliposikia habari hizo waliondoka.

6 Halafu neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi:

7 Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Utamwambia mufalme wa Yuda hivi ambaye amekutuma uniombe kwa ajili yake: Waaskari wa Mufalme wa Misri waliokuja kukusaidia, wako karibu kurudia kwao Misri.

8 Na Wakaldea watarudi kuushambulia muji huu. Watauteka muji na kuuteketeza kwa moto.

9 Yawe anasema hivi: Musijidanganye wenyewe na kusema kwamba waaskari wa Wakaldea wataondoka. Kweli hawataondoka.

10 Hata kama mukiwashinda waaskari wote wa Wakaldea wanaopigana nanyi na kunabaki tu katika mahema yao wale walioumizwa, hao watasimama na kuuteketeza muji huu kwa moto.


Yeremia anatiwa katika kifungo

11 Kundi la waaskari wa Wakaldea lilipoondoka Yerusalema kwa kulikimbia kundi la waaskari wa mufalme wa Misri lililokuwa linakaribia,

12 Yeremia aliondoka Yerusalema kwenda katika inchi ya Benjamina kwa kupokea sehemu ya urizi wake.

13 Alipokuwa katika mulango wa Benjamina, mulinzi mumoja anayeitwa Iria mwana wa Selemia, mujukuu wa Hanania, alimukamata Yeremia na kumwambia: Wewe unatoroka kusudi uende kujiunga na Wakaldea!

14 Yeremia akamwambia: Huo ni uongo! Mimi sitoroki na kwenda kujiunga na Wakaldea. Lakini Iria hakusadiki maneno ya Yeremia. Basi akamutia katika kifungo na kumupeleka kwa wakubwa.

15 Wakubwa hao walimukasirikia sana Yeremia wakamupiga, kisha wakamufunga katika kifungo katika nyumba ya katibu Yonatani iliyokuwa imegeuzwa kuwa gereza.

16 Yeremia alipokuwa amefungwa katika gereza kwa muda wa siku nyingi,

17 mufalme Zedekia alimwita na kumukaribisha kwake. Mufalme akamwuliza kwa siri wakiwa katika nyumba yake: Kuna neno lolote kutoka kwa Yawe? Yeremia akamujibu: Ndiyo, kuko. Kisha akaendelea kusema: Wewe utatiwa katika mikono ya mufalme wa Babeli.

18 Halafu Yeremia akamwuliza mufalme Zedekia: Nimekukosea nini, au nimewakosea nini watumishi wako au watu hawa, hata unitie katika kifungo?

19 Wako wapi manabii waliokutabiria wakisema: Mufalme wa Babeli hatakushambulia wewe wala inchi hii?

20 Sasa ninakuomba unisikilize, ee bwana wangu mufalme. Ninakusihi sana ulikubali ombi langu. Tafazali usinirudishe tena katika kifungo katika nyumba ya katibu Yonatani, nisipate kukufia humo.

21 Basi, mufalme Zedekia akatoa amri Yeremia awekwe katika chumba cha walinzi na kupewa mukate kila siku kutoka kwa wapikaji wa mukate mpaka mikate ilipotoweka kabisa huko katika muji. Basi, Yeremia alibaki katika chumba cha walinzi.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan