Yeremia 30 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Hili ni neno lililomufikia Yeremia kutoka Yawe: 2 Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Andika katika kitabu maneno yote ninayokuambia. 3 Maana, siku zinakuja ambapo nitatengeneza upya maisha ya watu wangu wa Israeli na Yuda. –Ni Yawe anayesema.– Nitawarudisha katika inchi niliyowapa babu zao, nao watairizi. 4 Haya ndiyo mambo aliyosema Yawe juu ya watu wa Israeli na Yuda: 5 Yawe anasema hivi: Kumesikilika kilio cha hofu, kweli ni sauti ya kutisha wala si ya amani. 6 Mujiulize sasa na kufahamu: Mwanaume anaweza kuzaa mutoto? Mbona basi, ninamwona kila mwanaume anajikamata kwenye kiuno kama mwanamuke anayesikia maumivu ya kuzaa na nyuso zimebadilika? 7 Kweli, siku hiyo ni kubwa, hakuna ingine kama hiyo; ni siku ya taabu kwa watu wa Yakobo; hata hivyo, wataokolewa toka humo. 8 Siku hiyo itakapofika, nitaivunja nira inayofungiwa katika shingo lao na kukata minyororo yao. 9 Nao hawatakuwa tena watumwa wa wageni, lakini watanitumikia mimi Yawe, Mungu wao pamoja na mufalme wa ukoo wa Daudi ambaye nitakayewasimikia. 10 Usiogope ee Yakobo, mutumishi wangu, wala usifazaike, ee Israeli. –Ni ujumbe wa Yawe.– Maana nitakuokoa toka huko mbali unapokuwa, nitawaokoa wazao wako kutoka katika uhamisho. Utarudi na kuishi kwa amani, wala hakuna mutu atakayekuogopesha. 11 Maana mimi niko pamoja nawe, nipate kukuokoa. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitayaangamiza kabisa mataifa yote, ambayo niliyokusambaza kati yao; lakini sitakuangamiza wewe kabisa. Nitakuazibu kadiri unavyostahili wala sitakuachilia uende bila kukuazibu. –Ni ujumbe wa Yawe. 12 Yawe anasema hivi: Mapigo yako hayaponi, vidonda vyako haviwezi kutunzwa. 13 Hakuna atakayekushugulikia, kidonda chako hakina dawa, wewe hautapona. 14 Wapenzi wako wote wamekusahau; hawajali kitu chochote juu yako. Nimekupiga sawa vile ungekuwa adui yangu. Umeazibiwa bila huruma, kwa sababu kosa lako ni kubwa, zambi zako ni nyingi sana. 15 Kwa nini unalia kwa ajili ya kidonda chako? Maumivu yako hayawezi kupona. Nimekutendea hayo yote, kwa sababu kosa lako ni kubwa, zambi zako ni nyingi sana. 16 Lakini wote wanaokuangamiza, wataangamizwa vilevile, na waadui zako wote watapelekwa katika uhamisho; nao wanaokukamata mateka watakamatwa mateka, nao wanaokuwinda, nitawawinda. 17 Sasa wanakuita wewe Sayuni: “Aliyetupiliwa”, “Muji usioshugulikiwa na mutu”. Lakini nitakurudishia afya yako, nitaponyesha vidonda vyako. –Ni ujumbe wa Yawe. 18 Yawe anasema hivi: Nitatengeneza upya maisha ya jamaa za wazao wa Yakobo, nitayaonea makao yao huruma; muji wao utajengwa upya kwenye mabomoko yake, nyumba ya kifalme itasimama pahali ilipokuwa mbele. 19 Humo mutasikilika nyimbo za shukrani nayo makelele ya wenye kufanya sherehe. Nitawaongeza wala hawatakuwa wachache; nitawafanya waheshimiwe wala hawatazarauliwa. 20 Watoto wao watakuwa kama walivyokuwa zamani, nayo makundi yatasimama imara mbele yangu, nami nitawaazibu wote wanaowagandamiza. 21 Mwongozi wao atakuwa mumoja wao, mutawala wao atatokea katikati yao. Nitamuruhusu kuwa karibu nami; maana, ni nani anayeweza kusubutu kuhatarisha uzima wake kwa kunikaribia? –Ni ujumbe wa Yawe.– 22 Mutakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. 23 Angalia, zoruba kali kutoka kwa Yawe! Kasirani yake imeamuka, upepo mukali utapiga kichwa cha mwovu. 24 Hasira ya Yawe haitatulia, mpaka atakapotimiza na kukamilisha mapenzi ya moyo wake. Kutakuja siku ambazo mutaelewa vema mambo hayo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo