Yeremia 32 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yeremia ananunua shamba 1 Yawe akamutolea Yeremia ujumbe katika mwaka wa kumi wa utawala wa Zedekia mufalme wa Yuda, ambao ulikuwa mwaka wa kumi na nane wa utawala wa Nebukadneza. 2 Wakati huo, waaskari wa mufalme wa Babeli walikuwa wakizunguka Yerusalema kwa vita, naye nabii Yeremia alikuwa amefungwa katika baraza la walinzi uliokuwa ndani ya nyumba ya mufalme wa Yuda. 3 Maana Zedekia, mufalme wa Yuda, alikuwa amemufunga Yeremia akisema: Kwa nini unatabiri na kusema: Yawe anasema hivi: Mimi ninautia muji huu katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atauteka. 4 Zedekia, mufalme wa Yuda, hataepuka kutiwa katika mikono ya Wakaldea; hakika atatekwa na mufalme wa Babeli, ataonana naye uso kwa uso na kuongea naye kinywa kwa kinywa. 5 Zedekia atapelekwa mpaka Babeli, naye atakaa huko mpaka nitakapomushugulikia. –Ni ujumbe wa Yawe.– Kama mukipigana na Wakaldea, hamutawashinda. 6 Yeremia akasema: Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: 7 Hanameli mwana wa baba yako mudogo Salumu atakuja kwako na kusema: Nunua shamba langu linalokuwa kule Anatoti, maana wewe ni ndugu yangu kabisa, nawe uko na haki ya kulikomboa. 8 Kisha binamu yangu Hanameli akanifikia katika baraza la walinzi kama alivyonifahamisha Yawe, akaniambia: Nunua shamba langu linalokuwa kule Anatoti katika inchi ya Benjamina maana wewe uko na haki ya kulikomboa. Ulinunue kwa faida yako. Basi nikajua kwamba neno hili ni la Yawe. 9 Nikalinunua shamba hilo linalokuwa kule Anatoti, kutoka kwa binamu yangu Hanameli, nikamulipa bei yake vikoroti kumi na saba vya feza. 10 Nikatia sahihi juu ya barua ya ununuzi, nikaipiga muhuri, nikawaita washuhuda na kuipima ile feza juu ya mizani. 11 Kisha, nikakamata ile barua ya ununuzi niliyoipiga muhuri, ambayo ilikuwa na masharti na kanuni, pamoja na barua ingine iliyokuwa wazi. 12 Nilimupa Baruku mwana wa Neria mujukuu wa Masea ile barua ya ununuzi mbele ya binamu yangu Hanameli na washuhuda waliokuwa wametia sahihi juu ya barua ya ununuzi, na mbele ya Wayuda wote waliokuwa wameikaa katika baraza la walinzi. 13 Mbele ya watu wote hao, nikamupa Baruku maagizo haya: 14 Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Twaa barua hizi zote mbili, barua hii ya ununuzi wa shamba iliyotiwa sahihi, na hii ingine inayokuwa wazi, uziweke katika chungu cha udongo kusudi zipate kulindwa kwa muda murefu. 15 Maana Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Nyumba na mashamba, pamoja na mashamba ya mizabibu katika inchi hii yatanunuliwa tena. 16 Kisha kumupatia Baruku mwana wa Neria barua ya ununuzi wa shamba, nilimwomba Yawe nikisema: 17 Ee Bwana wangu Yawe, ni wewe ambaye kwa nguvu zako nyingi na uwezo wako mukubwa, umeziumba mbingu na dunia. 18 Wewe unaonyesha mema yako kwa maelfu ya watu; lakini unawaazibu vilevile watu kwa sababu ya zambi za babu zao. Wewe ni Mungu Mukubwa, mwenye nguvu, Yawe wa majeshi ndilo jina lako. 19 Wewe unapanga kwa hekima na unafanya maajabu; njia za watu wote ziko wazi mbele yako, unamulipa kila mumoja kadiri ya njia zake na matendo yake. 20 Katika inchi ya Misri ulifanya maajabu, ukatenda miujiza, na unaendelea kufanya hivyo mpaka leo kati ya Waisraeli na katika mataifa mengine vilevile, jambo ambalo limekufanya ujulikane kila nafasi. 21 Kwa maajabu na miujiza uliyowatisha nayo Wamisri, uliwatoa watu wako Misri kwa nguvu zako nyingi na uwezo wako mukubwa. 22 Uliwapa inchi hii ambayo uliahidi kuwapa babu zao, inchi inayotiririka maziwa na asali. 23 Nao walifika, wakaitwaa na kuirizi. Lakini wao hawakukusikiliza, wala hawakufuata sheria zako. Hawakutenda mambo uliyoamuru. Ndiyo maana utawafanya wapatwe na hasara hii. 24 Angalia, Wakaldea wamechimba mifereji kuuzunguka muji; wanauzunguka kusudi wapate kuuteka; wanaushambulia. Vita, njaa na magonjwa vitaufanya muji utekwe na watu hao. Kweli mambo uliyotabiri yametokea. Unaona mwenyewe. 25 Lakini, ee Bwana wangu Yawe, wewe ndiwe uliyeniambia: “Nunua shamba kwa feza na kuweka washuhuda”, ingawa muji wenyewe umetekwa na Wakaldea. 26 Neno la Yawe lilimufikia Yeremia kusema hivi: 27 Mimi ni Yawe, Mungu wa watu wote. Hakuna lolote linaloweza kunishinda. 28 Yawe anasema hivi: Kwa hiyo, ninautoa muji huu kwa Wakaldea na kwa Nebukadneza mufalme wa Babeli, naye atauteka. 29 Wakaldea wanaoushambulia muji huu wataingia na kuuteketeza kwa moto; watauteketeza pamoja na nyumba ambazo juu ya paa zake ubani ulifukiziwa kwa mungu Bali na sadaka za divai zilitolewa kwa miungu mingine, kwa kunichokoza. 30 Maana Waisraeli na watu wa Yuda hawakufanya chochote mbele yangu isipokuwa uovu tangu ujana wao; watu wa Israeli hawakufanya chochote isipokuwa kunikasirikisha kwa matendo yao. –Ni ujumbe wa Yawe.– 31 Muji huu umechochea hasira yangu na kuniuzi tangu siku ulipojengwa mpaka leo hii. Kwa hiyo, nitauondoa kabisa mbele yangu, 32 kwa sababu ya uovu wote watu wa Israeli na Wayuda waliotenda, pamoja na wafalme na wakubwa wao, makuhani na manabii wao, na wakaaji wa Yerusalema. 33 Wao walinigeuzia mugongo pahali pa kunigeuzia nyuso zao; ingawa nimewafundisha tena na tena, wao hawakusikiliza na kuyapokea mafundisho yangu. 34 Waliweka sanamu za miungu yao ya kuchukiza katika nyumba hii inayojulikana kwa jina langu, wakaichafua. 35 Walimujengea mungu Bali mazabahu katika bonde la Mwana wa Hinomu, kusudi wamutolee mungu Moleki wana wao na wabinti zao, ingawa sikuwaamuru wala sikufikiria kwamba wangefanya hivyo. Wakasukuma watu wa Yuda watende zambi. Ahadi yenye tumaini 36 Sasa basi, Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Yeremia, watu hawa wanasema kwamba, kwa vita, njaa na magonjwa, muji huu utatiwa katika mikono ya mufalme wa Babeli. Lakini ninasema: 37 Nitawakusanya watu kutoka inchi zote ambako kwa hasira na kasirani na chuki yangu kubwa, niliwatawanya. Nitawarudisha tena hapa, na kuwafanya wakae salama. 38 Nao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao. 39 Nitawapa moyo mumoja na nia moja, wapate kuniheshimu mimi siku zote, kwa faida yao wenyewe na kwa faida ya watoto wao watakaofuata. 40 Nitafanya nao agano la milele, kwamba sitaacha kuwatendea mema hata kidogo; nitaweka ndani ya mioyo yao utii kwa ajili yangu kusudi wasiniache tena. 41 Nitafurahi kuwatendea mema; nitawasimika siku zote katika inchi hii na kuwatendea kwa uaminifu. 42 Yawe anasema hivi: Kama nilivyowaletea hasara watu hawa, ndivyo nitakavyowaletea mema niliyowaahidi. 43 Mashamba yatanunuliwa katika inchi hii ambayo unasema imekuwa ukiwa bila watu wala nyama, na kwamba imetolewa kwa Wakaldea. 44 Watu watanunua mashamba kwa feza, watazitia sahihi barua zake za ununuzi, watazipiga muhuri, na kuweka washuhuda katika inchi ya Benjamina, kandokando ya Yerusalema, katika miji ya Yuda, katika miji ya inchi ya milima, katika miji ya Shefela, na katika miji ya jangwa la Negebu. Maana nitawastawisha tena. –Ni ujumbe wa Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo