Yeremia 34 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ujumbe kwa Zedekia 1 Yawe akamutolea Yeremia ujumbe huu wakati Nebukadneza, mufalme wa Babeli, pamoja na waaskari wake wote na falme zote za dunia zilizokuwa chini ya utawala wake, vilevile na watu wote walipokuwa wakiushambulia Yerusalema na miji mingine yote ya kandokando yake: 2 Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kwenda usemezane na Zedekia, mufalme wa Yuda. Umwambie kwamba mimi Yawe ninasema hivi: Nimeutia muji huu katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atauteketeza kwa moto. 3 Nawe hautatoroka toka mikono yake, lakini kwa hakika utatekwa na kupelekwa kwake; utaonana na mufalme wa Babeli macho kwa macho, na kusema naye kinywa kwa kinywa; kisha, utakwenda Babeli. 4 Lakini, ewe Zedekia, mufalme wa Yuda, sikia ujumbe wa Yawe. Yawe anasema hivi juu yako: Wewe hautauawa kwa upanga katika vita. 5 Utakufa kwa amani. Na kama vile watu walivyochoma ubani walipowazika babu zako waliokuwa wafalme, ndivyo watakavyokuchomea ubani na kuomboleza wakisema: Masikini! Mufalme wetu amekufa! –Ni ujumbe wa Yawe. 6 Kisha, nabii Yeremia akamwelezea Zedekia, mufalme wa Yuda, maneno hayo yote huko Yerusalema, 7 wakati waaskari wa mufalme wa Babeli walipokuwa wanaushambulia Yerusalema na vilevile miji ya Lakisi na Azeka, ambayo ilikuwa miji pekee iliyobaki ikizungukwa na kuta. Uhuru wa muda wa watumwa 8 Huu ndio ujumbe uliotolewa kwa Yeremia kutoka kwa Yawe kisha mufalme Zedekia kufanya agano na watu wote wa Yerusalema kuwaachilia huru 9 watumwa na wajakazi wao wa Kiebrania, kusudi mutu yeyote asimufanye Muyuda mwenzake kuwa mutumwa. 10 Wakubwa wote na watu wote waliofanya agano hilo walikubaliana wote wawaachilie huru watumwa wao na wajakazi, na mutu yeyote asiwafanye tena kuwa watumwa. Walikubaliana, wakawaacha huru. 11 Lakini kisha walibadilisha nia zao, wakawashika tena watumwa na wajakazi hao ambao walikuwa wamewaacha huru, wakawafanya watumwa. 12 Halafu neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: 13 Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nilifanya agano na babu zenu nilipowatoa toka inchi ya Misri ambako walikuwa watumwa, nikawaambia: 14 Kila mwaka wa saba, kila mumoja wenu atamwachilia huru ndugu yake Muyuda aliyeuzishwa kuwa mutumwa kwa muda wa miaka sita. Munapaswa kuwaachilia huru, wasiwatumikie tena. Lakini babu zenu hawakunisikiliza wala kunitegea sikio. 15 Hivi karibu siku hizi ninyi mulibadilika, mukafanya mambo yanayokuwa sawa mbele yangu, mukawaachilia huru Waisraeli wenzenu na kufanya agano mbele yangu katika nyumba yangu. 16 Lakini muligeuka, mukachafua jina langu, wakati mulipowakamata tena watumwa na wajakazi walewale ambao mulikuwa mumewaachilia kama walivyotaka, mukawalazimisha kuwa watumwa tena. 17 Kwa hiyo, Yawe anasema hivi: Ninyi hamukunitii juu ya kuwapatia wandugu zenu Waisraeli uhuru. Basi, nami vilevile nitawapatia ninyi uhuru: uhuru wa kuuawa kwa upanga katika vita, kuuawa kwa ugonjwa mukali na kwa njaa. Nitawafanya ninyi kuwa kitambulisho cha kuogopesha kwa falme zote katika dunia. 18 Watu waliovunja agano langu na kukataa kufuata masharti ya agano walilofanya mbele yangu, nitawafanya kama yule mwana-ngombe waliyemukata sehemu mbili na kupita katikati ya vipande vile. 19 Watu hao ndio hao wakubwa wa inchi ya Yuda, wakubwa wa muji Yerusalema, matowashi wa mufalme, makuhani, pamoja na wanainchi wote waliopita katikati ya sehemu mbili za yule mwana-ngombe. 20 Watatiwa katika mikono ya waadui zao, na katika mikono ya watu wanaotaka kuwaua. Maiti zao zitakuliwa na ndege na nyama wa pori. 21 Naye Zedekia, mufalme wa Yuda, pamoja na wakubwa wake, nitawatia katika mikono ya waadui zao, na katika mikono ya watu wanaotaka kuwaua; ni kusema katika mikono ya waaskari wa mufalme wa Babeli ambao wameondoka na kuacha kuwashambulia. 22 Nitawaamuru nao wataurudia katika muji huu. Wataushambulia, watauteka na kuuteketeza kwa moto. Nitaifanya miji ya inchi ya Yuda kuwa ukiwa bila wakaaji. –Ni ujumbe wa Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo